Jumatano, Agosti 28, 2013

SIMULIZI FUPI "USIMDHARAU MTU KUTOKANA NA KIPATO CHAKE"

MTUNZI- ADELA DALLY KAVISHE
Kuna vijana walikuwa wamekaa kijiweni huku wakizungumza, ghafla akapita kijana mmoja anaitwa Sudi na aliwasalimia, huku akiwa anaendelea na safari yake kwa bahati mbaya aliteleza na kuanguka, lakini hakuna hata kijana mmoja aliyenyanyuka na kumsaidia wote waliangua vicheko na mmoja wao akisema "Huyu jamaa atakufa kwa mawazo, si anaishi hapo mtaa wa pili kwa ndugu zake yaani hawana chochote ni masikini sana kazi yao ni kuombaomba" Huku wakiendelea kumcheka. 

Sudi alinyanyuka na kuendelea na safari bila ya kuzungumza chochote huku machozi yakionekana kumlengalenga aliwaza moyoni mwake "Watu wengi wananidharau kutokana na hali duni ya maisha niliyonayo, eeh Mungu nisaidie" Pale kijiweni waliendelea kuzungumza "Unajua umasikini ni mbaya sana, kwani siku zote ukiwa masikini, basi ujue utapata shida sana, na ukizingatia yule aliyenacho ndiyo anazidi kuwa nacho." Mmoja kati ya wale vijana alikuwa anaitwa Frank alisimama na kusema "Hivi mbona mnadharau sana jamani, unajua usimdharau mtu usiyemjua kumbukeni kuna leo na kesho, na hakuna binadamu anayependa kuishi maisha ya shida, msikufuru jamani mshukuruni Mungu kwa kuwa nyinyi mna maisha mazuri, familia zenu ni matajiri lakini kumbukeni msitumie pesa kama fimbo ya kumchapia yule asiyenacho".

 Wote walimcheka na kusema "Kwenda zako, sisi watoto wakishua wewe, hatuwezi kujichanganya na marafiki kapuku kama wewe" Basi Frank aliondoka huku akisikitika sana. Baada ya kama wiki moja pale mtaani kulitokea ugomvi baadhi ya wale vijana walihusika kumpiga sana kijana mmoja anaitwa Juma wa pale mtaani ndipo walipokamatwa vijana wengi katika mtaa ule na kupelekwa  mahabusu, katika wale vijana na Sudi alikamatwa ijapokuwa hakuhusika, Baadaye Askari walitoa adhabu kwa vijana wote kufanya kazi ya kungoa kisiki kila mmoja alipewa sehemu yake, na walikuwa vijana kama saba. Kila mmoja alikabidhiwa sehemu yake na walipewa muda wa siku tatu tu wawe wamekwisha maliza.

 Sudi alifanya ile kazi kwa juhudi zote ili afanikiwe kurudi nyumbani na hatimaye kutokana na juhudi ndani ya siku moja tu alimaliza. wale wengine walishindwa hata kufikia nusu kutokana na kuwa ni wavivu na walikuwa hawawezi kazi ngumu, kwa moyo wa huruma Sudi alijitahidi kuwasaidia wenzake kwa kila hali bila ya kujali kuwa walikuwa wakimdharau na kumuona hafai lakini alimsaidia kila mmoja na baada ya siku tatu waliachiwa huru.Kutokana na kilichotokea wale vijana walimshukuru sana Sudi,  na kumuomba samahani. Sudi aliwasamehe bila ya kuweka kinyongo.

TUISHI KWA KUPENDANA, KUMBUKA BINADAMU TUNATEGEMEANA, SI KWA PESA TU BALI HATA KWA MAMBO MENGINE, USIMDHARAU MTU KUTOKANA NA KIPATO CHAKE, KUNA LEO NA KESHO, MAISHA HAYATABIRIKI HUJUI NANI ATAKUSAIDIA KESHO.


Maoni 3 :

Unknown alisema ...

vizuri

Unknown alisema ...

Nimellipenda hili. Watu wengi wanakuwa hivo hasa hasa huko nyumbani. Tunafikiri sana kuwa na pesa ndio mwisho wa mambo. Hamna maana tajiri ana haja ya maskini na maskini naye ana haja ya tajiri na, ndio maana Mungu ka hamua wawepo maskini na matajiri. Yaana maskini na tajiri ni jana MTU NA KIYOO. Mtu kwakujua uso wake ni lazima ajitazame ndani ya miror ijapokuwa hiki hakiongee.
Pat X2 Lion

Unknown alisema ...

Nimellipenda hili. Watu wengi wanakuwa hivo hasa hasa huko nyumbani. Tunafikiri sana kuwa na pesa ndio mwisho wa mambo. Hamna maana tajiri ana haja ya maskini na maskini naye ana haja ya tajiri na, ndio maana Mungu ka hamua wawepo maskini na matajiri. Yaana maskini na tajiri ni jana MTU NA KIYOO. Mtu kwakujua uso wake ni lazima ajitazame ndani ya miror ijapokuwa hiki hakiongee.
Pat X2 Lion

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom