Alhamisi, Agosti 13, 2015

ISOME KWA UMAKINI "Mitandao ya kijamii isiibue mfarakano"



Kilio kuhusiana na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii kinaendelea kushika kasi. Taasisi za umma na binafsi zimeendelea kukumbwa na athari za matumizi mabaya ya mitandao hii.  Kadhalika, watu binafsi pia hawako salama.

Kuanzia wasanii, viongozi wa kisiasa,  wakuu wa taasisi na idara mbalimbali na hata wananchi wa kawaida wamekuwa wakikumbana na athari hizi zitokanazo na taarifa potofu zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii.  

 
Hakika, hili ni tatizo. Ni kero kubwa kwa jamii ambayo ni dhahiri kuwa ikiachwa iendelee kama ilivyo sasa, ni wazi kwamba taifa linaweza kupata madhara makubwa ya kiuchumi, kisiasa na kijamii.  Sisi tunalaani matumizi haya mabaya ya mitandao ya kijamii. 
 
Tunaamini kwamba sasa ni wakati muafaka kwa wananchi wote kuungana na vyombo vya usalama katika kupambana kila uchao dhidi ya matumizi mabaya ya mitandao hii.  Kadri inavyofahamika, kuwapo kwa mitandao hii ya kijamii kama ya facebook, twitter, instagram na blogu mbalimbali kuna manufaa makubwa. Ni kwa sababu uwapo wake unatokana na matunda ya kukua kila uchao kwa teknolojia ya habari na mawasiliano. Hali hii hutoa fursa ya kuwaweka karibu zaidi watu wa mataifa mbalimbali. 
 
Kupitia mitandao ya kijamii, dunia sasa imekuwa kama kijiji. Kinachotokea eneo moja la uso wa dunia kinawafikia wengine walio katika ncha tofauti ya dunia kwa haraka, uhakika na ubora wa kiwango cha juu. wa mfano, kupitia kukua huku kwa teknolojia ya habari na mawasiliano, sasa ni rahisi zaidi kwa wakulima walio katika kijiji ‘A’ kinachotegemea kilimo kama njia kuu ya uchumi kupata taarifa za soko la mazao yao. 
 
Hili huwezesha biashara kufanyika kwa ufanisi na mwishowe kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla. Na huu ni mfano mdogo tu wa faida za kukua huku kwa teknolojia ya habari na mawasiliano kunakowezesha watu kupashana habari kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii.  Hata hivyo, inafahamika kuwa palipo na faida, hasara huwa hazikosekani.  Mitandao hii ya kijamii huwa na athari nyingi hasi pindi isipotumika vizuri. Kwa bahati mbaya, taifa letu lingali likikabiliwa na tatizo hili la matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii. 
 
Baadhi ya watu husambaza taarifa za uongo zinazoibua hofu na mfarakano. Wengine hutoa taarifa zinazotishia usalama wa taifa. Amani na utulivu huwa shakani. Zipo pia taarifa zinazopotosha umma kuhusiana na masuala ya afya. Mambo yote haya hayavumiliki hata kidogo. 
 
Mifano kuhusiana na matumizi mabaya ya mitandao iko mingi. Mathalan, katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25, baadhi ya watu wamekuwa wakisambaza taarifa nyingi potofu. 
 
Mmoja wa waathirika wa vitendo hivi katika siku za hivi karibuni ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Ghalib Mohamed Bilal. Wasambazaji wa taarifa potofu walieneza uvumi kupitia mitandao ya kijamii kuwa kiongozi huyu wa juu amekihama chama chake tawala (CCM) na kuhamia upinzani. 
 
Hali hii haipendezi hata kidogo. Kwa sababu hiyo, sisi tunadhani kwamba kuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba vitendo hivi vinadhibitiwa. Vikiachwa vinaweza kuibua mfarakano kila uchao katika jamii. Na tunatambua kuwa hii siyo kazi ndogo. Hata hivyo, inawezekana kudhibiti hali hii ikiwa kampeni endelevu za kuelimisha jamii kuhusiana na matumizi ya mitandao ya kijamii itafanyika bila kuchoka. Vyombo vya dola viendelee kuimarishwa kadri inavyowezekana, hasa katika idara zao za mawasiliano ili mwishowe kupunguza athari za matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii. 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom