Jumatano, Julai 29, 2015

WASEMAVYO WADAU KUHUSU UAMUZI WA LOWASA KUHAMIA CHADEMA.


Uamuzi wa jana wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kujitoa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kujiunga na Chama cha Demokrasia na maendeleo (Chadema), wananchi kadhaa wametoa maoni tofauti kuhusiana na uamuzi wa mwanasiasa huyo.
 
MAKAMU RAIS TEC
Makamu wa Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Mhashamu Severine Niwemugizi, alisema hatua ya Lowassa ni ukomavu wa vyama vya siasa nchini hasa vya upinzani kuwa mtu yoyote anaweza kuhama na kujiunga na chama chochote.
 
Alisema kuhama kwa Lowassa kunatafsiri kuwa mchakato wa uteuzi ndani ya CCM haukumridhisha.
 
“Tafsiri ni kuwa ameona CCM haikumtendea haki na kama binadamu yeyote ana haki ya kuchukua hatua kama binadamu mwingine, mtu anapoona hajatendewa haki kama binadamu uamuzi ni wake kuondoka kama wengine wanavyobadilisha vyama, hatushangai ni jambo linatokea kwa wengi siyo la pekee sana,” alisema na kuongeza:
 
 
“Tafsiri nyingine ni ukomavu wa vyama vyote vinaendelea kukua kiasiasa, kusema vyama vya upinzani havijakomaa siyo kweli, kama kiongozi wa juu anaweza kuona chama cha upinzani ni mbadala, wasiendelee kushambuliana kwenye majukwa.”
 
Askofu Niwemugizi alisema Lowassa siyo wa kwanza kukihama chama tawala kwani kuna nchi nyingi hata marais wanahama vyama vyao waliwahi kuhama, hivyo ni ukomavu wa demokrasia nchini.
 
Alisema anaamini Lowassa ataleta ushindani mkubwa, kwani mchuano utakuwa mkali kwa kuwa watanzania wengi wanamuunga mkono huku Mgombea wa CCM, Dk. John Magufuli, naye anaungwa mkono.
 
“Matarajio ya umma ni makubwa, tunachoomba kusiwe na rafu kila mmoja awe muungwana wakati wa kampeni,” alisema.
 
Mwenyekiti wa CCK, Constantine Akitanda, alisema hata katibu Mkuu wa zamani wa CCM, Hayati Horace Kolimba, alikihama chama hicho, hivyo ni jambo la kawaida na ni haki yake.
 
“Kuhama Chama ni haki ya kidemokrasia ya kila mtu, kama unaona mfumo unakubana katika chama ulipo haufai unaweza kuhama ukaenda mahali ambapo unaona ni sahihi, hilo siyo jambo baya,” alisema Akitanda.
 
Mwenyekiti wa Alliance For Democratic Change (ADC),  Said Miraaj, alisema kabla ya kurejesha mfumo wa vyama vingi  ilikuwa ngumu kuhama chama, lakini baada ya kurejeshwa mfumo huo ilimpa uhuru kila mtu kujiunga na chama anachotaka.
 
 
Alisema  alichokifanya Lowassa siyo kitu cha ajabu kwa kuwa hata  wengine waliopita walishawahi kufanya hivyo kwa kuwa ni  haki ya kila mtu kujiunga na chama chochote anachoona kinamfaa.
 
Alisema wapo waanzilishi katika vyama mbalimbali waliovihama vyama vyao licha ya kwamba walivianzisha na kwamba asilimia 80 ya wanzilishi wa vyama hivyo walivihama.
 
Mwenyekiti wa Chama Cha  United Peoples Democratic Party (UPDP), Fahmi Dovutwa, alisema uamuzi wa Lowassa siyo mbaya kwa kuwa ana haki ya kufanya hivyo.
 
“Mimi sioni ubaya kwa Lowassa kuhamia Chadema kwa kuwa ni haki yake ya kidemokrasia, wala sioni ubaya Chadema kumpokea  kwa kuwa ndiyo kazi ya chama cha siasa kuongeza wanachama,” alisema Dovutwa na kuongeza:
“Labda kaona hapo alipokuwa hawezi kutimiza malengo yake na huko alikoenda atatimiza malengo siyo mbaya , mimi naona  alichofanya ni sahihi.”
 
DK. Bana Mhadhiri Mwandamizi wa Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaa (UDSM), Dk. Benson Bana, alisema ni haki ya kila Mtanzania kuhama au kuchagua chama anachoona kinamfaa.
 
Alisema maamuzi ya Lowassa ni haki yake ya kidemokrasia, hivyo maamuzi yake yanahitaji kuheshimiwa.
“Naona yuko sawa, lakini kama kweli atahamia Ukawa bado naona atakuwa amekwenda kwa ajili ya kupata madaraka iwapo atateuliwa na Ukawa kugombea urais,” alisema Dk. Bana.
 
Alieleza kuwa Lowassa atakuwa sahihi endapo atakuwa amejiunga Chadema kwa sababu ya kushawishika na sera za Chadema kwa malengo ya kuzitumia na kukijenga chama, lakini si kwenda huko na kupewa nafasi ya kugombea urais.
 
Alieleza kuwakama Ukawa wanaweza kumsimamisha kuwania nafasi hiyo kubwa wanajifedhehesha na kuwaaminisha Watanzania kuwa Lowassa ni mkubwa kuliko taasisi zilizounda Ukawa.
 
“Akiwania urais inatupa ukakasi kwani haiwezekani taasisi zote zikamsimamisha mtu mmoja pekee ambaye hakuwepo katika umoja huo, itamaanisha kuwa amezinunua taasisi zote hizi. Pia Ukawa wasishangae kuitwa CCM namba mbili kwani sasa watamsimamisha mgombea anayetokana na CCM,” alisema Dk. Bana.
 
KIJO BISIMBA
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk. Hellen-Kijo Bisimba, alisema kitendo cha Lowassa kujiunga na Chadema hakimaamishi kuwa kweli ana wito wa kuwatumikia Watanzania.
 
“Kama anakwenda huko ni haki yake, lakini kama anajiunga na umoja huo ili kutaka kuwania nafasi ya urais ni wazi kuwa anafanya hivyo kwa maslahi binafsi,” alisema Bisimba.
 
Alieleza kuwa kama Lowassa kweli alikuwa na dhamira ya dhati ya kuwasaidia Watanzania, angefanya hivyo akiwa ndani ya chama chake.
 
“Chama alichotoka Lowassa hakiendani kabisa na sera za chama anachokwenda, sasa anawezaje kwenda huko na kupewa madaraka badala ya kuwa mwanachama kwanza?” alihoji na kuendelea: “Huku ni kutafuta madaraka.”
 
 “Kama Lowassa atapatiwa nafasi hiyo ni wazi kuwa kimwili atakuwa na umoja huo, lakini akili na mawazo yake yatakuwa bado yako CCM kwani lengo na dhamira yake ni kupata uongozi na atakuwa hajaachana na itikadi za chama chake,” alisema.
 
NICOLAUS MGAYA

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom