Ijumaa, Januari 08, 2016

NI KWELI, TRA ikienda na kasi hii, Tanzania itasahau kibaba cha omba omba

 
Hii ni baada ya kukusanya mapato ya Sh. trilioni 1.3 Novemba, mwaka jana ambayo pia ilikuwa rekodi serikali ya awamu ya tano ilipongia madarakani na kufanya mabadiliko kwenye uongozi wa TRA na kudhibiti ukusanyaji mapato.Ni jambo la kupongezwa kwani ni miaka mingi viongozi walijenga dhana kuwa Tanzania ni maskini isiyoweza kujitegemea.
 
Matokeo yake wananchi wamekuwa wakiishi kwa mateso makubwa kwa kuaminishwa kuwa nchi kama Tanzania ni maskini na ilipaswa kutegemea misaada ya nchi za nje.
 
Na hiyo ndiyo ikawa staili ya viongozi wengi kuhalalisha safari za kwenda nchi za kigeni kusaka misaada `eti’ kwa kuwa nchi yetu ni maskini.
TRA imepata mafanikio haya baada ya serikali kubana eneo moja tu la bandari katika kuhakikisha watu wanalipa kodi kihalali. Mamlaka hiyo imevunja rekodi ya kukusanya mapato ya awamu ya nne, ambayo kiwango chake cha juu kilikuwa kati ya Sh. bilioni 800 na bilioni 900.
 
Tunaupongeza uongozi wa TRA na serikali katika kuhakikisha kuwa kiwango kikubwa cha mapato kinakusanywa.
 
Fedha hizo tayari zimeanza kutumika kupunguza makali ya maisha kwa Watanzania mathalani, zile zilizokusanywa  Novemba zimeelekezwa kusaidia utekelezaji wa ahadi ya Rais Dk. John Magufuli, ya kutoa elimu bure.
 
Katika kutekeleza mpango huo wa elimu bure, serikali ilitenga Sh. bilioni 131 ambazo zitatumika katika shule mbalimbali. Mpango huo wa kutoa elimu bure unahusisha kutoa vitabu na kugharimia chakula.
 
Tunaamini katika serikali na TRA wakiendeleza kasi hii ya kukusanya mapato, kuna uwezekano kabisa wa kuifanya nchi yetu kujitegemea. Waasisi wa taifa hili, Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere na hayati Abeid Karume, ndoto yao kubwa ilikuwa kuifanya nchi yetu ijitegemee.
 
Ndiyo Mwalimu Nyerere aliweka mkazo katika kilimo na ujenzi wa viwanda kwa kuamini vingechochea maendeleo na kuifanya nchi yetu kutotegemea misaada kutoka nje.
 
 
Hayati Karume naye alitumia zao la karafuu kuiendeleza Zanzibar na ndipo alipoanza mradi wa ujenzi wa nyumba kwa ajili ya watu wake na miundombinu.
Bahati mbaya katika miaka ya karibuni, viongozi wengi waliopewa dhamana ya kuongoza nchi yetu walijielekeza zaidi katika kujineemesha. Kwa sasa, si jambo la ajabu kusikia viongozi wakitumia mabilioni ya fedha kwa kisingizio cha kwenda kusaka fedha za misaada nchi za nje badala ya kuandaa mikakati ya kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kuondokana na aibu ya kuomba omba misaada nchi za nje.
 
Mathalani, serikali ikianza kubana mapato yanayokusanywa na halmashauri mbalimbali nchini ina maana mapato ya serikali yatapanda maradufu.
Bado hatujazungumzia kampuni mbalimbali ya uwekezaji, ambazo zimekuwa zikipewa misamaha ya kodi na mengine yanayolalamikiwa kama ya masuala ya gesi na madini.
 
Kwa mafanikio haya ya muda mfupi ya Serikali ya awamu ya tano, inadhihirisha kuwa umaskini wa Tanzania unachangiwa zaidi na mipango mibovu.
 
Tunaamini serikali ya awamu ya tano ikiendelea na kasi hii itafanikiwa katika kipindi kifupi kutimiza ndoto ya Mwalimu Nyerere ya Tanzania kujitegemea na kuachana na kuomba omba misaada.
 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom