Jumatatu, Julai 28, 2014

SIMULIZI YA MAISHA "USILIE NADIA SEHEMU YA TATU"




SEHEMU YA TATU

Niliendelea kumsihi Nadia asiendelee kulia kilio kikuu namna ile. Laiti kama angechomoka katika mikono yangu bila shaka angefanya kitu kimoja kibaya sana, ndio! Nilihisi ni kibaya lakini sikujua ni kitu gani angeweza kuongozwa na hasira zake kukifanya.

Hatimaye alitulia akabaki kulia kwa kwikwi tu binti yule aliyekeketwa katika safari yake ya kutafuta ndoa. Ndoa ya hayawani!!

“Unajua Nadia, sometime you have to let it go…ukiwa mtu wa….” Kabla sijamaliza akiwa amelala chali aliyaingilia maongezi yangu. Wakati huu sikupata nafasi ya kukishika kifaa changu cha kuinasa sauti yake. Hivyo nikaweka umakini kumsikia anachotaka kusema. Huenda katika kauli yangu fupi kuna kitu alikumbuka.

“Desmund! Alikuwa na lafudhi mbaya kweli, hakujua hata ‘give me some water’ ina maanisha nipe maji ya kunywa, sikupenda kuonekana nipo juu yake kwa kila kitu, nikamwanzishia kozi ya kujifunza kiingereza. Wanafunzi wenzake walimcheka alivyoshindwa kujitambulisha iwapo yeye ni ‘boy’ ama ‘girl’ nikasimama kidete kumshauri juu ya hilo nikampa moyo asonge mbele. Akanielewa akazidi kujituma, mwishowe akaanza kukijua kiingereza.

 Wakati huo sijui hata kama atakuja kukitumia kila kiingereza vibaya kwa kuniambia ‘you bitch pack your things and leave! My house!!’….sasa niende wapi na kwa kosa lipi sijui, halafu ilke nyumba kodi yote nilikuwa nimelipa mimi lakini akadai ni nyumba yake nichukue kilicho changu niondoke. Hakuishia hapo akaniuliza swali ambalo lilinifanya nimuone mpuuzi na mwendawazimu, eti ‘don’t you understand English?’ ..sasa mimi nimemchukua akiwa hakijui hata hicho kiingereza lakini leo hii ananiuliza eti iwapo sijui kiingereza was he crazy!!!” hapa Nadia kwa mara ya kwanza tangu tuanze safari alifanya kicheko kidogo, kasha akaendelea “wanaume huwa mnakuwa wapumbavu sana mkishashika pesa kidogo halafu mkagundua kuwa mnapendwa mnavimba sana vichwa. Basi Desmund akawa ana kiburi kilichopitiliza, eti hapo kisa tu nilimwambia yeye ni kila kitu kwangu. Desmund akayatumia madhaifu yale kunifanya apendavyo.
Unajua kaka…katika haya maisha hakika tunatenda maovu mengi sana, mengine yanasameheka lakini kwa akili ya kibinadamu mengine yanakuwa magumu sana kusamehe, ujue kucheza na akili ya mwanadamu mwenzako ni kitu kibaya sana maana hujui ataathirika kiasi gani akijua kuwa unamchota akili. Fikiri kuhusu Desmund yaani na miaka yake thelathini na mbili, alikuwa ananidekeza sana. Nitake nini Desmund asinifanyie, mara apike uji mara anibembe mgongoni. Nikinuna kidogo ananibembeleza na kila alivyonikumbusha kuwa ananipenda sana mwanaume alitoa machozi, alilia haswaa. Chozi lake nililiona la thamani sana lakini nikagundua baadaye kuwa anacheza na hisia zangu, niliumia alivyokuwa analia lakini yeye alikuwa akinitukana kuwa niache kujilizaliza. Niache kujiliza wakati nimeumizwa kabisa, Desmund hakuliona chozi hili akawasaidia wale wanawake kunitawanya miguu yangu kisha wembe mkali ukanifyeka, nikakeketwa Nadia mie. Nikakeketwa ili niolewe.

Wakati mwingine najilaumu mimi mwenyewe halafu nahisi ni laana hii inaniandama kakangu, hii itakuwa laana tu. Ujue mama alilia sana siku ambayo baba alikuwa ananifukuza nyumbani, wadogo zangu walilia sana kaka, wote wakanisihi kwa kiarabu kuwa nibadili maamuzi yangu. Tayari alikuwa amechaguliwa mchumba wa kiarabu kutokea Jedah kwa ajili yangu nikimaliza chuo. Mchumba ambaye alinivumulia tangu nikiwa mdogo hadi nikiwa chuo kikuu, huyo nikaona hana maana nikakabidhi maisha yangu kwa Desmund. Mama alisema maneno mengi huku akigalagala chini, alilia sana, na kwa mara ya kwanza katika maisha yangu mzee wangu Ramadhani licha ya ukorofi wake uliokithiri na usiomithirika alitokwa na chozi katika jicho moja. Nikaondoka na sikutaka kuangalia nyuma. Nikaenda kwa Desmund ambaye alikuwa kila kitu kwangu. Nikaamini kuwa nipo katika njia sahihi kabisa, wala sikujilaumu!!

Elimu ilinipotosha hakika, bila elimu sidhani kama ningeyajua mambo ya kujichagulia mume wa kunioa, mimi nilifunguliwa na elimu nikajichagulia Desmund labda kweli elimu ni ufunguo wa maisha lakini kwangu mimi el;imu ilinifungua na kasha ikanifunga katika utumwa wa mapenzi.
Mdogo wangu alinipigia simu kwa mara ya mwisho akanieleza taarifa mbaya sana ambayo nd’o naiita laana maishani. Hakika ilikuwa laana, mdogo wangu alikuwa analia na akaniambia waziwazi kuwa familia nzima inanichukia tena inanichukia sana. Hakunipa nafasi ya kuongea neon lolote aliendelea kuzungumza akinirushia lawama kuwa nimemuua mama, hapa nikahisi kuzizima kabisa, Kassim akaniambia kuwa mama alikufa akinilaumu kwa kila neno, na neno lake la mwisho alisema ‘Nikifa mnitupe baharini ama mnichome moto simtaki Nadia kaburini kwangu, sitaki kuisikia sauti yake, kama ataweza aiombe bahari initapike kama ataweza ayaombe majivu yaungane tena aweze kuniona. Msinizike aje kulowanisha kaburi langu na machozi yake yaliyolaaniwa, sitaki kelele za kilio chake zinisumbue katika usingizi wangu wa milele. Mwambieni namchukia kupita watoto wangu wote kwa yote aliyonifanyia na kunifedhehesha!!!’. Maneno yale yalikuwa makali sana, kisha simu ikakatwa. Nilipojaribu kupiga haikuwezekana.
Simu ilipigwa kutoka katika vibanda vya simu Jeddah Saudi Arabia. 
Huo ukawa mwisho wa kuwasiliana na ndugu zangu, ndugu pekee alibaki kuwa Desmund, na nilimweleza yote haya kuwa mama yangu amekufa akinilaani, nikamsihi Desmund awe mkweli kwangu ili mama yangu popote alipo atambue kuwa huyu alikuwa mwanaume sahihi, najua roho ya mama inanizomea kwa wakati huu kwa sababu nimeaibika tayari. Nilimvumilia Desmund ili mama asijue kama tuna matatizo katika familia lakini haikuwa hivyo kwa upande wangu, kwa maana hiyo Desmund aliona sawa tu nilivyochukiwa na familia, aliona sawa tu mama yangu mpenzi alipokufa akinilaani, yaani kwa ufupi kila lililo baya Desmund aliona sawa tu….aliona Nadia alizaliwa ili ateseke…Desmund u mwanaume gani sasa wewe…eeh Desmund..” kilio kikamzidi…akajilaza tena, nikampiga piga begani bila kusema naye lolote. Huku nikidhani kuwa amenyamaza na hatazungumza tena kumbe alikuwa akijifuta machozi kisha akaendelea, sasa alikuwa anakaripia. Ni kama mbele yake alikuwapo huyo wa kuitwa Desmund….hapa nilikumbuka kurekodi.

“Mbona alifanya hivyo Desmund!! Naamini alifanya yeye japo sina uthibitisho lakini Desmund alinitafutia sababu maksudi, kivipi mwanamke ambaye nimeamua kupoteza kila kitu kwa ajili yake ashindwe kunisikiliza na kujifanya anamuamini sana Frank, Frank si amekutana naye akiwa ameng’ara tayari, wanajifanya wanajua sana wanaongea kiingereza cha kipumbavu, kiingereza nilichoongea darasa la pili wao wanakuja kukiongea mbele yangu na kujifanya wananificha wanachozungumza. Yaani rafiki yako anakueleza kuwa mkeo ni Malaya nawe unatabasamu unasema ndio ndio….Desmund hivi ulirogwa. Walikuroga Desmund!!! Umuulize basi niliufanya wapi, si ni huyu nilikwambia anavyonitazama sipendi maana anaonyesha matamanio, mwanzoni ukanielewa leo hii anakuletea ujinga kwamba mimi nilikuwa Malaya SAUT (Saint Augustine University Of Tanzania) na wewe unaamini Desmund, ama hakika walikuroga wewe si bure nasema, sio wewe ulifanya mapenzi na mimi mara ya kwanza nikikueleza kuwa sijawahi kushirikiana na mwanaume tangu nizaliwe, sio wewe nilikueleza kuwa nilikuwa nangojewa na bweana wa kiarabu anioe huku nikiwa na bikira yangu, huo umalaya niliufanyia mdomoni we fala!! Nakuuliza niliufanyia mdomoni mimi, au niliufanyaje sasa hadi ukanikuta na bikira yangu. Desmund kumbe u mpumbavu kiasi kile, mimi nikawa mpuuzi nikafanya sherehe kubwa kukutambulisha kwa rafiki zangu kama mchumba wangu. Marafiki wakakutukana kabisa kwa kunong’ona kuwa wewe si saizi yangu, wakakucheka na kimwili chako kilichokondeana, hivi ningekuwa wa kuitwa Malaya wewe nawe ulikuwa mwanaume wa kushiriki nami mapenzi…..au kwa kuwa nilikusifu kuwa unaniridhisha kila siku Desmund. Sikukusifu bure, sikufanya maigizo yoyote mimi, lakini aaah Desmund ukaja kusema mimi ni mzigo tu kitandani tena Malaya wa kutupwa wewe na huyo rafiki yako Frank mnanitukana, kumbuka nilikuokota mimi nilikuokota Deeees niliku…..okotaaa….leo hii unanitupa kwa kishindo, nilikuokota wewe nikiwa nikiwa peke yangu, kwa uamuzi wangu nikatumia pesa zangu mimi mwenyewe!!! lakini unashirikiana na rafiki zako kunitupa Desmund….Desmu…..Desmuuu kweliiii wanifanyia hivi kweli mimi yaani….aaargh!!!” hii haikuzuilika sasa, vifaa vikawekwa kando nikachukua jukumu la kumbembeleza, alilia kwa sauti kuu sauti ilishtua sana, kuna mengi moyo wa huyu dada ulibeba hakika. 
Mimi nikazidi kuumizwa na hii simulizi na kwa mara ya kwanza nikatamani kumwona huyo Desmund ili nimfikishe katika vyombo vya dola kwa unyama huu, japo simulizi ilikuwa nusunusu bado. Japo kwa matukio hayo tu ningeweza kumfikisha pabaya, walau kwa kalamu na karatasi ningemfanya dunia aione chungu na mahali pasipokuwa salama kabisa.

KUMBE!!!!!

MOJA: Mama yake Nadia alimlaani vikali kiasi kile!!! Je ni laana inaishi??

MBILI: Familia ilimtamkia kuwa inamchukia, na wamekaa kimya moja kwa moja ama??

TATU: Desmund na FRANK!! Jina jipya tena huyu naye anamuitaje mke wa mtu Malaya???

NNE: Desmund na kiingereza….hapa niliweka nukuu ili niwe nacheka mwenyewe…hajui ‘boy na girl’ zina maana gani. Huenda elimu ndogo nayo ilichangia.

TANO: Desmund akamkuta msichana ana bikra halafu analeta dharau…bikra zilivyokuwa hadimu!!!

SITA: Hivi wapo wapi hawa akina Desmund mpumbavu na Frank mshenzi?? Swali hili nililihitaji jibu lake sana.

“NADIA…..USILIE NADIA……nipo kwa ajili yamko” niliyasema maneno yale kimoyomoyo huku nikiogopa asiweze kunisikia maana bila shaka alikuwa akiwachukia wanaume wote na mimi nikiwemo…..

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Uwii story inaskitisha hii..

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom