Jumatano, Agosti 26, 2015

TUSISAHAU HILI "Tujipange mapema kukabili El-Nino".


Kuna taarifa kuwa Tanzania na nchi nyingine za ukanda wa Afrika Mashariki ziko katika hatari ya kukumbwa na mvua kubwa za El-Nino katika kipindi cha kuanzia mwezi ujao hadi Desemba, 2015.
 
Taarifa iliyomkariri Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) ilieleza jana kuwa tishio hilo linatokana na kuwapo kwa ongezeko la joto katika Bahari ya Pacific na kwamba, wananchi wanapaswa kuwa macho kuanzia Septemba Mosi kwa kufuatilia taarifa zao (TMA) ili kujua hali itakavyokuwa.
 
Sisi tunawapongeza TMA kwa kutoa taarifa hii mapema, tukiamini kuwa kwa kufanya hivyo, wananchi na wadau wengine wa masuala ya hali ya hewa watakuwa na nafasi ya kujipanga kukabiliana na mvua hizo. 
 
Hata hivyo, pamoja na tahadhari hiyo itokanayo na taarifa za kitaalam, bado kuna uwezekano wa kutofanyiwa kazi kwa taarifa hiyo. Uzoefu unaonyesha kuwa siyo wananchi wote huchukulia kwa uzito unaostahili tahadhari za aina hii. Vilevile, siyo mamlaka zote zinazopaswa kutumia taarifa hizi zitatekeleza wajibu wao kwa kujiandaa mapema ili kupunguza makali ya El-Nino.
 
Ni katika kutambua ukweli huo, ndipo sisi tunapoona kuwa sasa kuna kila sababu kwa wananchi na wadau wengine wote wanaoguswa na taarifa za TMA kuanza kujiandaa katika kukabiliana na athari za El-Nino. 
 
Tunakumbushia jambo hili huku tukiamini kuwa athari za mvua hizi siyo ngeni. Ziliwahi kutokea nchini na kusababisha maafa makubwa. Madaraja yalibomolewa, miundombinu ya barabara iliharibiwa vibaya na mazao ya chakula yaliangamizwa na mvua hizi zinazonyesha mfululizo, kwa kasi na kwa wingi. Uchumi wa nchi na pia wa watu mmoja mmoja uliwahi kutikiswa na mvua za El-Nino. Siyo jambo dogo.
 
Sisi hatuombei balaa hili kujirudia. Bali, tunadhani kwamba kipindi hiki ambacho El-Nino bado haijatua kitumiwe kwa maandalizi kabambe. 
 
Tunasisitiza kuwa tishio hili la El-Nino lisifanyiwe mzaha. Watu wanaoishi maeneo ya bondeni ni vyema wakawa wa kwanza kujiandaa kwa kuhakikisha kuwa wanahama mara moja, hata ikibidi wafanye hivyo kwa muda ili kujinusuru na baa la mafuriko linaloweza kuzimeza nyumba zao na kutishia uhai wao.
 
Kadhalika, wakulima watumie pia taarifa hizi kwa kuhakikisha kuwa wanachukua hatua za kukabiliana na njaa itakayotokana na baadhi ya mazao yao kusombwa na mvua. Mamlaka za serikali, zikiwamo halmshauri za wilaya, manispaa, miji, majiji na taasisi nyingine za umma zinazoshughulikia miundombinu ya barabara kama Wakala wa Ujenzi wa Barabara (Tanroads) zinapaswa kujiandaa mapema vilevile ili kuhakikisha kuwa madhara yatokanayo na mvua hayawi makubwa kiasi cha kuligharimu taifa fedha nyingi. 
 
Muhimu kuzingatia ni kuhakikisha kuwa yale yote yanayoweza kufanywa sasa ili kukabiliana na athari za mvua za El-Nino yafanyike mapema ili hali itakapokuwa mbaya tayari kuwe na majawabu ya namna ya kuikabili. 
Mathalan, kama kuna mitaro ya maji ya barabara imeziba, ni vyema ikasafishwa sasa ili kuruhusu maji kupita kwa urahisi pindi mvua zitakapoanza kunyesha na hivyo kujiepusha na ukubwa wa mafuriko utokanao na tatizo hili.
 
Shime, taarifa za TMA kuhusiana na tishio la mvua za mafuriko zifanyiwe kazi sasa ili kupunguza madhara. Tujipange.
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom