Jumanne, Mei 06, 2014

POLE SANA RAY C "HOMA YA DENGUE YAITIKISA DAR"

Ray C alazwa Mwananyamala kwa ugonjwa huo, wawakumba madaktari na wauguzi.PICHA|MAKTABA MUNGU AKUTANGULIE UPONE HARAKA

Ugonjwa wa homa ya dengue umezidi kusambaa mkoani Dar es Salaam na sasa umeathiri wilaya zake tatu na kuzua hofu kwa wananchi.
Miongoni mwa walioathiriwa na homa hiyo ni mwanamuziki maarufu Rehema Chalamila (Ray C) ambaye amelazwa katika Wodi Namba Tano ya Hospitali ya Mwananyamala.


Mmoja wa madaktari wa hospitali hiyo, alithibitisha kulazwa kwa Ray C kutokana na ugonjwa huo jana.
“Tumethibitisha kwamba Ray C ana dalili zote za dengue, lakini kimaadili siruhusiwi kutoa taarifa za mgonjwa,” alisema daktari huyo ambaye hakutaka kutajwa jina lake.
Hata hivyo, waandishi wa gazeti hili walimwona mwanamuziki huyo hospitalini hapo akiwa katika usingizi mzito na madaktari walisema hakuwa katika hali mbaya bali alikuwa amelala kwa sababu ya uchovu wa dawa.
Mbali na Ray C, pia madaktari watatu na muuguzi mmoja wameripotiwa kuugua ugonjwa huo.
Tayari mamlaka zimetoa tahadhari kwa wananchi kuwataka wachukue hatua za haraka kuzuia maambukizi ya homa hiyo inayosababishwa na mbu anayejulikana kitaalamu kama aedes egyptiae.
Hadi sasa wagonjwa zaidi ya 100 wameripotiwa kuugua ugonjwa huo katika wilaya za Kinondoni, Ilala na Temeke na baadhi wakiripotiwa kupoteza maisha.
Takwimu kutoka Kitengo cha Utafiti wa Magonjwa cha Ifakara (IHI), kilichoweka kambi katika Hospitali ya Mwananyamala kutafiti aina za homa, zinaonyesha kuwa kwa miezi miwili ya Machi na Aprili pekee, wagonjwa 85 walibainika kuwa na homa hiyo.
Hata hivyo, idadi inaweza kuwa kubwa zaidi kutokana na kukosekana kwa takwimu, vipimo na watu kuufananisha ugonjwa huo na malaria.
Daktari kiongozi wa hospitali hiyo ambaye pia ni mtaalamu wa ugonjwa huo, Dk Mrisho Rupinda alisema kuwa kuna taarifa za wagonjwa wa dengue walioripotiwa katika maeneo yote ya Dar es Salaam.
“Katika kipindi cha wiki moja iliyopita tayari madaktari wawili kwenye hospitali hii wamebainika kuugua ugonjwa huo, tunahisi walipata maambukizi kwenye maeneo ya humuhumu ndani hospitali,” alisema Dk Rupinda.

CHANZO MWANANCHI

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom