Jumatatu, Agosti 05, 2013

SIMULIZI FUPI 'NDUGU LAWAMA"


SIMULIZI FUPI_ NDUGU LAWAMA
MTUNZI _ADELA DALLY KAVISHE

"Asante sana shemeji Beni kwa msaada ulionipa, lakini nilikuwa naomba uniongezee kiasi cha shilingi laki tano tu, kuna jambo nataka kulifanya, nimepungukiwa kidogo, naimani utanisaidia". Alikuwa ni shemeji yangu ambaye ni kwa kipindi kirefu nimekuwa nikimsaidia kuendeleza biashara zake,  kwa wakati huo nilikuwa sina kiasi  hicho cha fedha "Ningependa kukusaidia shemeji lakini hali yangu kiuchumi kwa sasa imeyumba ila usiwe na shaka nitafanya mikakati ndani ya siku mbili tatu nitakupa hiyo pesa.lakini shemeji kuwa makini sana na utumiaji  wa pesa kwani kwa sasa pesa imekuwa ngumu kupatikana hivyo ni vyema ukawa makini sana katika biashara yako". Baada ya kumaliza mazungumzo shemeji alinielewa na kuondoka.

Kesho yake asubuhi ilikuwa ni siku ya jumamosi ambapo siku hiyo si kwenda kazini, alikuja dada yangu akiwa pamoja na mtoto wake mdogo wa kike.  "Habari za masiku dada, karibu sana" Dada alinitizama huku akisema "Kaka habari yangu si njema kwani hapa nilipo, nimekuja kwako nina shida  mtoto amerudishwa nyumbani kwasababu ya anadaiwa ada, sasa kaka naomba unisaidie shilingi laki tatu niweze kumrudisha  mjomba wako shule, yaani hapa nilipo sina mtu mwingine wa kumtegemea zaidi yako". 

Nilikuwa nimeketi  pale sebuleni huku nikiwaza na nafsi yangu "Mhhh hapa nilipo leo nimeamka nina shilingi elfu kumi na tano tu mfukoni mwangu sasa nitawezaje kumsaidia dada yangu" Nilimtizama dada na kusema "Daah, hali ni mbaya sana dada yangu, umenikuta sina pesa kabisa lakini embu subiri naweza kumkopa rafiki yangu kiasi hicho cha pesa ili mtoto aende shule." Nilimpigia simu rafiki yangu anaitwa Zuberi na kumuomba anikopeshe pesa kidogo, kwa bahati nzuri nilifanikiwa hivyo nilimpa kiasi kile cha fedha dada.

Baada ya dada yangu kuondoka mke wangu alikuja  akiwa ametoka sokoni "Mume wangu imekuwa ni vizuri nimekukuta kwani mama amenipigia simu alikuwa anataka kuongea na wewe" Basi moja kwa moja mke wangu akampigia simu Mama mkwe wangu  kisha akanipa simu niongee naye. "Shikamoo Mama habari za hapo nyumbani" Mama aliitika kwa sauti ya unyonge "Habari si njema mwanangu  mwili unaniuma sana, halafu sina pesa kabisa, naomba unitumie hela ya kununua mchele na sukari pamoja na ya kwenda Hospitali" Nilikuwa nikimsikiliza kwa umakini na baadaye nilimuahidi kuwa nitamtumia pesa kwaajili ya matibabu na chakula. Nilikuwa sina hela ilinibidi nikope pesa kwaajili ya kumtumia mama mkwe.

Baada  ya siku tatu kupita yule shemeji yangu alinipigia simu na kunikumbusha kile kiasi cha pesa alichoniomba, kwa bahati nzuri siku hiyo nilikuwa nimefanikiwa kupata pesa katika biashara zangu hivyo sikusita kumsaidia. Maisha yangu yalikuwa yamezungukwa ndugu wengi waliokuwa wakinitegemea katika mahitaji mbalimbali ijapokuwa nilikuwa sina uwezo mkubwa sana kifedha. Lakini nilijitahidi kwa kila hali kuhakikisha nawasaidia.

Baada ya miaka mitatu siku moja nikiwa natoka kazini nilipata ajali nikiwa naendesha gari aina ya Corola, na kunisababishia kuvunjika miguu, nilikuwa katika wakati mgumu sana kwani nilikuwa sina uwezo wa kufanya kazi tena.

 Na sasa nilikuwa nahitaji msaada kwa ndugu zangu, lakini chakushangaza wale ndugu niliokuwa nawasaidia hata sikumoja hakuna aliyekuja kunisaidia kwa chochote, walikuja kunisalimia maramoja tu na baada ya hapo sikumuona tena ndugu yeyote. Siku moja alikuja shemeji yangu na Mama mkwe  kwa nia ya kumshauri mke wangu aniache kwani sina uwezo wa kumsaidia. Niliumia sana moyoni "Inamaana leo hii  mimi Beni, naonekana sifai baada ya kupata ajali, na mbona nilikuwa nikiwasaidia sana, hivi ni kweli wananichukia kiasi hiki. Mungu nisaidie nipone, ama kweli binadamu  hawatabiriki."

Mke wangu, alikuwa na msimamo na hivyo hakuniacha aliendelea kuwa na mimi hivyohivyo. Ndugu zake walimtenga kabisa, kwasababu yangu.Maisha yalliendelea  baada ya mwaka mmoja kupita, hatimaye nilipona kabisa nakurudi katika hali yangu ya kawaida. Nilirudi katika kazi yangu ya awali  bila matatizo. Kwani nilipokelewa vizuri na sasa nilipandishwa cheo. Maisha yangu yalirudi katika ramani nzuri, wale ndugu walionikimbia wakati naumwa, baada ya kusikia kuwa nimerudi kazini. haikuchukua muda walianza kuja kunitembelea tena wakijidai wamekuja kunijulia hali.Lakini kwasababu tayari nilikuwa nimejifunza mambo mengi hivyo nilijua namna gani naweza kuishi nao. Safari hii nilikuwa makini zaidi. Sikutaka kulipiza kisasi  naishi nao vizuri. 

AMA KWELI BINADAMU HAWATABIRIKI, ANAWEZA KUKUPENDA UKIWA NACHO UKIWA HAUNA KITU ANAKUKIMBIA.

Maoni 6 :

Bila jina alisema ...

duuh!!! umenigusa kweli!

Ruky alisema ...

Du...nimejifunza kitu kikubwa sana hapa thankx Adela..

Unknown alisema ...

Maisha ndivyo yalivyo. Dada Adela naruhusiwa kuishea hii stori

Unknown alisema ...

Maisha ndivyo yalivyo

Unknown alisema ...

Daah may be napitia the same pathway nmepata matatizo makubwa nipo home najiuguza na majority wa ndugu zangu wengi hawana time kabisa,naumia bt cna jnc i hope Mungu atansaidia ntarudi km mwanzo

Unknown alisema ...

Nlipata paralysis mwanzoni mwaka huu ndugu na friends zangu weng wakajitenga kabisa nami,now nakaribia kumaliza mwaka nmepata nafuu km kwa asilimia 80
hvi,namshuru Mungu kwa nlipofikia sasa kwan naamin ntarecover asilia 10 na ntarejea kwa majukum yangu,dunia ina mambo mengi sn wadau usije ukaona una ndugu na marafiki weng ukpata matatizo watabak wachache sn utabaki na familia yako ti

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom