Alhamisi, Novemba 26, 2015

Posho za vikao vya wabunge zitazamwe kwa undani zaidi.

Wabunge wawili, Elibariki Kingu, wa Singida Magharibi (CCM) na Zitto Kabwe, wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), wamezua mjadala kwa kitendo chao cha kuamua kutochukua posho za vikao vya Bunge (sitting allowances).
Kingu alizungumza na waandishi wa habari kuhusu suala hilo na pia Kabwe amekuwa akielelezea msimamo wake kupitia maandiko yake kwenye mitandao ya kijamii.
Wabunge hao wamekataa posho ya vikao ya Sh. 220,000 kwa siku wakidai kuwa siyo sahihi.
Wanaona kuwa si sawa kwao kuchukua posho hiyo wakati wanalipwa mshahara wa kila mwezi na posho ya kujikimu wanapokuwa kwenye vikao vya Bunge.
Kwa hatua hiyo, wabunge hao katika miaka yao mitano, watakuwa wameachia Sh. milioni 200 kila mmoja na wametaka zielekezwe kufanya shughuli za maendeleo.
Hatua hiyo imekuja wakati Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dk. John Magufuli, ikichukua hatua kali za kubana matumizi ya serikali. Hivi karibuni, Rais Magufuli alizuia viongozi kusafiri nje akitaka badala yake fedha hizo zielekezwe kufanya shughuli za maendeleo.
Pia Rais Magufuli alipunguza fedha zilizochangwa kwa  sherehe ya kuwapongeza wabunge na kuelekeza fedha zilizobaki zikanunue vitanda na dawa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Pia alifanya uamuzi mgumu wa kufuta gwaride na shamrashamra za sherehe za Uhuru na kuagiza kufanyika usafi nchini nzima ili kukabiliana na ugonjwa wa kipindupindu. 
Hatua ya wabunge hawa wawili, pia tunaishauri serikali iangalie utoaji posho kwa wabunge pamoja na watendaji wa serikali. Hii inatokana na ukweli kwamba, siku za karibuni umezuka mtindo wa kulipana posho miongoni mwa watendaji wa serikali hata kama ni kazi zao za kila siku wanazolipwa mshahara. Moja ya vitu vinavyokwamisha maendeleo ya nchi yetu, ni kutokana na serikali kuwa na matumizi 
 makubwa yasiyokuwa ya lazima.
Na jambo la kusikitisha zaidi fedha nyingi zimekuwa zikipotea kutokana na matumizi makubwa tena yasiyokuwa na tija kwa wananchi. Mathalan, fedha nyingi zimekuwa zikielelezwa kwenye masuala ya posho na safari na pia kwenye manunuzi. Itakuwa jambo zuri ikiwa Serikali na Bunge vitaangalia madai haya ya wabunge na kupima ulazima kwa posho za vikao kwao.
Serikali inapaswa kuweka mkazo kwa kuhakikisha kuwa mapato yake yanaelekezwa kuinua hali za wananchi na si vinginevyo. Wananchi wanapenda kuona wakinufaika na maendeleo ya nchi yao na siyo kuwanufaisha wachache.
Wakati wa kampeni, watu hupita sehemu mbalimbali kuomba kura huku wakiahidi kuinua hali za maisha ya wananchi. Kila kunapokuwa na hali ngumu ya uchumi, viongozi wetu wamekuwa mstari wa mbele kuwaomba wananchi kuvumulia huku wakiahidi hali itatengemaa.
Mathalan, wengi wanakumbuka kuwa mwaka 1979, mara baada ya kumalizika kwa vita vya kumng’oa dikiteta Nduli Iddi Amini, wa Uganda, Nduli Iddi Amin, wananchi walipoombwa kujifunga mkanda kwa miezi 18.
Tunashauri Bunge na Serikali kuangalia kwa mapana na marefu suala hili la posho kwa kupima hali ya uchumi wetu na uwezo wa serikali ili kupunguza masuala ya kulipana posho nyingi wakati wananchi wakiteseka na ugumu wa maisha. 
Itakuwa jambo jema ikiwa viongozi wetu watakuwa tayari kujibana na kukumbuka kuwa wakati wao wakifaidi vinono, kuna watu wanapata shida kupata hata mlo mmoja kwa siku.
CHANZO: NIPASHE

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

AMA KWELI TANZANIA SI NCHI MASIKINI
ANGALIA POSHO YAO KWA SIKU MIE WAKATI MWINGINE SIJUI NTAWALISHA NINI WANANGU

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom