Alhamisi, Oktoba 24, 2013

MWISHO WA SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA. NDANI YA KITABU IKIWA NI SIMULIZI YA KWANZA KATIKA KITABU HIKI KILICHOBEBA SIMULIZI TATU TOFAUTI.

Kitabu hiki cha MALIPO NI HAPAHAPA kina simulizi tatu tofauti. baada ya simulizi hii itakujia simulizi  NYINGINE
ENDELEA KUPATA UHONDO. KWA ANAYEHITAJI KITABU TUWASILIANE KUPITIA della.media@ymail.com au 0752817444

ILIPOISHIA
 “Yuko wapi mama yangu, namtaka mama yangu.” Aliuliza Julieth huku
akilia na akiwa katika hali ya kuchanganyikiwa.
Yule kaka hakumwelewa anachozungumza akabaki anamshangaa. Ghafla
Julieth alianguka chini na kuzimia. Yule kaka na Zubeda walisaidiana
kumnyanyua Julieth na kumwingiza ndani kisha wakamlaza chini huku
feni ikimpepea. Yule kaka akamuuliza Zubeda aliyekuwa amewabeba
watoto wa Julieth.
“Vipi huyu mwenzio ana matatizo gani?” Aliuliza yule kaka.  JE NINI KITAENDELEA USIKOSE SIMULIZI HII HADI MWISHO WAKE

INAPOENDELEA
Zubeda akamwelezea kila kitu yule kaka ambaye ndiye mpangaji mpya
katika ile nyumba, alimwonea huruma sana Julieth. Baada ya Julieth
kuzinduka aliendelea kulia asijue nini cha kufanya kwa yote yaliyomkuta.
“Usijali Julieth nitakusaidia ulale hapa mpaka kesho. Karibu sana mimi
naitwa Baraka, Zubeda amenieleza matatizo yote uliyonayo pole sana.”
Aliongea Baraka ili kumfariji Julieth.
“Asante sana kaka Baraka.” Alishukuru Julieth.

Baraka alimtayarishia maji ya kuoga na baada ya kuoga Julieth alijisikia
vizuri sana kisha alipewa chakula. Muda wa kulala ulipofika Baraka
alimwonyesha Julieth chumba cha kulala akiwa na watoto wake Domina
na Dominiki.
Alipokuwa chumbani aliwaza mambo mengi sana huku moyoni akijilaumu
mwenyewe;

“Mimi ndio chanzo cha kila kitu, hivi kwa nini niliondoka na kumuacha
mama yangu wakati nilijua anaumwa?, Ewe mama popote ulipo naomba
unisamehe na wadogo zangu Joseph na Peter sijui wako wapi, maisha
yangu ni ya mateso siku zote kwa nini lakini? Sijui nitakwenda wapi. John
alinidanganya na kuniacha, sasa na mama nimempoteza mimi nitakuwa
mgeni wa nani?” Alilia kwa uchungu huku akiwaangalia watoto wake
waliokuwa wadogo sana wasioelewa chochote, baadaye akalala usingizi
mzito kutokana na uchovu wa mawazo na safari.

Kesho yake asubuhi Baraka aliamka mapema na kuandaa chai mezani
kisha akamwamsha Julieth ajiandae wakapate kifungua kinywa. Wakiwa
mezani Baraka alitaka kumfahamu vizuri Julieth. Maskini Julieth
alimweleza kila kitu kuhusu mkasa mzima wa maisha yake na pia
akamwambia hajui atakwenda wapi.Yule kaka akamwambia ataendelea
kuishi pale ili aweze kuwalea watoto wake vizuri na pia atamsaidia
kuwatafuta wadogo zake. Julieth alimshukuru sana Baraka kwa kumpa
nafasi ya kuishi pale nyumbani kwake. Baraka alikuwa ni mfanyabiashara
palepale mkoani Arusha. Alimsaidia sana Julieth na kumfariji wakati wote
kwani Julieth alikuwa amekata tamaa ya maisha.

Baada ya siku kadhaa kupita Julieth alianza kuzoea mazingira, aliishi vizuri
na watoto wake. Baada ya mwaka mmoja Julieth na Baraka walianza
uhususiano wa kimapenzi. Urafiki wao ulimfanya Julieth asahau yote
aliyotendewa na John. Maisha yaliendelea na hatimaye Julieth na Baraka
wakawa wapenzi na baadaye walifunga ndoa kanisani. Wazazi wa Baraka
walimpenda sana Julieth na kuwatakia kila la heri katika maisha yao. Baraka
aliwapenda sana watoto wa Julieth na hatimaye hata jina la ukoo walitumia
jina la Baraka.

Julieth hakutaka kumkumbuka John kabisa na wala hakutaka kumsikia
tena katika maisha yake. Wakati huo Julieth alikwisha wapata wadogo zake
na kuishi nao kwa furaha sana kama familia moja. Watoto wa Julieth
walikua wakimjua baba yao ni Baraka.

**********Baada ya miaka mitatu************

Baada ya miaka mitatu Julieth alifanikiwa kumpata mtoto mwingine wa
kiume aliyeitwa Novatus. Julieth alifurahi kuliko kawaida kwani familia
ilizidi kuongezeka. Maisha yao yalikuwa mazuri sana kuliko yalivyokuwa
kwa John. Kwani kwa Baraka waliishi kwa amani na upendo.

Huko Mwanza katika maisha ya John yalibadilika, biashara zilimwendea
vibaya na kuanza kuuza baadhi ya vitu. Siku moja wakiwa wanatoka
kwenda katika matembezi John na mke wake pamoja na mtoto wao
wakiwa katika gari . walipata ajali mbaya sana. Mke wake pamoja na mtoto
walifariki dunia palepale ila John alipoteza fahamu na kuumia baadhi ya
sehemu katika mwili wake. John alikimbizwa hospitali ambako alikaa muda
mrefu sana akiwa anatibiwa. Kutokana na kushindwa kunyanyuka
kitandani alishindwa kuhudhuria hata mazishi ya mtoto na mke wake, hata
hivyo baadaye alipona na kuruhusiwa.

Lakini wakati akiondoka, daktari alimwambia kuwa kutokana na ajali
aliyoipata hata kuwa na uwezo wa kuzaa tena. Ilikuwa ni mshtuko sana
kwa John ambaye alikuwa hana mtoto mwingine tena zaidi ya Philipo
aliyefariki kwenye ajali. John alichanganyikiwa.
Baada ya kupata nafuu John aliruhusiwa kurudi nyumbani. Siku ya tatu
tangu atoke hospitali, John alikuwa amekaa chini ya mti wenye kivuli
kikubwa alianza kuwaza juu ya mambo yaliyokuwa yanaendelea kutokea
dhidi yake. “Kweli mimi yamenikuta, sina mke, sina mtoto halafu sina uwezo wa kupata mtoto maisha yangu yote. Maisha yangu yamefika mwisho na
biashara nazo zinaniendea vibaya nitafanyaje?”

Akiwa anawaza ghafla akamkumbuka Julieth ambaye alizaa naye watoto
mapacha kisha akamfukuza baada ya mke wake kurudi kutoka Dar es
Salaam; “Julieth ana watoto wangu mapacha sijui atakuwa wapi, labda
atakuwa kwao Arusha na kwa mabaya yote niliyomfanyia na sasa ni miaka
mitano imepita itanibidi nimtafute alipo ikibidi niende Arusha.” Aliwaza
John huku akiwa na matumaini atakapomuona Julieth atawapata watoto
wake. John alianza kuulizia wapi Julieth alipo baadaye aligundua Julieth
yupo Arusha na moja kwa moja alipanga safari ya kwenda kumtafuta
Julieth.
Baada ya wiki moja John alianza safari ya kwenda Arusha kumtafuta
Julieth. Akiwa njiani aliwaza sana moyoni;
“Nikimpata nitamwomba msamaha kwa yote niliyomfanyia halafu tuanze
maisha mapya na watoto wetu.” Aliwaza John huku safari ikiendelea.

Alipofika Arusha alichukua teksi kuelekea nyumbani kwa akina Julieth.
Kutokana na kwamba nyumba ile anaikumbuka kwa hiyo alikwenda moja
kwa moja. Ilikuwa yapata saa moja jioni ambapo Julieth pamoja na familia
yake walikuwa wamekaa sebuleni wakizungumza huku geti likiwa wazi.
John alipofika alipita moja kwa moja na kwenda kugonga mlango wa
sebuleni. Mlango ulifungualiwa na mdogo wake Julieth yaani Joseph
ambaye alimkaribisha ingawa alikwisha msahau kutokana na mabadiliko
aliyokuwa nayo baada ya kupata ajali. Ilikuwa ni miaka mingi imepita
tangu waonane, kwa mshtuko mkubwa sana Julieth aliyemtambua
alinyanyuka na kusema.

“Nani amekuruhusu uingie humu ndani? Hivi wewe ni binadamu wa aina
gani umeona haitoshi uliyonifanyia bado unanifuatafuata, unataka kuniua
au? Naomba utoke nje sasa hivi.” Alisema Julieth huku midomo
ikimtetemeka kwa hasira na kuwaacha waliokaa pale sebuleni wakishangaa
kuna nini.
“Vipi mke wangu huyu mtu ni nani?” Aliuliza Baraka.
“Huyu ndiye John aliyenitesa katika maisha yangu, nashangaa amefuata
nini hapa.” Alijibu Julieth.

John aliyekuwa amesimama alianguka chini kwa magoti na kuanza kulia
huku akiomba msamaha;
“Julieth naomba unisamehe najua nimekukosea sana katika maisha yako
na mimi Mungu amenipa pigo la maisha hapa nilipo sina uwezo wa kuzaa
tena. Nilipata ajali mke na mtoto wangu walifariki, naishi katika mazingira
magumu. Julieth naomba unisamehe unipe nafasi ya kuwa karibu na
watoto wangu nakuomba Julieth.” Alibembeleza John.

“Kweli malipo ni hapahapa leo hii wewe unanipigia mimi magoti, baada
ya kunifukuza kama mbwa na kuwakana watoto leo unasema unataka uwe
karibu na nani?. Una kichaa kweli wewe, hawa watoto sio wako yule pale
ndio baba yao anaitwa Baraka. Mimi sikujui na wala sitaki kukuona
naomba uondoke” Alifoka Julieth huku akicheka kicheko cha kejeli.
“Kama ni kukusamehe nilikwisha kusamehe ila naomba uondoke na
watoto wangu uwasahau.” Alisisitiza Julieth huku akisimama na kuelekea
chumbani akibamiza mlango kwa hasira.

John hakuwa na cha kusema zaidi, aliwaangalia Domina na Dominiki
watoto ambao walikuwa hawaelewi chochote. Watoto nao walimshangaa
sana John wakimwacha na maumivu zaidi moyoni akilia kwa uchungu.
Aliaga na kuondoka huku akitembea hatua moja na kugeuka nyuma
kuwaangalia watoto wake ambao hakuwa na uwezo wa kuwachukua tena.
Julieth na mume wake walibaki wakiwa wanatafakari kilichotokea, Julieth
alikuwa ni mtu mwenye hasira sana siku hiyo.

John aliondoka akiwa amechanganyikiwa asijue anaelekea wapi. Ghafla
akiwa anavuka barabara aligongwa na gari na kufa palepale ukawa mwisho
wa maisha yake.
Julieth na watoto wake walibaki wakiwa katika maisha ya furaha na amani
na kwa Julieth Baraka ndiye alikuwa chaguo lake la moyo walipendana
sana wakaishi maisha ya furaha na amani.
**********Mwisho********* USIKOSE SIMULIZI YA PILI. 

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom