Jumatatu, Juni 10, 2013

SIMULIZI...BADO MIMI....SURA YA .....20.......

 ILIPOISHIA
Ngozi ya mwili wake ilionekana kubadilika katika upande mmoja wa mwili wake ilionekana kuwa na ngozi ya ajabu kama magamaba ya nyoka, ilikuwa ni ngozi ya kutisha sana, niliogopa na kutetemeka huku nikiwa kama nataka nitimue mbio, Mama Bilionea aliniita “Usiogope Kandida naomba uketi unisikilize mwanangu”  Nilisogea huku nikiwa siamini kile ninachokiona “Mama Bilionea umepatwa na kitu gani, mbona ngozi yako inabadilika”.Yaani nilikuwa nahisi kama nataka kuzimia kwasababu sikujua ni kitu gani kinataka kutokea kwa muda ule. JE NINI KITAENDELEA USIKOSE SURA YA......20.....

INAPOENDELEA
Nilijisogeza kwambali kidogo, huku nikiwa na jikunyata kwa kuogopa kile nilichokuwa nakiona. Mama Bilionea kwa sauti ya upole akasema “Kandida wakati wangu umefika, narudi nyumbani kwa Mama yangu Bibi Bilionea, naimani utathamini nakuenzi hekalu la Bilionea siku zote za maisha yako, naomba uchukue huu mfuko” Huku akiwa ananionyesha mfuko mkubwa uliokuwa na rangi nyekundu akaniambia humo ndani kuna vitambaa vingi sana na mikufu ya rangi nyekundu. Lakini pia kuna kitabu ambacho kitakusaidia kukuongoza katika kukamilisha kazi za Bilionea, Maisha yako yatakuwa mazuri sana,  kama tu utafuata masharti yalipo katika kitabu”.

 Sikuamini kile nilichokuwa nakisikia inamaana Mama Bilionea alikuwa ananirithisha mikoba yake. “Lakini Mama sintoweza kumtoa kafara mtu yeyote nakuomba usiniachie mimi tafadhali, niruhusu tu niondoke.” Mama Bilionea alikohoa kidogo na kusema “Hapana haiwezekani, wewe tayari jina lako lipo katika hekalu la Bilionea na tayari ulishasaini mkataba kwa kutoa kafara ya Baba yako ni vigumu kutoka katika maisha ya Bilionea labda uwe umekufa” Akiwa anaendelea kuzungumza hali yake ilizidi kuwa mbaya.

Nilikuwa naogopa sana kwa jinsi Mama Bilionea alivyokuwa akibadilika, huku akiwa anaendelea kusema “Kandida kitambaa na  mkufu utakuwa unampa mtu ambaye umeoteshwa kuwa tunahitaji kafara kutoka kwake, usiogope siyo kila wakati  utatoa kafara ni mpaka atakapokuambia Bibi Bilionea na pia yeyote atakayeniulizia mwambie nilihamia nje ya nchi. Kwani mwili wangu hautoonekana, nakutakia maisha mema Kandida” Nilikuwa bado sijielewi nikahisi labda naota lakini haikuwa ndoto “Mama Bilionea Mimi sintoweza kabisa kufanya hivyo tafadhali nakuomba uniruhusu niondoke.”


 Nilikuwa naongea huku nikiwa nimetizama pembeni kwani nilikuwa naogopa kumuangalia Mama Bilionea pale kitandani. kumbe masikini nilikuwa naongea peke yangu, Nilipojaribu kugeuka tu sikumuona tena Mama Bilionea pale kitandani "Mungu wangu! Inamaana Mama Bilionea ametoweka, maajabu gani haya jamani, na je huu mfuko wake mimi nitaupeleka wapi? Siwezi mimi, Eeeh Mungu wangu nisaidie." 

Sikuamini macho yango kwani Mama Bilionea alikuwa ametoweka. Nilikuwa kama nimechanganyikiwa nilitoka pale chumbani bila ya kugusa kitu chochote.Mfuko alionipa Mama Bilionea sikuuuchukua niliuacha na kufunga mlango kwa nguvu. Huku nikiwa natizama huku na kule  nikiwa nataka kukimbia nilisikia sauti ya Renata "Dada Kandida, Dada" Niliendelea kupepesa macho bila hata ya kuitika ilimbidi Renata anivute gauni nililokuwa nimevaa huku akiniita kwa nguvu "Dada, Dada, , unashangaa nini? Mama Bilionea yuko wapi?".Nilimtizama mdogo wangu na kumshika mkono kisha nikaenda naye chumbani,sikumjibu kitu chochote pamoja na maswali yote aliyokuwa ananiuliza.Mawazo yangu yote nilikuwa nawaza niondoke katika ile nyumba ya Mama Bilionea.

Wakati huu  sikutaka kupoteza muda nilitamani niondoke muda ule lakini ilikuwa ni usiku sana. Renata alinitizama na kusema "Dada mbona umeniacha kitandani peke yangu, ulikuwa wapi, au ulienda kulala chumbani kwa Mama Bilionea" Alikuwa anaongea Renata huku mimi nikiwa bado na wasiwasi na kwasababu Renata alikuwa ni mdogo nilishindwa kumueleza chochote. Nilichokifanya nilichukua begi langu nakuanza kukunja nguo ili ikifika tu asubuhi na mapema niwachukue wadogo zangu tuondoke.

Moyoni mwangu nilikuwa nawaza "Sijawahi kuona maajabu kama haya tokea nizaliwe katika hii dunia, Yaani mimi Maisha yangu yapo mikononi mwa shetani, nawezaje kutoka huku jamani, Siwezi kufanya yale aliyoniambia Mama Bilionea. Sina budi kuondoka kabisa katika hii nyumba, vinginevyo familia yangu itaangamia.Renata alikuwa akinishangaa na baadaye alipanda kitandani na kulala fofofo, Mimi sikulala kabisa siku hiyo nilikuwa nawaza kupambazuke tuondoke.

Kesho yake asubuhi na mapema niliwachukua wadogo zangu na kuwaambia kuwa tunasafiri, kwenda kumfuata Mama Bilionea. Walikuwa wakiniuliza maswali mengi sana huku wakitaka kujua Mama Bilionea yuko wapi. Nilitoka nje na kumtaarifu mlinzi kuwa nasafiri ili asinitafute wakati tukiwa tunaelekea barabarani kutafuta usafiri wa taksi tulikutana na kikundi cha watu wakiwa wanaimba na kusali pamoja huku  mchungaji akitamka maneno haya "Mungu ni kila kitu, katika Maisha ya mwanadamu, mpokee Mungu leo atakutoa katika giza, Maisha mazuri ni kwa Mungu, Mateso yote uliyonayo Mungu atakusaidia Mpokee Mungu leo atakutoa katika shimo la wachawi, shimo  la dhambi".

 Nilipokuwa nasikiliza yale maneno yaliniingia sana akilini, nilihisi yule mchungaji ananizungumzia mimi, niliguswa sana nakuamua kusogea mpaka pale walipokuwa wanafanya maombi.Nilipofika yule mchungaji alipomaliza maombi alinifuata na kusema "Unaonekana unamatatizo makubwa sana Binti yangu" Nilimtizama kwa macho yaliyoonyesha huzuni "Ni kweli kabisa mchungaji naomba unisaidie".

 Yule mchungaji alinisogeza pembeni nikamsimulia mkasa mzima bila kuficha chochote. Alisikitika sana na kusema "Hapana Kandida siyo lazima utoke katika nyumba uliyokuwa unaishi, kwani unatakiwa kumshukuru Mungu na kuomba sana unaweza kusali na kuibariki nyumba ikawa mahali patakatifu" Nilikuwa namsikiliza yule mchungaji kwa umakini sana baadaye alinitaka turudi kule kwa Mama Bilionea ili aende kufanya maombi na kuibariki ile nyumba.Binafsi nilikuwa naogopa kabisa kuishi katika ile nyumba. Lakini kutokana na ushauri wa mchungaji niliona bora nimpeleke anaweza kutusaidia.JE NINI KITAENDELEA....USIKOSE SURA YA ....21 SIKU YA ALHAMISI.... KWANI MAMBO NDIYO KWANZA YANAANZA...NINI HATIMA YA MAISHA YA KANDIDA....KESHO USIKOSE SIMULIZI YA HAKUNA SIRI
 

Maoni 8 :

Bila jina alisema ...

majangaaaa

Bila jina alisema ...

mhhhhhhhhhh sasa hapo mapambano yanahanza uwiiiiiiiiii inanogaje kila cku?ongera dada Adela jmn,nimejarib kukuad fb huna marafk wengi swz.

Bila jina alisema ...

Nice story my sister.

Bila jina alisema ...

Nice story my sister.

Bila jina alisema ...

nice

Unknown alisema ...

Hapo sasa

Bila jina alisema ...

Aisee! Pole zake kandida

Bila jina alisema ...

Duuu! Kazi ipo.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom