Jumatatu, Julai 22, 2013

SIMULIZI YA ...BADO MIMI...SEHEMU YA ....28......



 ILIPOISHIA
Nilikuwa nawaza huku Renata akinitikisa mkono kwa nguvu na kunivuta “Dada twende tukamtafute Tumaini, twende dada” Wakati huo Charito alikuwa amesimama pembeni na kusema “Inawezekanaje mlinzi alikuwepo hapa getini halafu mtoto anakimbia anashindwa kumrudisha, sasa atakuwa amekimbilia wapi, si unajua Dar es salaam ni kubwa” Alisema Charito huku akiwa anaelekea kumtafuta mlinzi na mimi nikawaza kuwa hawezekani Tumaini akawa ameenda  sehemu ya mbali labda atakuwa maeneo ya karibu, haraka nilitoka nje na kuanza kuwauliza majirani JE NINI KITAENDELEA USIKOSE...... SEHEMU YA........28.........

INAPOENDELEA
Nilizunguka huku na kule kumtafuta Tumaini bila ya mafanikio. kwani kila jirani nileyekuwa nikimuulizaa alisema hakumuona Tumaini.Nilikuwa na mawazo sana huku nikiwa na hisia labda Tumaini anaweza kupotea kabisa au hata kugongwa na gari.Wazo la kwenda kuripoti kituo cha polisi sikuwa nalo kabisa kichwani niliendelea kuzunguka huku na kule na machozi yalikuwa yakinilengalenga kutokana na hofu ya kuwa naweza nisimpate mdogo wangu.
 
Kwa wakati huo mume wangu naye alikuwa akizunguka kumtafuta Tumaini.Yalipita masaa kama matatu huku tukimtafuta Tumaini bila ya mafanikio ilinibidi nirudi nyumbani huku mawazo yangu yakinipelekea kuwa yawezekana Tumaini akarudi mwenyewe.

Nilipofika nyumbani nilimkuta mume wangu  akiwa ameketi sebuleni pamoja na Renata "Vipi jamani, inamaana Tumaini hajarudi nyumbani" Charito alinitizama na kusema "Nimehangaika sana kumtafuta huku na kule bila ya mafanikio nilifikiri labda wewe utakuwa umempata, sasa sijui atakuwa ameelekea wapi" Wakati Charito akiwa anazungumza Renata alimtizama Charito  na kusema kwa sauti iliyojaa hasira kali "Wewe shemeji unajua wapi ameenda Tumaini, sema yuko wapi mdogo wangu?".


 Nilibaki nashangaa kwa namna ambavyo Renata alikuwa akiongea  kana kwamba Charito anajua alipo Tumaini. "Hee! Renata! Ni tabia gani hiyo umeanza, unawezaje kuongea na shemeji yako kwa sauti kali hivyo". Charito alimtizama Renata na kisha akanigeukia na kusema "Hapana mke wangu usimkaripie mtoto, kwani huyu  bado ni mdogo na pia fahamu bado tunamtafuta Tumaini, haileti maana kuanza kugombana hapa.

Renata alinyanyuka kwa hasira  na kusema  "Mimi ni mdogo, lakini najua kila kitu wewe shemeji siyo mtu mzuri unataka kutuuwa wote, nashangaa kwanini Dada Kandida hutaki kunielewa, tizama sasa Tumaini yuko wapi?" Aliongea Renata huku akiwa anaelekea chumbani kwake, na kumuacha Kandida na Charito wakiwa wanashangaa namna ambavyo Renata alikuwa na ujasiri  wa kuzungumza bila ya kuogopa chochote. "Unajua, huyu mtoto sijawahi kumpiga, yaani ipo siku nitamchapa hadi achanganyikiwe" Aliongea Kandida huku Charito akitabasamu na kusema "Hapana mke wangu usiwe na hasira kiasi hicho."

Renata akiwa chumbani, ndani ya kabati lake la nguo alisikia kama kitu kikiwa kinagongagonga. Alishutuka na kusema "Mungu wangu, ni nini hicho, nani huyo, eeh kuna nini?...Dada  Kandida, daadaaaa" Aliita kwa sauti kali sana. Kwa haraka Kandida aliinuka na kuelekea chumbani "Nini wewe jamani, kuna nini tena, mbona unapiga kelele" Renata alikuwa akiongea huku anatetemeka na kusema "Dada kuna kitu kipo kwenye kabati" Kandida alisogea na kufungua kabati "Mungu wangu, Tumaini, unafanya nini huku jamani" Alikuwa ni Tumaini ambaye alikuwa amejifungia ndani ya kabati huku akiwa amejikunyata mithili ya mtu aliyekuwa anasikia baridi kali sana. "Dada Kandida, kuna mtoto ananikimbiza, mtoto mdogo anataka kuniua".

 Aliongea Tumaini huku akionekana kuwa na hofu sana "Hee! Mtoto, yuko wapi? na kwanini anakukimbiza" Alihoji Kandida huku Renata aliyekuwa pembeni akasema "Siyo mtoto, ni kibwengo, hicho kimetumwa na shemeji hata mimi nilishakiona" Nilimgeukia Renata na kusema "Funga bakuli lako, mjinga mkubwa unaona mwenzako analia halafu unaongea vitu vya ajabu toka hapo". Siku zote nilikuwa siamini chochote alichokuwa akizungumza Kandida lakini baada ya kumtoa Tumaini ndani ya kabati, nilirudi na kuketi sebuleni ambapo, sikumkuta Charito alikuwa ametoka. Nilibaki nikiwa natafakari peke yangu "Hivii, hii nyumba ina kitu gani? Mbona yanatokea mambo ya ajabu sana, siku hizi Renata anaongea mambo amabayo simuelewi, lakini pia Tumaini ameanza kuona vitu vya ajabu, sijui kuna nini jamani eeh Mungu tusaidie".

Baadaye Charito alirudi na nilimsimulia hali halisi na kile alichokiona Tumaini. Alibaki akiwa anashangaa "Haiwezekani mmmh mambo gani haya itabidi tuende kuonana na mchungaji" Alisema Charito huku akiwa ananitizama.Tulikubaliana ni vyema kwenda kuonana na Mchungaji Mkombozi ili aweze kutusaidia. Binafsi nilikuwa na hofu zaidi kutokana na  ujauzito niliokuwa nao. Baada ya mwezi mmoja tukiwa tunaendelea na maisha. Siku moja mume wangu alikuja akiwa amebeba chupa ya juisi amabapo alifika na kunimiminia kwenye kikombe kisha alinipa "Mke wangu hii juisi ni nzuri sana  kwa hali yako kwani inasaidia kuongeza damu mwili, si unajua, Mama mjamzito anatakiwa kuwa na damu nyingi"Charito alizungumza huku akitabasamu.Nilikunywa ile juisi yote ilikuwa na harufu nzuri sana ya zabibu. Kila siku Charito alikuwa akiniletea juisi.

Ilipita kama wiki moja, siku hiyo nilikuwa nimepumzika peke yangu, huku nikiwa natizama tamthilia. Ghafla tumbo lilianza kuniuma sana "Mama yangu, uwiiii, aaaah aaaah , Mamaaaaa, mbona tumbo linauma hivi. Eeeh Mungu wangu, maumivu yanzidi." Yaani nilikuwa nasikia maumivu makali sana, pale nyumbani kulikuwa hakuna mtu zaidi ya mdogo wangu Renata. Maumivu yalinizidi hatimaye damu zikaanza kunitoka kwa wingi, niliogopa huku nikilia kwa uchungu. Renata alikuja na kunishika huku akipiga kelele kuomba msaada. Majirani walikuja na kunibeba haraka kunikimbiza hospitalini. JE ...NINI KITAENDELEA USIKOSE...SEHEMU YA ...29...


Maoni 7 :

Bila jina alisema ...

kadinda natamn nimnase vibao,yn naomba wadgo zake wasife life yy mjinga kbsa,charito kashampa mivtu ya ajabu.

Bila jina alisema ...

Kufa 2 tule wali maana hamna jinsi kwa sababu hutaki kuckia ushauri wa mdogo wako renata

Bila jina alisema ...

Tatizo lake kandida ni kumpuuza sana mdogo wake renata. ngoja akome ndo ajifunze maana ya ushauri ni nini. huyo ni wa kuzabuliwa mabanzi ili ajifunze.

Bila jina alisema ...

Maiweeeeee,! kandida lazima aporomoshe mimba yake 2

Bila jina alisema ...

Tobaaaa,! yamekuwa hayo tena! pole sana kandida kwa majaribu hayo. lkn hii yote ni kwa 7bu hutaki kuambiwa na mdogo wako renata. jaribu kuwa unamsikiliza hata kama ni mdogo.

Bila jina alisema ...

Vipi mamy hii hadithi huiendelezi tena? Mana nimuda tangu u stop...

Bila jina alisema ...

Vipi dear hii story mbona huiendelezi tena?

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom