Alhamisi, Novemba 13, 2014

SIMULIZI YA MAISHA USILIE NADIA SEHEMU YA 23



 ILIPOISHIA
Jonas atathubutu kutoa kilio niweze kumziba mdomo, hekaheka ziliendelea katika lile kochi bila shaka walikuwa wakibusiana, na walikuwa wamenogewa hadi pale honi ilipopigwa.
“Ndo hao uliokuja nao.” Stephano aliuliza.
“Nimekuja naye mmoja tu mbona, tumechukua teksi tu walishauri hivyo.” Alijibu mama Aswile sasa niliweza kuisikia sauti yake vizuri.
“Mpenzi yaani nd’o alikukwangua hivi?” mchungaji aliuliza.
“Mwendawazimu sana yule mtoto, namfunga maisha haki ya Mungu!!” aliapa kwa hasira, nami nikazidi kutetemeka lakini sikuhamisha macho kutoka machoni mwa Jonas. USIKOSE SEHEMU YA 23
 
INAPOENDELEA
“Kitu cha msingi wewe muuzie kesi kuwa alimuua mzee wako, hapo tu utamaliza. Ushahidi wa kutosha nitautoa mimi na Monica mtoto wako. Anafia jela huyu, na hapa ujue kitu kimoja yaani akibaki tu ujue muda wowote ule tunaumbuka.” Mchungaji alimsisitiza mama Aswile, na hapo wakasimama kisha wakatoka nje, kimya kikatanda kidogo, nikatega sikio langu kwa makini kabisa na hapo nikasikia vishindo kwa mbali. Wakaingia hadi sebuleni. Nikahesabu miguu iliyokuwa inakatiza pale kupitia upenyo uliopoa chini ya kochi. Walikuwa watu wanne, wote watu wazima. 

“Kwa hiyo yupo na mtoto sivyo.” Aliuliza mwanaume ambaye sauti yake niliitambua kuwa ipo kiaskari.
“Yupo na mtoto ndio, lakini mkorofi na ana nguvu ndo maana nataka tumshike wote yule…” mama Aswile alisema kwa sauti ya uoga. Nikajisikia fahari kuwa kipigo nilichokitoa kule nyumbani kiliacha heshima ya kutosha.


“Siwezi kubabaishwa na msichana hata wakiwa kumi mimi.” Mchungaji Stephano alijitamba, kisha akamalizia “Ila twende tu wote kama unavyosema.”

Wakatoweka pale sebuleni, nami hapo nikafanya tukio la kutumia sekunde chache sana kuokoa uhai na kuendelea na maisha yangu. Nikamkwapua Jonas, kisha nikanyata upesi na kutokea mlango wa sebuleni, huko nikatimua mbio zaidi. Nikaikuta ile gari pale nje, nikajifikiria kuingia ndani ya gari kisha niondoke nayo kwa sababu nilijua kuendesha vyema lakini nikahofia kuzidisha kuyafanya mambo kuwa magumu zaidi. 

Nikaamua kupita kona kadhaa hadi nikafika stendi, nikasimamisha gari, lilikuwa lkimejaza sana na watu walinionea huruma sana kuwa nina mtoto sitaweza kupanda lakini ni gari hilo nilikuwa nalihitaji.
Nikapanda mwanaume mmoja akanisaidia kumbeba mtoto, gari likaondoka nikiwa nimebanwa mlangoni.
Gari lilikuwa linaelekea Mbalizi Mbeya, hapo mfukoni nikiwa na shilingi elfu mbili tu za kitanzania. Sikuwahi kufika Mbalizi hapo kabla na wala hilo halikuwa lengo langu. Kila kituo watu walikuwa wanashuka na hatimaye nikapata nafasi ya kukaa, nikajipekua katika nguo zangu.

Alhamdulilah!! Pesa haikuwepo, nikajipekua huku na kule, hakika pesa haikuwepo. Na katika kipindi hicho yule kondakta alianza kudai nauli kwa watu wote ambao walikuwa wamepandia njiani. Akili ilizunguka upesi sana nikijiuliza nafanya nini iliaweze kunielewa kijana yule ambaye hakuwa na dalili zozote za huruma.

Hatimaye akanifikia nikiwa nimempakata Jonas. Akanidai nauli yake. Nilimtazama kama sijamsikia, na yeye akanidai tena nauli.
“Nimeibiwa kaka yangu!!” hatimaye niliamua kuusema ukweli. Kondakta akaanza kucheka kwa fedheha, ni kama hakuwa tayari kuniamini hata kwa mbali.
“Hadi kina mama mnaanza kuwa wasanii siku hizi.” Akasema kauli hiyo, mimi sikusema lolote lile.
“Haya bwana sadaka yangu hiyo siku nyingi sijatoa sadaka wala sijaenda katika nyumba za ibada.” Alisema kama anayetania kisha kweli akaniacha hadi niliposhuka Mbeya mjini.
Nilijikuta tu nikiona Mbalizi si mahali stahiki kwangu, hivyo nikaamua kuimalizia safari yangu Mbeya mjini, walau hapo ningeweza kuwa karibu na huduma zozote za dharula.
Ilikuwa ni saa tano asubuhi wakati Jonas alipoanza kulia huku akilalamika njaa. Nilijaribu kuitafuta tena na tena ile pesa ambayo awali niliikosa katika gari lakini sikufanikiwa kuiona, nilitafuta kila mahali, nikajaribu kumbembeleza Jonas lakini bado hakuonyesha dalili ya kunyamaza na alikuwa akihitaji chakula. Ukimya wangu usingeweza kunisaidia kitu, nikatembea huku na kule hadi katika mgahawa mmoja wa watu duni. Nikamkuta mwanaume akiwa ameketi na ni kama alikuwa msimamizi wa mgahawa ule. Nikamwendea kwa heshima ya uoga.

Nikamsalimia na kumweleza shida yangu.
“Baba mimi nakuomba unisaidie, nioshe vyombo ama chochote ambacho naweza kusaidia hapa na umpatie mwanangu chakula, mwanangu tu!! Mimi hakuna haja nitahimili lakini huyu mtoto tangu asubuhi ya jana amekula wali kidogo tu!!” nilimsihi. Maneno yakamgusa na bila shaka kilio cha Jonas kutoka mgongoni  kiliam,sha hisia zake, wanawake waliokuwa wafanyakazi pale wakawa wanamtazama ni maamuzi gani atachukua, nadhani hili nalo lilimtia aibu zaidi.
Akafikia hatua ya kunipa chakula bila kunifanyisha kazi yoyote, Jonas akala kwa fujo kabisa kuonyesha kuwa alikuwa na njaa kali. Na mimi nikapewa sahani yangu nikala. Hakika utu aliouonyesha yule baba ulikuwa wa aina yake. Nikamshukuru kwa utu wake kisha nikamfunga mwanangu mgongoni tukaondoka nikiwa bado sijajua baada ya kupata chakula mkile nini kinafuata?
Wazo kuu nilitaka kujua nafika vipi katika mji wa Musoma tena kwa ajili ya kudai haki yangu. Muda nao ulizidi kusogea kuikimbilia jioni nikiwa sina maamuzi thabiti, majira ya jioni ya saa kumi na mbili na dakika kadhaa nilianza kuona hekaheka huku na kule na baada ya dakika kadhaa nikaisikia adhana, hapa nikawaona watu wengi wakiwa wamejikita katika kula na kunywa katika namna ya kuharakisha.
“Kuna nini kwani?” nilimuuliza kijana mmoja muuza karanga aliyekuwa jirani nami.
“Mambo ya kufuturu hayo.” Alijibu kwa ufupi. Ile kusikia neno futuru akili yangu nayo ikapata uhai, si kwamba naweza kupata chakula cha bwelele jioni ile bali naweza kupata na kitu kingine cha ziada cha kuniwezesha kufika ninapotaka. Sikuonyesha mshtuko wowote na badala yake nilitabasamu tu lakini nilikuwa nimepata nguvu mpya kabisa. Na hapo nikajihakikishia kuwa nitalala Mbeya kwa tabu usiku huo tu lakini baada ya hapo nitaondoka na kufikia azma yangu vyema.
Nilikuwa nimemuhoji maswali mengi sana yule kijana na alikuwa ameyajibu vyema, sasa niliweza kuondoka na kutafuta mahali pa kufuturu. Kwa sababu nilikuwa muislamu na niliijua miiko ya dini hiyo hata sikuhangaika sana, mwisho nikapata mahali nikafuturu. Na kama bahati nyumba mbili baada ya mji ule kulikuwa na msiba, nami nikajumuika katika msiba ule. Huko nikajishughulisha na shughuli mbili tatu, lengo langu kuu likiwa ni kupata sehemu ya kulala, Jonas alipata fursa nnyingine ya kucheza na watoto wenzake. Kweli nikalala na asubuhi kulipokucha tu, nikaondoka na kuwa wa kwanza katika ofisi ya mabasi yaendayo jijini Dar es salaam, nikavizia hadi nilipomuona mmiliki wa basi nililokuwa nalihitaji.
Alipoingia tu na mimi nikaingia, nikazuiliwa mlangoni lakini nikajifanya kuwa ni abiria na nina shida na bosi yule. Nikakubaliwa kuonana naye.
Nikaingia ana kwa ana na mkurugenzi.
“Asalaamaleykum Shehe…” nilimsalimia. Akanijibu na kunikaribisha.
Nikachukua nafasi na moja kwa moja nikaingia katika mada iliyonileta.
“Mkuu, mimi si ombaomba lakini nina shida. Nimelitafuta kimbilio sahihi katika jiji hili nisilolijua na nimeona waweza kuwa mtatuzi sahihi. Shida yangu ni moja tu nisikupotezee wakati wao kaka yangu. Nahitaji kufika jijini Dar es saam, nahitaji kufika aidha kwa kusimama katika gari lako na kama ingekuwa inafaa hata kunihifadhi katika sehemu ya kuhifadhia mizigo kwangu ni sawa. Nimetelekezwa jijini hapa, naishi kwa kutangatanga, ukinisaidia tu kufika nyumbani sihitaji jambo lolote lile jingine. Nahitaji tu kufika nyumbani, nikishushwa pale Ubungo tu mimi nitakuwa nimefika, nitazame kwa jicho la huruma, kukataa kwako tu kunifikisha huko basi kiumbe hiki mikononi mwangu kitalala nje tena kikipigwa baridi. Usinionee huruma mimi na wala usitoe maamuzi yako kwa kunitazama mimi bali kitazame kiumbe hiki mikononi mwangu. Sina hata senti tano ya kukinunulia chakula, nisaidie ewe mkuu.” Nilimaliza kuzungumza nilichopanga kusema naye. Maneno yale yakamgusa haswa. Akawa kama anayekosa kauli.
“Kama haitawezekana nielekeze kwa wenzangu walio katika mfungo niwaeleze kama watanisikiliza.” Nikauvunja ukimya. Kauli hiyo ikawa shabaha maana nilijua kuwa amefunga mwezi mtukufu wa Ramadhani, kukataa kwake jambo ambalo lipo ndani ya uwezo wake ni kuiharibu funga yake, na kunielekeza kwenda kwa waislamu wengine basi angekuwa anaikaribisha dhambi waziwazi na pia kuwa katika hatia kubwa.
“Sasa unajua kusimamisha watu siku hizi hawaruhusu na basi langu haliruhusu kabisa…unaitwa nani?” aliniuliza.
“Naitwa Mariam bosi.” Nilimjibu kwa unyenyekevu mkuu.
“Mariam!! Mariam…haya basi kesho njoo asubuhi tuangalie itakavyokuwa.” Aliniambia hatimaye, nikajua kuwa tayari amenikubalia.
“Sijui nikushukuru vipi kwa kunipa nafasi hii hadimu ya kunisikiliza, nitafika hapa asubuhi sana” tuliagana akanipatia shilingi elfu tano.
Siku hiyo sikucheza mbali na stendi kuu!! Na nililala msibani tena hadi alfajiri.
Yule mkurugenzi akakutana nami asubuhi akampa maelekezo kondakta wake, kisha akanieleza kuwa yule atanisimamia hadi nafika jijini.
“Funga yako ni funga ya kweli!! Ubarikiwe sana” nilimweleza wakati naondoka kuingia ndani ya gari na yeye akajibu ‘inshalah’ Wakati nilitegemea kuwa yule bwana ameelekezwa kuwa nisimame ama nikae katika injini haikuwa hivyo, nilipatiwa siti mbele kabisa. Nikakaa!!
Nikajishukuru mwenyewe kwa ujasiri wangu kwani kama si hivyo aibu ingenikutia Mbeya.”
Kondakta alikuwa karibu yangu na mara kwa mara alikuwa akinijulia hali, yeye pia alikuwa mkarimu sana. Tuliingia Dar es salaam majira ya saa mbili usiku baada ya kuharibikiwa gari maeneo ya Iringa.
“Njoo huku dada.” Aliniongoza yule kondakta.
“Itabidi ukae hapa mpaka nitakapokupa maelekezo zaidi aliyonipa.” Alimalizia nami nikamsikiliza kwa makini na kumuelewa huku nikizidi kukumbuka ukarimu wa mmiliki wa magari hayo.” Hapa Nadia akasita na kisha akapiga mwayo mrefu kabla hajaketi vyema na kisha kuendelea.
“Mwandishi si kila mtu anayekwambia amefunga ujue amefunga kweli kuna watu ni majambazi na wenyewe unakuta wanajiita waumini safi kabisa mida ya mchana na wengine mchana wananyenyekea lakini usiku ni wazinzi. Mtu unapoamua kufunga basi usifunge ili fulani ajue wewe umefunga, maana utakuwa unajidanganya wewe mwenyewe, angalia huyu Rama yaani tangu Mbeya hakutia kitu mfukoni na kila mara alidai kuwa ameizoea swaumu tayari alizihesabu tasbihi mikononi na kila alipopata nafasi alionekana kuwa katika tafakari nzito, hali iliyonipelekea kuamini kuwa bosi wa kampuni ile alikuwa ameajiri watu makini na wacha Mungu sana, hata tulipofika Ubungo bado niliendelea kuwa na imani juu ya kampuni hilo la usafirishaji.
Lakini usilolijua ni sawa na usiku wa giza, kama Rama alikuwa vile kwangu bila shaka kwa mtu yeyote yule angeweza kuwa vile na bado akaonekana mtiifu.
Rama aliniweka pale hadi majira ya saa nne na nusu usiku, nilikula chakula kizuri na Jonas alifurahia chakula alichokuwa anakitaka, mwisho Rama alifika na kunitaka radhi kuwa alikuwa anafunga mahesabu kwa magari yote ya kampuni hiyo hapo ndipo nikatambua kuwa yeye ni kondakta mkuu ama la alikuwa ndiye anayeaminiwa zaidi na alipewa cheo fulani.
“Ujue muheshimiwa akisikia upo hapa hadi muda huu atachachamaa sana.” Alisema tena katika namna ya hofu kiasi, na hapo akanichukua na kuniongoza katika taksi. Mimi nikiwa kama kondoo nafuata kile ninachoambiwa, taksi ilienda kwa mwendo mfupi tukashuka na kuingia katika katika hoteli jirani tu na stendi ya Ubungo. Hapo tukaingia katika hoteli hiyo ambayo nilihisi kuwa amelipia chumba tayari, akanipeleka moja kwa moja hadi katika chumba hicho.
“Hii ndiyo hoteli ya bosi, akiwa na wageni wake huwa wanafikia hapa na gharama zote juu yake.” Alisema kauli ambayo ilinitoa hofu kabisa na kurejesha tumaini tena. Ukarimu wa mkurugenzi ule ulikuwa wa aina yake.
Chumba kilikuwa kikubwa!! Ramadhani akanielekeza kila kitu mle ndani na kisha yeye akatoka na kuahidi kurejea baadaye iwapo itabidi.
Kauli yake ikanitia utata, tayari ametukabidhi chumba sasa kwa namna gani tena anasema atarejea wakati ni usiku mnene ule?
Nikaipuuza kauli ile nikiamini ameitoa kimakosa, kwanza likuwa katika mfungo wa Ramadhani kama lilivyo jina lake sikutegemea kama atataka kuwa karibu na msichana yeyote yule kwani kwa kufanya hivyo ni kujikaribishia majaribu.
Kukumbuka kuwa huo ulikuwa mwezi wa toba kukanitia nguvu!! Nikapanda kitandani na kulala, niliangaza funguo niweze kufunga chumba sikuziona, nikajisahihisha kuwa huenda ni ushamba wangu labda mlango ule haufungwi kwa funguo.
Baada ya hapo nikajitupa kitandani na kujaribu kuutafuta usingizi huku nikiwa na maswali kuwa kesho yangu itakuwa vipi………hapo nikamsahau Ramadhani..” Nadia akapiga tena mwayo mrefu.
“Vipi ni njaa ama!!!”
:Yaani kama vile upo katika akili yangu, nina njaa kali kwakweli. Leo waambie walete chai ya maziwa na chapatti maana siku nyingi sana sijala halafu nd’o zitatibu njaa yangu.” Akanielekeza, nikanyanyua simu na kupiga kwa wahudumu. Nikasikilizwa, kisha nikaambiwa muda si mrefu tutakidhiwa haja zetu.
Hapo sasa maongezi yakawa juu ya vyakula mara Nadia aseme anapenda hiki nami namwambia napenda kile, mara aseme hiki anajua kukipika mimi nijigambe najua kupika zaidi yake. Mambo yalienda hivyo hadi muhudumu mnene alipokigonga chumba. Nikaenda kukifungua nikampokea alichokuwa amebeba. Alikuwa anathema juu juu. Nadia akauliza kulikoni.
“Nimepanda ngazi aisee leo lifti mbovu.” Alilalamika huku akitweta. Mimi nikampa pole, Nadia akaguna huku akibetua midomo.
Muhudumu alipoondoka nikamuuliza Nadia kulikoni mbona anaguna.
“Si namshangaa huyo kaka, yaani hivi vingazi sijui vingapi vinamtoa jasho hivyo, dah kuna watu wamezoea raha duniani jamani. Hivi mwandishi hizo chai na mtoto wa miaka miwili kipi kizito.’ Aliniuliza.
“Mtoto hata kama ni wa mwaka mmoja atakuwa mzito kupita chai.” Nilimjibu.
“Na ghorofa mbili na kumi na moja wapi kuna ngazi nyingi?” akauliza tena.
“We Nadia nawe, ghorofa kumi na moja kuna ngazi nyingi mbona..”
“Sasa huyu mkaka anavyolalamika hizi ngazi ngapi sijui je ingekuwa ngazi mia angeweza huyu kweli ama ndo angefia njiani!!!”
“Sio yeye tu hata mimi na wewe hakuna wa kupenya pale kirahisi bila kukomea njiani ama kuchoka sana.” Nilimpinga Nadia. Hapa sasa badala ya kukaa vyema kunywa chai akakaa vyema kusimulia ilimradi tu anithibitishie jambo analotaka kuniambia.
“G nitake radhi, yaani hizo ngazi zinishinde…labda kama hujafikwa na matatizo wewe na unaenda tu kwa starehe, lakini mimi niliziona chache sana siku hiyo. Tena ni siku ile ambayo Rama alitupeleka katika kile chumba akidai kuwa ni bosi wake amemwambia atuchukulie, mimi nikalala nimebweteka mara nasikia mpapaso, nakuja kustuka nakutana na Rama. Akanifanyia ishara ya kukaa kimya. Nikaamka na kuketi. Rama akataka kuendelea kunipapasa nikamzuia, hapo usingizi wote ukaisha.
“Rama wewe si umefunga wewe!!” nilimuhoji.
“Kufunga mchana bwana muda huu nimefungua lakini.” Lijibu kwa kujiamini, nikamlaani yeye na wengine wote ambao wanajifanya watakatifu mbele za watu wakati wakiwa mafichoni wanafanya mambo yao ya hovyo kwa sababu tu hakuna awaonaye.
“Rama hapana….” Nilikataa. Akaendelea kunipapasa.
“Sikia Mariam, mimi ni kondakta mkuu hapo, na hiki chumba wala si bosi nimekuchukulia mimi hapa upumzike mtoto mzuri, sasa wewe kigumu kwako nini eeh!! Wewe tufanye kisha nitaongeza pesa utaishi hapa na mtoto wako mambo mengine tutaangalia yanakuwaje.” Aliniongelesha katika maudhui ya kihuni, jambo ambalo sikupenda kabisa. Rama alionekana kuzichukulia shida zangu kama mtaji, hivyo kwa kuniambia tambo zile alijua kuwa lazima nitaingia mtegoni. Hakujua mimi ni wa aina gani, hakujua kuwa kama isingekuwa kudhulumiwa ningekuwa na pesa na mali nyingi tu na huenda tusingeweza kukutana katika mazingira yale katika namna yoyote ile.
“Rama naomba mimi nilale na kesho uniache tu nitaenda ninapojua kaka yangu.” Nikamsihi tena lakini Rama hakuonekana kuwa tayari kuniacha wakati amegharamia chumba.
“Mariam eeh acha utoto basi, kwani wewe bikra hadi ujifanye kubana, wamekuzalisha huko wamekukimbia watu tunataka kukuweka mjini wewe unaleta pozi za kishamba hapa??” sasa aliongea kama anayegombeza na wakati huohuo analazimisha.
“Rama nakuomba ujiheshimu basi….ona aibu mwanangu huyu hapa unataka kunifanyia mambo ya dharau kiasi hicho, acha Rama naomba utoke humu chumbani ama mimi na mwanangu tutoke twende tunapojua.” Nilimsihi huku nikihisi jazba ikianza kunipanda, Rama alikuwa ananikera na hapo hapo nikamkumbuka Ramso yule mwanaume aliyenilawiti jijini Mwanza. Nikawachukia Rama wote, hakika nilijiaminisha kuwa akina Rama wote ni walewale. Hasira ikanipanda maradufu, sasa nikawa najisikia kutetemeka. Sikutaka aniguse tena, lakini alionekana kutojali.
“Kwani bila haya mambo huyu mtoto ungempata mbona unaleta mambo ya kitoto kama umezaliwa jana.” Aliniambia kwa jazba. Sasa alikuwa akinizongazonga kama anayelazimisha.
“Sikia Mariam, kwani wewe unataka shilingi ngapi? Sema nikupe!!!”
“Rama sihitaji chochote kutoka kwako, mimi sio changudoa, sijiuzi Rama.” Nilijitahidi kuwa mstaarabu lakini bado haikuwezekana.USIKOSE SEHEMU YA 24

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

tunaomba adella uendelee na simulizi ya kosa langu nini? au imwesha ili tujue mwisho wa joyce na fredi.asante

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom