Alhamisi, Oktoba 16, 2014

SIMULIZI YA MAISHA USOLIE NADIA SEHEMU YA 16

Ilipoishia
Nikavaa makubadhi yangu na yeye akajitanda kiremba chake tukafunga chumba na kutelemka chini!!! Huku nikiwa nina wahka wa kujua nini kilijiri??? USIKOSE SEHEMU YA 16

Inapoendelea
Nilimshika mkono Nadia tukakiacha chumba na kuteremsha chini ambapo nia yetu ilikuwa kununua maji ya kunywa. Nadia alikuwa mchangamfu sana tofauti na siku nyingine. Tukakifikia kibanda kidogo maalumu kwa huduma hizo tukanunua chupa mbili za maji ya baridi. Nikafanya malipo tukarejea tena juu.

“Hivi keshokutwa nd’o safari eeh.” Aliniuliza. “Duh unakumbukumbu wewe, mi nilishaanza kunogewa na kanda ya ziwa. Yah! Keshokutwa ndani ya basi tena Dar es salaam hiyo, umepamis eeh!!” nilimjibu huku nikimtazama usoni ataipokea vipi ile hali. Niliamini anatamani sana kufika Dar es salaam maana mazungumzo yetu ya awali kabisa hadi kufikia hapo Mwanza kulikuwa na mazuri mengi sana tuliyoyataegemea jijini Dar es salaam. Jiji hilo ungekuwa mwanzo wa kuungana tena na familia yake iliyobakia. Nilikuwa nimemuhakikishia hilo, nami nilikuwa nimehakikishiwa na watu waliokuwa wameniagiza.

“Dar es salaam, Dar es salaam, Dar Dar es salaam.” Nadia akawa kama anayeimba kwa sauti ya chini, furaha ikapotea usoni mwake na macho yake yakabadilika na kuwa mekundu tena, yakang’ara kwa ishara ya machozi muda wowote.
Tukaufikia mlango wa chumba changu nikaufungua, Nadia akatangulia kuingia na kujirusha kitandani. Mimi nikaweka vifaa vyangu vya kurekodia sawasawia ili kama lipo neno kuhusiana na Dar es saalam ama chochote kile aweze kunieleza nami nirekodi.


“Dar es salaam, dah marafiki zangu enzi hizo wal;ikuwa wananitamani sana nilipowaambia kuwa naishi Dar es saalam, mimi pamoja na wao tuliiona Dar kama paradise na mahali ambapo pana kila aina ya starehe.
Lakini tukasahau kuwa hata mateso pia yanaweza kuwepo, lakini utayafahamu vipi mateso kama wewe mwenyewe hujawahi kuteseka. Shida ikukumbe wewe nd’o utaweza kuhadithia vizuri, hata wewe mwandishi najua unanisikiliza lakini huwezi kujua uchungu nilionao nikikwambia niliteseka.

Dar es salaam si mahali sahihi na niliingia huko nikiitwa Mariam. Jina hili sijui kama lilikuwa sahihi kutoka kwa Jesca maana liliniiingiza pabaya. Baada ya kutekwa na watu nisiowajua na kisha kutupwa katika kile chumba cha watu ambao ni sahihi kuwaita wafu, aah!! Mzee Mwaijande jamani…” alisita akaanza kulia kidogo kisha akaendelea.

“Kila wema upande wa Nadia hawadumu, yaani yule mzee angeishi walau siku mbili hakika yasingenikuta yale yaliyonikuta, mzee wa watu akajifia!! Na walimuua kwa mateso wale. Ni mzee Mwaijande alikuwa walau na uwezo kidogo wa kuzungumza akanieleza kuwa nijipe pole kwani nipo katika tundu baya tayari, tundu la kifo!! Sikumuelewa nikaendelea kumuhoji, akanieleza kuwa kwa sababu mimi nina nguvu ningeweza kulikwepa japo ni hatari kuthubutu kutoroka. Akaendelea kwa shida kuzungumza akaniambia kuwa yeye alikuwa katika ugomvi na mtu akajikuta yumo humo ndani baada ya kuonekana ule ugomvi wa kuwania kiwanja alikuwa akielekea kuushinda. Nayeye akawa kama mimi akashindwa kukiri kuwa yule mpinzani wake ndiye aliyemtupa humo ndani.
“Kwani wewe uligombana na nani.”
“Na mzee Makorani wa hapo hivi Area C”
“Area C wapi tena mzee wangu.”

“Si hapa Dodoma ama wewe si mwenyeji!!” alinijibu bila wasiwasi. Hapo sasa nikapagawa, mimi nilikuwa Mwanza, sasa naambiwa Dodoma. Nikiwa katika hamaniko mara mwanamke mwingine akadai hapo tulipokuwa ni Singida, mwingine akajikaza kazungumza kuwa tupo Mugumu Serengeti. Hapo sasa nikatambua fika kuwa hakuna ajuaye ni wapi tulipo kila mmoja aliletwa bila kujitambua.
Mzee Mwaijande akaendelea kuniambia kuwa humo kuna mawili ama matatu kama yapo, lakini kubwa zaidi ni biashara ya madawa ya kulevya.
“Watakupasua tumbo lako na kuweka madawa yao, si unawaona wenzako hao wote wamesafiri mara kadhaa.” Mwili ukanisisimka kusikia jambo lile. Nilikuwa naona tu katika luninga mambo kama hayo ya mtu kupasuliwa tumbo na kisha kuhifadhi madawa ya kulevya, sasa naambiwa kuwa na mimi nitakuwa mmoja wao.
“Kama wewe ni mrembo wataanza na wewe kwanza kuwafurahisha na baada ya hapo utawatumikia katika biashara yao. Wenzako hao wamekuja humu ndani wakiwa warembo sasa wamejiishia. Mwingine anasema alikuwa Miss wapi sijui, miss Upareni.” Aliposema hivyo nikazifdi kusisimka, kumbe miss Upareni hakufa mwandishi, wala hakupotea katika mazingira ya kutatanisha alitekwa na kisha nafasi yake ikachukuliwa na mtu mwingine. Niliduwaa kwa sababu niliwahi kusoma katika gazeti tukio hilo.
“Lakini wewe unaweza kutoka hai humu ndani. Zipo njia zao mimi kama mkongwe ninazifahamu. Hivi huu ni mwaka gani kwani?” aliniuliza.

Nikamtajia mwaka ambao nilifahamu tupo.
“Doh! Nimekaa miaka mitano humu sasa. Jitahidi utoke binti, ukitoka wewe unaweza kutukomboa na sisi.” Alinisihi na mara milango ikafunguliwa. Wakavutwa watu kadhaa wenye nguvu kiasi. Mimi wakaniacha, nikiwa naduwaa mara wakarejea mara ya pili wakanichukua.
Nikakutana na mwili wa mzee Mwaijande ukiwa mfu tayari. Niliwasikia wakipiga simu na kuwaeleza watu wao kuwa mzee alikuwa amechoka tayari.
Naam simulizi yake ikaishia pale huku akiniacha bila kuijua njia.

Kutoijua njia kukanisababisha nifike Dar es salaam, walinisafirisha katika namna ileile ya kwanza. Sijui sasa kutoka katika nyumba ile hadi Dar ni muda gani lakini pale Dar nikafikishwa katika hospitali ambayo nimeisahau jina lakini inajulikana tu. Tukifika Dar nitakuonyesha. Mwandishi nikiisikia Dar najisikia uchungu, yaani natamani isingekuwepo ama nisingefahamu pale nilipokuwa ni wapi, lakini nilipafahamu na huyo Daktari niliwahi kumwona hapo kabla. Daktari akanichoma sindano ya ganzi hapo nikiwa namuona, wamenifunga kamba ngumu. Bora wangefanya hivyo nikiwa najaribu kujifungua mtoto lakini wao walifanya vile kwa lengo lao la kunibebesha madawa ya kulevya.
Sijui ni kitu gani nilikuwa nimewakosea, nakumbuka nilipiga kelele sana, lakini macho na midomo ikawa mizito. Nikasinzia.

Nilizindukia katika hospitali nyingine, huku sasa walikuwa ni madaktari wengine wazungu. Nikajikuta nimeshonwa tumboni.
Bila shaka walikuwa wamenitumia tayari.
Nilijilaani na kukitamani kifo, lakini kila nilipotamani kufa nikawa namkumbuka Desmund!! Sikutakiwa kufa, nikaamini hivyo.
Baada ya hapo nilipoteza fahamu tena na nikaibukia tena katika kile chumba katika mji tusioujua wote kwa pamoja.

Ule usemi wa kizuri chajiuza na kibaya chajitembeza ulichukua nafasi yake baadaye kidogo. Nilikuwa napewa huduma nzuri sana, nikafanyishwa mazoezi na mara nikawa nalazwa kitandani, sikuchanganyika tena na wale wenzangu, sikujua wana nia gani mpya, nikaendelea kuvumilia. Hadi nilipopona kabisa ndipo nikakutana na mzee wa kiarabu.
Mkutano wetu wa kwanza ulikuwa chumbani tukiwa wawili pekee. Nikiwa uchi wa mnyama. Yeye alikuwa na taulo tu.
Mara akanisemesha kiarabu, nikaambulia baadhi ya maneno maana nilijifunza kutoka kwa baba yangu enzi hizo lakini sikumjibu. Mara akanisogelea na kuanza kunipapasa. Nikajua yale maneno ya Mwaijande yanatimia. Unadhani ningefanya nini na ningekimbilia wapi? Akazidi kunipapasa. Hapo nikanyanyua kinywa changu nikasema nisamehe kwa kiarabu. Akashtuka akaniangalia na kukoma kunipapasa.

“Wewe unatoka wapi?” aliniuliza kwa kiarabu, hilo nalo nikalinasa lakini kujibu ikawa kazi ngumu. Lakini nikajikakamua na kumjibu niwezavyo, “Familia ya Barghash.” Nikajibu
Akaendelea kuzungumza harakaharaka nikamwambia simwelewi, akajaribu kusema Kiswahili, naam Kiswahili kibovu kabisa.
Lakini afadhali nilinasa mawili matatu.
Akanieleza kuwa kama nikiwa mpenzi wake atanisaidia. Ningeanza vipi kumkatalia wakati nilimkatalia mzee Matata na sasa nipo katika matata.

Uhusiano ukaanza siku ile!!
Uhusiano wa kujilazimisha ilimradi kama kweli ataweza anisaidie nitoroke. Nilifanikiwa kujua kuwa yeye hakuwa na sauti ya mwisho, kwani kuna mzee mmoja alikuwa akiamrisha na yeye anatii. Hapo nikajua kuwa kazi ipo.
Jicho la yule mzee mkuu zaidi sijui kama lilikuwa halijawahi kuniona ama vipi, maana siku ambayo nilonana naye alikuwa kama zezeta anayetazama nzi arukavyo na kutua. Akanipandiosha na kunishusha.
Baadaye akahitaji kuonana nami tukiwa wawili tu. Bahati nzuri alikuwa anajua kiingereza na mimi hapo palikuwa nyumbani.
Tulizungumza mengi, na baada ya kutoka hapo nilikuwa na cheo. Cheo katika taasisi nisiyoijua na mbaya zaidi hata sikujua ni nani amesababisha nitupwe hapo na sikujua hata ni nchi gani.
Nikaanza kukitumikia kile cheo, jukumu langu likiwa kuhesabu kila siku ni akina nani wapo hai na wangapi wamekufa! Hivyo tu, kila mmoja alikuwa amefungwa namba mkononi ambayo ilikuwa haivuliwi hadi pale unapofariki.
Mwanzoni nilikuwa muoga sana kushuhudia mtu anavyokufa lakini baadaye na hata sasa ua mtu mbele yangu na wala sitatikisa hata mkono. Nilibadilishwa roho yangu na kuwa ya kinyama sana. Nikawa nawahesabu wenzangu, kila siku lazima mmoja alikufa nikiwa naona. Kila walivyokuwa wanakufa nikawa natamani kushuhudia kifo cha Desmund kwa macho yangu kwa mambo haya magumu aliyonisababishia.
Lakini sikujua hata nilipokuwa.

Baadaye mkuu akanitaka kimapenzi na wakati huo Barakat alikuwa mpenzi wangu. Sikumkataa na yeye nikamwachia anachotaka, sikuwa na thamani mwandishi, thamani yangu ipo wapi? Kama sina uhuru ni kitu gani cha kunilinda? Hakikuwepo….
Nilidhani mkuu yule waliyezoea kumuita masta alinitaka kimapenzi tu kisha basi ajiondokee zake lakini mara akaniganda, kila baada ya juma moja ananivamia na kunitaka kimapenzi.
Siku ya siku ambayo sikuwa naijua hata jina lake baada ya kuishi kwa muda katika mazingira yale. Siku iliyonihamishia katika ukimbizi mwingine.
Mwandishi yule masta alinifumania na Barakat, tulikuwa tumekumbatiana tu kimahaba. Aisee mimi nilijifanya nimezoea kuona watu wakiwa wafu ama wamekufa, kumbe kuna wenzangu wanajua kuua.
Masta alirusha sijui kitu gani kile kikauparaza mkono wa Barakati ukawa kama unataka kukatika, Barakati naye akajitutumua akachomoa jambia akarusha likapasua bega la masta. Hapo sasa wakavaana kimya kimya, mimi nikajua yeyote yule atakayepona ataniua mimi..hapo nikaamua kutimua mbio, kuelekea popote pale ambapo ningeweza kufikia tamati yangu.
Nilikimbia sana na huku nyuma nikasikia sauti ikiita jina langu kwa namna, maana walizoea kuniita 105 (one zero Five)…nikaibaini ile sauti kuwa ni ya yule masta, sikutaka kugeka maana kwa vyovyote vile nilikuwa nakufa. Asingenipa muda wa kujieleza. Mara taa zikazimwa, giza kali na sikujua naelekea wapi tena, lakini sikuacha kukimbia, nilizidi kupenya huku na kule, mara nianguke nasimama tena, sikuwa na uhakika hata asilimia moja kuwa huko mbele kuna njia maana sikuwahi kufika huko. Sauti ya masta sasa niliisikia kwa mbali sana. Nikaendelea mbele, nikafikia vyuma nikajibamiza nakuanguka chini, nikaisikia damu ikivuja kutoka katika midomo yangu.
Nikatulia pale huku nikikisikia kifua changu kikipiga filimbi kila nilivyokuwa napumua. Giza tu ndo macho yangu yaliweza kuona. Nilibaki kushika vyuma vile nikisubiri wafike na kuniua. Maana miguu ilikuwa inavuta sana na sikuwa na nguvu za kuendelea kukimbia na hata ningekuwanazo ningekimbia kwenda wapi??

Nikakumbuka kufanya sala ili Mungu anichukue kabla hawajanifikia ikibidi. Wakati nasali sauti ya masta nayo ikazidi kusogea karibu na masikio yangu.
Alikuwa anatukana matusi ya kiingereza, hakika alikuwa amekasirika maana aliweka na kiapo kuwa akinikamata ananikata vipandevipande. Mwandishi hata sala sikuweza kuimaliza, nikakisubiri kifo changu.
“Nakulaani Desmund na damu hii inayoenda kumwagika, roho hii inayohukumiwa bila hatia Desmund popote ulipo, isiondoke roho hii kabla haijakusulubisha wewe na ukoo wote na kizazi chako chote, Desmund nakufa mimi…nakufa d’o kitu ulichokuwa unataka, lakini nakuaminisha kuwa upendo wangu ulioulipa kwa mabaya haya utakusulubu maisha yako yote, na damu hii haitakauaka kabla haujajutia….” Nilizungumza huku nikiisikia sauti yangu ikijirudiarudia.

Badala ya kusikia jibu kutoka kwa Desmund mara nikasikia nikikamatwa mguu wangu!!
“Mpumbavu, Malaya mkubwa wewe.” Masta alikoroma kiingereza.Nadia nilikuwa nimekamatika.

Hilo likawa neno lake la mwisho kwa kiingereza akaanza kuzungumza kiarabu cha ndani kabisa. Alinivuta lakini sikutaka kumfuata. Niliendelea kung’ang’ania vyuma nilivyokuwa nimeshikilia. Lakini nilijua tu ni mfa maji haishi kutapatapa…….” Akasita kisha akaendelea, “Yaani nimesema maji nd’o nakumbuka tumenunua maji na hadi sasa hatujanywa!! Duh yasije yakawa ya moto tena.” Alisema Nadia kisha akachukua maji nami nikatwaa yangu, hakika makoo yalikuwa yamekaua haswaa!!USIKOSE SEHEMU YA 17

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom