Jumatano, Julai 23, 2014

SIMULIZI YA MAISHA "USILIE NADIA "SEHEMU YA PILI"

SEHEMU YA PILI

Baada ya kumlaza mapajani kwangu huku akilia kwa uchungu mkuu, nami nikifanya jitihada za kuyafuta machozi yake. Hatimaye Nadia alitulia. Nilipomtazama alikuwa amepitiwa na usingizi, nikamfunika na upande wa kanga yake. Kisha nikaiweka mikono yangu vyema aweze kuegemea vizuri.
Ukimya uliotanda ukanifanya nami nianze kusukwa sukwa na usingizi, nilijitahidi kuukabiri lakini sikuweza. Nikajiegesha vyema katika kiti, nikasinzia pia.

SAUTI nzito ya mpiga debe ndo ilitukurupua.

“Oyooo mwisho wa gari hapa!!” 

Nadia naye alisikia sanjari na mimi, tukatazamana na kutabasamu kama kwamba tuliambiana kufanya hivyo. Nadia akajinyoosha huku akipekecha macho yake, mimi nikajishughulisha katika kuweka sawa mabegi yetu. Tukatoka ndani ya gari tukiwa abiria wa mwisho kabisa. Tukaikanyaga stendi ya Buzuluga jijini Mwanza, safari yetu fupi kutoka Musoma kwenda Mwanza ikawa imekamilika.

Nadia alilalamika njaa inamuuma. Nilitazama huku na kule nikauona mgahawa ng’ambo ya pili ya barabara. Nikamshika kiganja cha mkono wake, tukavuka barabara kama hatuzisikii kelele za madereva taksi waliokuwa wakitupigia kelele ili tukodi mojawapo ya teksi kwa ajili ya safari yetu.

Hakika tulikuwa na haja na teksi lakini matumbo yalikuwa matupu, tulihitaji chochote kitu hasahasa cha moto. 
Tulisfutahi kimya kimya bila mazungumzo baina yetu. Kila mmoja alionekana kuwa na uchovu wake. 

Baada ya hapo nd’o tulihitaji taksi, ikatuchukua hadi G & G Hotels, ni huku nilipendekeza. Teksi ilipotoweka, Nadia aliniuliza swali. 
“Umeifahamu vipi hii hoteli kaka.” 

Kwanza nilimtazama huku nikitafakari nini cha kujibu.
“Hi ndo hoteli yangu mara kwa mara nikitembelea jiji hili.” Nilimjibu, kisha nikaongezea kidadisi, “Kwani kuna tatizo?”
Hakujibu kitu nami sikuuliza tena, nilitambua kwa nini hakujibu, bila shaka ni uwepo wa watu kadhaa mahali tulipokuwa, nikajisogeza mapokezi nikafanya malipo ya vyumba viwili tofauti vyenye hadhi ya ‘Deluxe’ kisha nikamfanyia ishara Nadia akanifuata. Nikamwongoza hadi katika chumba ambacho angelala siku ile.

Alipokiona chumba alishusha pumzi kwa nguvu, nikakifungua akaingia, hapa akafika na kusimama katikati ya chumba akiwa anatazama dirishani. Upesi nikachukua vifaa vyangu. Bila shaka Nadia alitaka kujibu lile swali dogo nililomuuliza na kutarajia majibu ya kawaida.

“Kila moyo huwa na shukrani, lakini mwanadamu hana shukrani. Naamini kabisa mwanadamu hana shukrani, Afadhali Punda aliyejiweka wazi na shukrani yake ya mateke kuliko mwanadamu. yaani angekuwa mlemavu Yule. Huduma mbovu za kule Musoma wakadai anatakiwa akatwe mguu. Nikamdanganya mzee wangu kuwa nimepoteza Laptop ya rafiki yangu yenye thamani ya milioni nyingi. Mzee wangu mimi na upendo wote anaonionyesha lakini bado nikamdanganya eti kisa Desmund. 

Tukakodisha usafiri akaletwa Bugando, naikumbuka siku aliyofika kwa mara ya kwanza tulifikia hoteli hii, laiti ningeyajua ambayo yangekuja kutokea nisingepoteza pesa zangu wala nisingemlaghai baba, Desmund bila ndugu yeyote mimi nikawa kila kitu. Alifikia hatua ya kuniita Mungu wake, akanililia siku ambayo aliweza kusimama kwa mara ya kwanza, nikamshika mkono akiwa anafanya mazoezi ya kuimarisha miguu, nikaacha kuingia darasani hadi alipopona. 

Nilipomrudisha Musoma kwao ndo hapo niliposikitika zaidi, kile chumba alichokuwa akiishi Desmund tulimkuta mtu mwingine, alipoulizia samani zake akapewa mkeka na sufuria ndogo mbili. Nilishangaa lakini yale nd’o yalikuwa maisha yake halisi.

Sitaisahau siku ambayo tulilala wote ili nimtazame afya yake, sikutaka awe mbali nami. Moyoni nilianza kukumbwa na pepo mchafu, pepo wa maajabu aliyesema eti siwezi kukaa mbali na Desmund. Nikalala naye katika hoteli ya Grand Villa huko Musoma. Ni usiku huo ambapo nilianza rasmi mahusiano na Desmund, vishawishi vya kimwili, tamaa ya muda mfupi nikajikuta kwa hiari yangu nafanya mapenzi na Desmund. Siwezi kusema alinilaghai la! Hata yeye hakutegemea kama jambo hilo litatokea, hakika siwezi kujuta maana ni upendo wa dhati ulinituma.

Desmund akatumia neno hilo ‘nakupenda’ nililomtamkia kuanza kunisulubu. Alijua nampenda sana hilo alilijua hadi siku ya mwisho na ataendelea kulijua. Nikampangia chumba kikubwa na kumnunulia baadhi ya vifaa vya ndani, hii nyumba ikaja kuwa chungu kwangu kile kitanda, lile godoro na mashuka niliyonunua mimi ikafikia kipindi akawa jasiri kuingiza wasichana pale ndani. Alimuingiza hadi yule msichana ambaye alisababisha anitegue mguu kwa mpini wa jembe.
Desmund alikuwa mshamba wakati naanza naye mahusiano, hakuna chakula cha kifahari alichokitambua zaidi ya Chipsi kuku. Nikamwonyesha dunia ilivyo, hakujua hata mkanda wa ndege unafungwa vipi? Nikampandisha ndege….hakujua nini maana ya ‘body exercise’ yote haya nikamwonyesha mimi, akatanua kifua na kuvaa vizuri hatimaye akapendeza.

Kweli yule Desmund ambaye hata hakuwa akijua nini maana ya ‘Piza na Baga’ ikafikia kipindi akanipiga mateke akisema mimi ni mshamba sana, nimekalia kukuza matiti tu kila kukicha, sijui kuoga. Na mbaya zaidi akafikia hatua ya kusema eti ninanuka sana hawezi kuishi na mimi anajilazimisha. Nilitamani sana kuondoka lakini ningeenda wapi mimi ningekimbilia kwa nani? Kila mtu anayeitwa ndugu yangu alikuwa amenitenga.” Safari hii Nadia hakulia bali alifanya tabasamu hafifu…lakini alikuwa amechukia. Nikaaga na kuelekea chumbani kwangu. Majibu yake ya sasa yakiwa yanaongeza giza mbele yangu. Sikupata jibu kabisa alikuwa ana maanisha nini.
Nikavuta subira nikaenda chumbani kwangu. Nikaoga na kubadili nguo kisha nikarejea chumbani kwa Nadia.

Nilimkuta akiwa analia, nilipoufungua mlango akazidi kulia, japo kwa sauti ya chini. Luninga ilikuwa ikipiga kelele na hakuonekana kama alikuwa anaitazama.
Nikaketi pembeni yake mara akasimama ghafla.
“Hivi wanaume mnataka mfanyiwe nini hasa, mnataka mliliwe vipi ndipo mjue kuwa mnapendwa eeh….hivi mnataka roho zetu eeeh nakuuliza ..nakuuliza wewe na wewe ni mwanaume ujue nasema na wewe …” Hapa akanikamata ukosi wa shati langu kwa ghadhabu, akaanza kunitikisa, sikujishughulisha kuitoa mikono yake nilitaka aseme kitu akiwa na hasira. Kweli akaendelea.

“Yaani wakaona kuninyoa nywele zangu haitoishi, wakanifanyta mtumishi wao wa ndani nayo pia haikutosha. Kweli Desmund akawaangalia dada zake wananimwagia maji mimi, maji machafu…Desmund ulishindwa kuwakaripia waache kunionea.
Mama yake naye niliyedhani kuwa anaweza kunionea huruma akapigilia nyundo ya mwisho katika kidonda change. Eti hakuna ndoa wala ndoano mpaka….yaani mpaka nifanyiwe tohara. Nilishtuka nikataka kukimbia lakini nani angenipokea kama ningekimbia kila mtu alikuwa ananiona mimi adui. Mbaya zaidi baba na mama yangu hawakutaka kunisikia na kubwa zaidi walijikusanya na kurejea Doha Saudi Arabia. Nikabaki Tanzania nikiwa peke yangu. Licha ya upweke ule mwanaume na mwanadamu pekee niliyetegemea atasimama upande wangu kila siku akaniacha nikakamatwa kwa nguvu. Naikumbuka siku hiyo nililia lakini hawakuniachia, wakanifikisha mahali ambapo ni kama machinjioni, looh!! Kuna makabila yana roho mbaya namna hii, kumbe kabila la Desmund lina mambo haya.

Wakanifanyia ukeketaji, Desmund akiwa mkimya kabisa, lakini kumbe haya yote yalifanyika ili mimi nikate tamaa ya kuolewa na Desmund, walijua kuwa nitakataa lakini mimi nikakubali kumbe Desmund hakunipenda alikuwa na mchumba aliyechaguliwa na mama yake. Lakini mchumba wa kupewa na mama mimi sina tatizo, mbona sasa akaanza kulewa, mbona sasa akaanza kuwabadili wasichana hovyo, au kwa sababu …au kwa sababu nilikuwa sizaiiii….eeeh au kwa sababu sikumzalia mtoto mimiii……Desmund hivi sio wewe uliyenisindikiza kutoa mimba mara tatuw tofauti. Si wewe Desmund uliyesema kondomu huwa zinakuwasha na hauzipendi hata kidogo. 

Nikakusihi tuwe makini ukanikaripia nikakusikiliza usemayo mume wangu. Kama mimba tulienda kutoa wote mbona nilipopata tatizo la kizazi ukanitenga, ukanitupia katika midomo ya mawifi zangu. Nikatukanwa nikasemwa kikabila chenu, wakanitukana kikabila chenu wewe naye ukasema nao kikabila chenu ili nisiweze kuwasikia. Kumbe nawe ulinitenga Desmund…..Desmund….
Wakanilaza jikoni huku wewe ukilala chumbani kwa raha zako, ukaridhika kuniona nasulubika, asubuhi ukaondoka bila kunisalimia..na ukatoweka kwa siku ishirini. 
Desmund nilikunong’oneza kuwa siyajui maisha ya kijijini, nawe ukasema hutaniacha pekee kamwe, lakini ukatoweka, nikawa mtumwa rasmi, nikaosha vyombo nikafua hadi nguo za mawifi. Nikakamua ng’ombe maziwa, mara nikaambiwa niwe naenda kuwapeleka malishoni.

Ni lini mimi nimejua kuchunga ng’ombe…lini nimejifunza kitu hiki. Nilikwambia Desmund kuwa maisha niliyotoka mimi ni ya kudekezwa sana, sawa sikatai kuchunga ng’ombe lakini walau basi ningefundishwa taratibu.
Nikaenda malishoni, ng’ombe wakapandwa mori zao mmoja akanitupa mbali kwa pembe zake, nikavunjika kiuno. Desmund ukanipa pole kwa njia ya simu…..kweli kiuno kimevunjiaka ukatumia simu …Desmund….simu!!!!! aaaargh Des…De…..Desmu…..Desmuuu…….” hapa uvumilivu ukashindikana akaangua kilio, hiki cha sasa kilikuwa kilio kitakatifu, akajirusharusha kitandani, akaruka huku na kule. Hapa nikashtuka kuwa anaweza kujizuru, nikamkamata mabega yake nikamgandamiza kitandani. Akashindwa kufurukuta lakini hakika alikuwa amechachamaa sana.
Niliendelea kumgandamiza huku nikimchukia Desmund.

MOJA. Yaani mkeo anavunjika kiuno hufiki kumwona unapiga simu.
MBILI: Mwanamke aliyeweka masomo kando akakupigania unashindwa kumpigania mbele ya ndugu zako.
TATU: Yani kumbe Desmund mpuuzi bado anaendekeza mila za kizamani za tohara.

“MASKINI NADIA ……USILIE NADIA……jikaze jikaze ndo wanadamu hawa…..jikaze usilie…” nilimsihi……..USIKOSE NINI KITAENDELEA

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom