Alhamisi, Julai 16, 2015

TUWE MAKINI"Siasa zisiwe chanzo kukaribisha maafa ya mafuriko Jangwani Dar."


Kuna mgogoro umeibuka katika eneo la Jangwani jijini Dar es Salaam. Watu wanaodaiwa kuwa ni wafanyabiashara ndogondogo maarufu kama 'machinga' wamevamia eneo hilo na kuanza kuuziana maeneo ya viwanja kwa ajili ya kufanyia biashara zao.
 
Taarifa zinaeleza zaidi kuwa wahusika wanagawiana maeneo hayo kwa kuuziana kila kipande kwa kati ya Sh. 50,000 na kuendelea. Kutokana na hali hiyo, Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala ameingilia kati na kutangaza kusimamishwa mara moja kwa mpango huo huku akiwataka wote waliopo kuondoka mara moja.
 
Kadhalika, Mkurugenzi huyo amekaririwa akikiri kuwa awali, wao (Manispaa ya Ilala) na serikali walikubaliana kugawa sehemu ndogo ya eneo hilo kwa wafanyabiashara wadogo ili walitumie kwa shughuli zao, lengo likiwa ni kupunguza msongamano katika eneo la Soko la Kariakoo. Kwamba, hao waliovamia sasa kabla ya utaratibu kutolewa wanatakiwa kuondoka mara moja kwa vile wanakiuka sheria kwa kujimilikisha eneo hilo kinyemela, tena bila kusubiri kuwekwa kwa miundombinu muhimu kama ya vyoo.
 
Hakika, taarifa hii ya kuligawa eneo la Jangwani kwa Wamachinga inashangaza. Sisi hatudhani kwamba ni jambo lenye manufaa kwani eneo hilo hukumbwa na mafuriko mara kwa mara. Kwa sababu hiyo, tunashauri kuwa mpango huu usitishwe siyo kwa wavamizi tu bali kwa yeyote. Badala yake, mkurugenzi na viongozi wengine wa Ilala waendelee kukamilisha mipango yao ya kuandaa maeneo sahihi ya kuwapeleka wafanyabiashara hao, yakiwamo yanayotajwa kuwa katika maandalizi ya Mchikichini, Kisutu na Buguruni.
 
Tunatoa tahadhari hii kutokana na ukweli kuwa eneo la Jangwani siyo salama hata kidogo. Kijiografia, Jangwani ni mojawapo ya eneo la mapitio ya maji yaendayo katika Bahari ya Hindi. Hukumbwa na mafuriko karibu katika kila msimu wa mvua. Hata aliyewahi kuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka, aliwahi kutoa tahadhari juu ya matumizi ya ardhi kwa shughuli za aina hiyo kwenye eneo lote la Bonde la Msimbazi kwa maelezo kuwa ramani ya mipango miji ya Dar es Salaam inalitaka liwe huru kupitisha maji yanayokwenda baharini, tena yakitokea katika maeneo mbalimbali yakiwamo ya Vingunguti na kwingineko.
 
Ipo mifano mingi juu ya athari ambazo hutokea kila mara kwa wote wanaokiuka ukweli huu kuhusu eneo la Jangwani. Kwa mfano, Desemba 2011, taifa lilipatwa na msiba mkubwa baada ya watu zaidi ya 10 kufariki dunia na wengine kadhaa kukosa mahala pa kuishi baada ya kukumbwa na mafuriko katika maeneo wanayoishi yaliyo kwenye mapitio ya maji jijini Dar es Salaam. Wengi miongoni mwa waathirika wa mafuriko hayo walikuwa ni wakazi wa maeneo ya Jangwani na kwingineko katika ukanda wa Bonde la Msimbazi. Maafa mengine yaliyotokana na mafuriko katika maeneo ya Jangwani na maeneo mengine ya mabondeni jijini Dar es Salaam yalitokea pia Mei mwaka huu. 
 
Kwa kuzingatia yote hayo, sisi tunaona kuwa uamuzi wowote ule wa kuwapeleka wamachinga Jangwani haufai. Ni kwa sababu unawaweka wahusika katika hatari kubwa ya kupoteza maisha yao na mali zao, hasa  kutokana na ukweli kuwa wakati mwingine, mafuriko hayo hutokea ghafla kutokana na mvua kubwa ambazo hunyesha mbali na jiji la Dar es Salaam.
 
Sisi tunadhani kuwa badala ya kufikiria mipango ya kuwahamishia Wamachinga Jangwani, Manispaaa ya Ilala iangalie uwezekano wa kuwaondoa watu wote walio katika eneo hilo ili kuepusha maafa ya kujitakia. Kama hiyo haitoshi, itafute pia uwezekano wa kuwatumia wataalamu wa mazingira kuishauri serikali juu ya umuhimu wa kuhakikisha kuwa eneo lote la mapitio ya maji jijini Dar es Salaam linaachwa huru, hasa kwa kuzingatia maelekezo ya ramani za mipango miji. Kinyume chake, ni sawa na kukaribisha maafa ya mafuriko yatakayoleta kilio siku moja.
 
Aidha, sisi tunatambua kuwa katika kipindi hiki cha kukaribia uchaguzi mkuu huwa kuna baadhi ya maamuzi hufanywa na wanasiasa kwa minajili ya kuwafurahisha wapiga kura wao. Tunahofia kuwa uamuzi huu wa kutaka kuwahamishia Wwafanyabiashara katika maeneo ya Jangwani unaweza ukawa ni miongoni mwa nguvu za siasa katika kipindi hiki. Na kama hivyo ndivyo, basi tunashauri kuwa harakati hizo ziachwe mara moja. Mkurugenzi na watendaji wengine wa Manispaa ya Ilala watangulize weledi wao katika kila wanachoamua ili kuepusha maafa yanayoweza kuepukika kirahisi. Hili lizingatiwe.
 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom