Jumatano, Desemba 11, 2013

SIMULIZI FUPI ,,,LOVE STORY



Kijana mmoja alitokea kumpenda sana dada mmoja ijapokuwa dada huyo alikuwa akimtolea nje mara kwa mara lakini kijana hakukata tamaa, akiendelea kurusha ndoano huku akiamini siku moja atafanikiwa.Siku moja dada huyo akiwa yupo nyumbani aliamua kumpigia simu huyu kaka na kumtaka aje nyumbani kwake, yule kijana alifurahi na kuhisi sasa ombi lake limekubaliwa. 


Akiwa nyumbani kwake dada huyo , alikuwa amevalia kanga moja laini, kutokana na hali ya hewa ya joto la Dar es salaam.Kwa upande wa yule kijana alikuwa amefurahi sana na haraka alijiandaa na kuanza safari kuelekea kwa huyu dada, njia ni kaka huyu alikuwa akijiuliza maswali mengi, huku akiwa haamini kama yule dada amemuita nyumbani kwake. Alipofika, alibisha hodi na yuel dada akafungua mlango huku akionyesha tabasamu pana katika paji la uso wake. 



Kaka huyu aliingia ndani huku kijasho kikimteremka mithili ya mtu aliyekuwa anakimbia. Dada huyu alimkaribisha vizuri, yule kaka aliomba maji ya kunywa huku muda wote akimtizama kwa umakini dada huyu mrembo, aliyeumbika kila idara na ile kanga nyepesi aliyovaa ilikuwa ikionyesha umbo zuri la dada huyu ambaye waswahili huwa wanasema, mtoto kajaaliwa (mashalaah) Kaka alikuwa akivuta pumzi kwa haraka haraka, na kusema "Nimefurahi sana, umenikaribisha nyumbani kwako ni pazuri sana." Yule dada alitabasamu na kusema "Asante sana, nimefurahi pia umeitikia wito wangu, samahani kwa usumbufu wangu".

Yule kaka alitabasamu huku akijisogeza sogeza "Hakuna tatizo, usijali kabisa, mimi nipo kwa ajili yako, naimani sasa nina...." Kabla hajamilizia kuongea yule dada alimshika mikono yake miwili huku akimtizama machoni, kwa macho yake malegevu, mithili ya mtu aliyekula kungu "Samahani kaka, mimi nimekuita hapa kuna jambo nataka unishauri, nataka kujua ni zawadi gani nzuri unaweza kumpatia mwanaume unayempenda" Kaka yule alikuwa akitetemeka na kusema "Chochote tu, zawadi ni zawadi, alimradi kuwe na mapenzi ya kweli" Dada yule alitabasamu na kusema "Ni kweli, mapenzi ya kweli ndiyo jambo la msingi, nitampenda maisha yangu yote" Kaka yule akauliza "Utampenda? Nani huyo"
.
 Yule dada alitabasamu tena na kusema "Samahani, rafiki nilikuwa sijakuambia, wiki ijayo nafunga ndoa na mpenzi wangu wa muda mrefu ambaye nampenda sana, na pia nilikuita ili nikupe kadi ya harusi, nitafurahi kukuona, kwani wewe ni rafiki yangu pia" Yule kaka alibaki amepigwa na butwaa, "Ati, nini unaolewa, daaah, jamani, kwahiyo." Alinyanyuka na kuondoka bila ya kuaga huku akimuacha yule dada anamuita ili ampatie kadi bila ya mafanikio.

SIYO KILA UNACHOKIWAZA MOYONI MWAKO KITATOKEA KAMA UNAVYOTAKA. KWAHIYO NI VYEMA KUJIANDAA KUKUBALIWA AU KUKATALIWA

by ADELA KAVISHE


Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom