Jumatano, Desemba 03, 2014

MWISHO WA SIMULIZI YA MAISHA USILIE NADIA SEHEMU YA 25



 ILIPOISHIA
“Gari ya mama ileee.” Tukiwa nje yule mtoto alinionyesha kwa kidole gari iliyokuwa inaingia pale shuleni. Akimaanisha ni ya mama yake, nikazidisha mwendo na kukata kona mbili tatu. Sikutaka kupoteza muda zaidi, nikafanya nilichopanga, nikampa yule mtoto pipi, akaidaka na kuitupia mdomoni, baada ya dakika ishirini nilikuwa nimetoa kanga na alikuwa mgongoni kwangu kama mwanangu wa kumzaa vile amelala hoi. Hatua ya kwanza ilikuwa imefanikiwa kwa kiasi kikubwa.USIKOSE MWISHO WA SIMULIZI HII

INAPOENDELEA 

Alipokuja kustuka alikuwa kitandani, nikamchukua na kumwogesha aliniuliza maswali nikamjibu vyema na kumtaka awe mtulivu kabisa.Alilala Musoma na sasa ameamka akiwa jijini Mwanza. Harakati zangu zilienda kwa usahihi sana.
Nia yangu ya kumnyanyasa Desmund na mkewe kimawazo ilikuwa inatimia sasa, nilijua watahangaika sana na mwisho watajiona hawana thamani yoyote katika maisha yao. 

Namba ya Desmund ilikuwa kichwani mwangu na bado sikutaka kuwasiliana naye. Cha muhimu zaidi nilitaka ateseke hadi nafsi yangu iridhike.” Nadia akakomea hapa, uchovu ulikuwa umemshika akaaga na kwenda chumbani mwake. Mimi nilipojilaza kidogo nikapitiwa na usingizi kwa sababu usiku kucha nililala kwa kujibana  sana katika kochi.
Nilikuwa naamini sasa mwisho wa simulizi unakaribia kwa sababu tayari Desmund alishaanza kuguswa pabaya.

Nikasubiri kwa hamu kabisa siku ambayo Nadia ataendelea kusimulia ili nijue aliishia wapi katika harakati zake hizo.
Nilikuja kushtuka mchana jua likiwa kali kabisa, nilitaka kwenda chumbani mwa Nadia lakini nikasita na kuamua kupiga simu ya chumbani mwake, iliita bila kupokelewa. Nikajua na yeye atakuwa katika dimbwi la usingizi mzito kabisa kama mimi nikapuuzia na kuendelea kulala.


Majira ya jioni nikapata cha kuingia chumbani mwa Nadia. Ni kumchukua twende kupata chakula na pia kujiandaa kwa safari ya kwenda jijini Dar es salaam kwa ajili ya kumtimizia ndoto zake za kuwa huru tena na mwenye furaha.

Nilifika nikakigonga chumba chake lakini hakujibu kitu, hii haikuwa kawaida ya Nadia hata kidogo, nikaamua kufungua, kitasa kikafunguka vizuri tu!! Kuingia chumbani hapakuwa na mtu. Lakini kitandani palikuwa na ujumbe mfupi.
“Nimetoka kidogo!!” ujumbe huu ulinishangaza, yawezekana vipi Nadia kutoka peke yake katika jiji hilo la Mwanza tangu nifike naye pale, hapa nikapata walakini. Nikajiuliza nichukue hatua gani lakini sikupata namna ya kufanya. Mara macho yangu yakakutana na rekoda yangu!! 

Nikaduwaa imefika vipi pale ndani, wasiwasi ukaniingia maana hadi ninaposinzia ilikuwa katika chumba changu.
Nikaichukua na kutazama, nikakuta kuna kitu kimeongezeka katika ile reekoda, mara ya mwisho nilikuwa nimerekoda kwa masaa nane, lakini sasa yalikuwa masaa tisa. Hivyo kuna jambo la ziada.

HAKIKA katika maisha unatakiwa kujifunza na kukubaliana na ukweli kuwa moyo wa mtu ni fumbo gumu kabisa, fumbo lisilofumbuliwa kirahisi. Kuna jambo Nadia alikuwa amelihifadhi katika moyo wake ambalo sikulijua na mbaya zaidi ulikuwa mpango wake wa siku nyingi.
Nikaiwasha ile rekoda kuanzia pale nilipoishia yaani saa moja nyuma.
Nikakutana na sauti ileile ya Nadia.
“Gerlad Iron! Mwandishi mpole, msikivu muelewa mnyeyekevu na mwenye huruma, natamani sana moyo wako ungeukata kidogo na kuwagawia akina Desmund maana wapo wengi duniani. Naamini unahitaji sana kunisaidia huku ukihitaji pia kujua kila kitu kuhusu mimi. Lakini sina maana hata ukinisaidia mimi.
Mara ya mwisho kuzungumza nawe nilichoka ghafla kwa sababu tu sipendi kabisa kukumbuka kilichokuja kutokea katika maisha yangu! Sitaki kukumbuka machungu na maasi yangu.
Ni kweli nilifanikiwa kumteka mtoto wa Desmund na kumuhifadhi jijini Mwanza, hiyo kwangu ilikuwa hatua kubwa Desmund alitetemeka kama mtoto mdogo na bado hakujua kama ni mimi nahusika, baada ya kumweka mtoto Mwanza nyumbani kwa dada yangu aliyekuwa akiishi na Jonas niliamua kurejea Musoma tenma kwenda kukabiliana na Desmund, hakika walikuwa wamefadhaika sana na duka lilifunguliwa na yule kijana wa kichaga, mkewe  Desmund hakugusa kabisa pale, nilipoonana na yule mchaga alinieleza kuwa kale katoto kamepotea katika njia za kishirikina, nilitabasamu huku nikiyasikitikia mawazo yao. Nikiwa Musoma nilikutana na kundi moja la wahuni likijiita WEST LAWAMA, nilizungumza nao vyema, hawa nikawaagiza kijijini kwao Desmund kule alipokuwa anaishi mama yake, huku nilihitaji jambo moja tu la kuiteketeza akili ya Desmund zaid, nilihitaji waichome ile nyumba. Hilo halikuwa na shida hata kidogo biashara ilienda vizuri sana, Desmund akazidi kupagawa. Bado nilienda mbele zaidi kutuliza kidonda changu moyoni, nikawaagiza wapeleleze ni wapi nyumbani kwa mke wa Desmund, upesi wakapapata, nikawalipa na huku wakateketeza, bahati mbaya kwake na bahati nzuri kwangu, wadogo zake mke wa Desmund wawili waliteketea katika moto. Sikuwa na huruma hata kidogo maana nimelaniwa, nisingeweza kukusimulia haya nikiwa nakutazama maana mimi ni zaidi ya shetani kwa malipo haya, malipo yaliyokuwa yakinifariji moyo wangu.
Baada ya hapo nikaenda nyumbani kwa Desmund mida ambayo nilijua kabisa kuwa hayuipo nyumbani, nikaacha ujumbe kwa mlinzi kuwa ‘AKIJA MWAMBIE MWENYE NYUMA ALIKUJA’, nadhani aliupata ujumbe ule na bado akaupuuzia ni hapo nikampa tena pigo jingine, pesa niliyokuwanayo zaidi ya kula na kulala haikuwa na kazi nyingine ile, hivyo nikaendelea kuitumia vilivyo. Mdogo wake Desmund wa kiume aliyekuwa akiishi naye akacharangwa mapanga vibaya sana lakini hawakumuua, nami nilitaka iwe hivyo. Wakamuachia ujumbe kuwa mwenye mali anataka mali zake. Ujumbe alioufikisha kwa kaka yake bila shaka.
Diwani akazidi kukonda, diwani akapagawa. Nikaifurahia hali hiyo.
Mwandishi, ujue sikupanga kabisa kumdhuru Desmund wala mkewe baada ya adhabu hiyo, badala yake nilitaka anipe mali zangu hata nusu nijiondokee kwenda ninapojua lakini si kumdhuru, nilikuwa nina tatizo la kuwa na huruma sana. Hiyo ilikuwa mbaya sana kwangu.
Lakini mawazo yalibadilika ghafla na kujikuta nikifanya kitu nisichokitarajia hata kidogo.
Siku hiyo niliamua kwenda nyumbani kwa Desmund siku niliyoamini kuwa alikuwepo nyumbani yeye na mkewe.  Niliingia hadi ndani baada ya mlinzi kuambniwa aniruhusu. Nikaingia katika nyumba ya Desmund na mkewe, walikuwa wameketi wakiwa wanatazama luninga lakini hawakuwa wameitilia maanani sana.
Desmund alishtuka sana kuniona nikiwa pale, alitaka kupiga mayowe lakini nikawahi kumwambia akae kimya.
“Maonyo yangu unayapata ama huyapati.” Nilimweleza na kisha kabla hajafanya lolote nikamuonya, “Ukithubutu kuleta ujuaji wako, nyumba hii itachomwa moto dakika hii na utafia humu ndani wewe na hiki kikaragosi chako.” Niliongea kwa ujasiri sana na wote walitetemeka.
“Nadia tafadhali nakuomba sema chochote nitakupa, lakini unipe mwanangu Nadia.” Alinisihi kwa sauti ya huruma sana.
“Mali zangu unanipa ama hunipi wakati huu, ama ndo hunijui tena mimi ni nani.’ Nilimuuliza bado nikiwa nimesimama.
“Nadia nakupa kila kitu utakachotaka.” Aliendelea kunisihi kwa huruma.
“Desmund naondoka muda huu nitarejea baada ya siku tatu, nahitaji nikute nyumba hii ipo mnadani, uiuze, vitu vya dukani uviuze, gari uliuze na bila shaka haitakuwa chini ya miloni miambili mezani. Nitaichukua hiyo na utampata mtoto wako, lakini vinginevyo, nitaanza na kile kiuchafu chako nitanyonga, halafu wewe na huyu mjinga mwenzio nita..” kabla sijamaliza kuongea yule mwanamke akaja kunikabili kwa jazba akilalamika eti nimemtusi sana. Pole yake hakujua mimi ni wa aina gani kwa wakati huo, alikutana na teke moja maridhawa akaangukia kwenye viti huko akatokwa na yowe la hofu, Desmund akamkanya asiniguse. Nikaondoka na kuahidi kurejea baada ya siku hizo tatu.

Niliondoka pale na kuchukua mabasi kwa safari ya Mwanza, kila abiria alikuwa akizungumzia habari ambayo nilikuwa siijui lakini nilipolikanyaga jiji ndipo nikaamini laana yangu inashambulia hadi watu wasiohusika.
Jiji la Mwanza lilikuwa limekumbwa na mafuriko, nyumba ziliezuliwqa na nyingine kusombwa na maji, hali ilikuwa mbaya. Sikuishughulisha akili yangu kuwaza juu ya familia yangu kwa wakati huo, yaani Jonas na Desmund Jr. lakini akili ilichanganyikiwa baada ya kukuta eneo alilokuwa akiishi yule dada na wale watoto nyumba zikiwa zimemezwa na maji. Nilifanikiwa kuonana na jamaa yake yule dada.
“Mvua imeondoka na dada yangu jamaniii…” aliugulia, nikakosa la kusema.
“Na vile vitoto masikini vimekufa vikiwa vimekumbatiana naye, jamani aah!! Dada weee!!” alianza kulia, nikaungana naye kwa uchungu mkubwa, nikiwa nimepagawa kabisa nakujiuliza kama ni kweli nayasikia maneno yale ama la!! Nilikuwa naota….hapakuwa na ndoto pale hali ilikuwa halisi kabisa. Nikaongozana na yule kijana hadi Bugando mochwari tukajieleza na kisha tukaonyeshwa maiti zile. Hakika alikuwa ni Jonas na yule mwingine alikuwa ni Desmund jr.
Mwandishi sikuwahi kushikwa na uchungu wa moja kwa moja moyoni namna ile katika misiba lakini msiba huu ulinichanganya na kujina mimi sina haki ya kuishi kabisa, nilijiona niliyelaaniwa na laana yangu inaishi nami. Nikaamua kurejea Musoma baada ya kuwazika watoto wale, nikamkabili Desmund, alikuwa ndani ya nyumba ileile lakini milioni mia mbili zilikuwepo mezani.
Nikahitaji kujua ni kipi chanzo zcha yeye kunitenda vile hadi kunisababishia laana.
Desmund alinisimulia mkasa juu ya baba  yake mzazi alivyodhulumiwa mali na mzee wa kiarabu, akaelezea juu ya mzee huyo kumuua baba yake mzazi mbele ya macho yake yeye akiwa bado mdogo, hali hiyo ikamfanya awe na chuki na ngozi hii, baada ya kuamua kuendelea na maisha akaajiliwa na mwarabu huku napo akajikuta anateswa sana huku akizidi kupoteza uelekeao wa maisha, hiyo haikuwa simulizi pekee bali akaenda mbali zaidi na kunieleza juu ya kifo cha dada yake ambaye aliolewa na mwarabu licha ya yeye kumzuia, dada akayavumilia mengi ya ndoa lakini siku ya kukata roho akamweleza Desmund kuwa yule mwarabu alikuwa anamlawiti mara kwa mara, hivyo anakufa kwa sababu alikuwa anatendwa vibaya. Nilijisikia vibaya kumwona Desmund akliwa analia kwa uchungu huku akiikumbatia picha ya dada yake lakini nilijikaza nisidondoshe machozi kwani ungekuwa udhaifu wa hali ya juu.
Desmund akakiri kuwa alivurugwa akili kabisa na ngozi hiyo na hata ndugu zake na marafiki wa karibu walijikuta wakiichukia ngozi ile. Naam!! Desmund akanichukia na mimi na kuamua kutulizia maumivu yake huku. Nilimwelewa Desmund na sikutaka kumweleza zaidi juu ya upendo wangu kwake katika kipindi hicho. Sasa alikuwa amechelewa sana kunitaka radhi, nikambana na maswali juu ya nani alimuua Danny yule askari, akajibaraguza lakini baadaye akakiri kuwa angeweza kumdhuru mtu yeyote ambaye angeweza kunitetea, hivyo Danny alikosea kunitetea. Desmund alimuua Danny. Hasira zikanichemka nilipokikumbuka kifo cha Danny mtetezi wangu.
Hapa sasa nikaamua kufanya nililotaka kufanya, nikamkabili Desmund aliyekonda klidhaifu kabisa nikachomoa kisu changu na kukisukumiza katika mbavu zake, aliga kelele nikawa kumziba mdomo. Niliona mwanaume huyu hakufaa kuishi hata kidogo na sikutaka kuwa na udhaifu kama ule wa Jesca wa kumchekea adui. Aliyefuata baada ya pale ni mkewe, huyu alipoingia ndani tu nikamkaba, hata sikutumia kisu, nilimnyonga hadi akapoteza uhai. Nafsi yangu ikapata ahueni. Wataishi vipi watu hawa wabaya wakati kitoto kisichojua lolote kimekufa huko Mwanza kwa makosa ya wazazi wao.
Nikaunganisha safari yangu moja kwa moja hadi nyumbani kwa Mzee Matata, nikamuulizia hakuwa anapatikana tena hapo, lakini si hapo tu hata ulimwenguni hakuwa anapatikana, mzee Matata alikuwa marehemu, alikufa kwa kupigwa risasi. Waliompiga hawakujulikana.
Wamenisaidia hao!! Nilijisemea na kujiaminisha kuwa ni mzee huyu aliyeniteka na kunitupa katika dimbwi la kuwa msafirishaji wa madawa ya kulevya .
Nilipomaliza hapo, nilikuwa nimechakaa nafsi na sikujua kabisa kama nilikuwa nina chochote cha kufanya duniani, milioni mia mbili hazikuwa na maana yoyote kwangu nikaziacha nyumbani kwa Desmund.
Nikaondoka kwa nia moja tu ya kujiua, na hapo ndipo nikakutana nawe kichakani usiku ule mkiwa mmeharibikiwa damu, ukanisihi sana hadi nikaamua kufuatana nanyi, hakika unayo lugha ya ushawishi sana, uliweza kunibadili mawazo yangu, umeweza kunifanya mtu mwingine tena na kujikuta natabasamu mara kwa mara. Uliponichukua sikuamini kama nitakuamini hata kidogo, lakini umekuwa wa pekee sana kwangu, lakini kitu kimoja tu, sihitaji twende wote Dar es salaam mimi nina mikosi sitaki kukuambukiza mikosi yangu, sitaki maafa yaliyolikumba jiji la Mwanza yahamie pia Dar es salaam, hii yatosha.
Wewe ni mshauri mzuri sana tena mwenye ushawishi sasa nahofia kuwa katika maamuzi haya ningekushirikisha lazima ungeyabadili mawazo yangu tu hiyo lazima ingetokea.
Ni kweli labda kuna maswali yako mengi sijayajibu, hii yote labda ni kwa sababu ya uchovu wa akili na msongo wa mawazo vilevile, kama utabaki na maswali naamini hautapata nafasi ya kuyasikia nikiyajibu, si kwamba hatutaonana tena ama labda niseme si kwamba hautaniona tena bali utaniona lakini hakika sitakuwa tayari kusema lolote lile. Najua wewe ni bingwa wa kusihi na kubembeleza lakini sitabembelezeka katika hilo niliyokueleza yanatosha sana, yasambaze katika dunia, mimi Nadia nimekubali kuwa mfano kwa wasichana na wanadamu wenzangu usiogope kusema ukweli kama nililawitiwa, usifiche juu ya shughuli za usafirishaji madawa kuwa muwazi kama nilivyokuwa muwazi kwako. Gerlad Iron baki na sauti hii milele, iishi sauti hii kizazi hadi kizazi, tone la chozi langu wasimulie wahangaikaji wa dunia, kwikwi yangu iwe funzo kwao na amani ya bwana iwe nawe G katika lolote lile utakalofanya na limpendeze Mungu!!! Uwe na amani. Tutaonana inshalah!!”
Sauti ya Nadia ilimaliza na ule ukawa mwisho wa kurekodi, nilivaa viatu vyangu upesi upesi huku nikiamini kuwa natakiwa kwenda mahali lakini ni wapi ningeenda, nikawa mnyonge na kukaa chini tena. Nikajipa moyo kuwa huenda Nadia atarudi jioni. Hadi kufikia saa kumi na mbili bado mambo yalikuwa yaleyale. Lakini saa moja Nadia alirejea!!
Hakika alirejea chumbani lakini katika namna ambayo alikuwa ameahidi, hakuwa Nadia ninayeweza kumshika na kumliwaza bali alikuwa Nadia katika luninga akiwa ametulia tuli waandishi wa habari wakimpiga picha.
Nadia alikuwa amejinyonga!!!
Niliishiwa nguvu nikabaki kukodoa macho tu..mwandishi yule aliyeisoma habari hiyo kwa majonzi alipiga nyundo ya mwisho kwa kusema kuwa, marehemu aliacha ujumbe mfupi sana wenye majina mawili.
“Nadia Gerlad”, hapo nikazidi kusisimka na kupagawa zaidi. Lakini sikuwa na ujanja kifo hakina mbadala, alikufa na inabaki hivyo kuwa alikufa.
Kumbe Nadia alipanga kujiua!! Nilijiuliza lakini nani angenijibu!! Hakuna wa kunijibu!!
Nikapitiwa na usingizi, kesho yake nikaamkia kituo cha polisi kutoa taarifa kuwa Nadia ni dada yangu!! Wakanielewa na nikapewa ruhusa ya kuuchukua mwili.
Nilifanikiwa kuuchukua na kufuata hatua zote, Nadia akasafirishwa kuelekea jijini Dar es salaam, familia yangu ambayo ilikuwa na taarifa tayari iliupokea mwili wa Nadia, kisha mimi nilifika siku moja baadaye. Nadia akazikwa kwa heshima zote kama ndugu katika familia yetu.
Kampuni iliyoniajiri ilijumuika nasi katika msiba huu huku kila mmoja akingojea kusikia ni kitu gani nilivuna kwa miezi yote hiyo tangu nikutane na Nadia.
Baada ya siku arobaini, niliibuka hadharani nikiwa na kila kitu kuhusiana na Nadia, sauti na baadhi ya picha.
Kila mwenye moyo wa nyama aliposikia juu ya Nadia alitokwa na machozi. Wengi walijifunza kutokana na simulizi ya Nadia
Kuna kipindi nilikuwa najiuliza hivi ni kweli nilikutana na Nadia, na hapo nikajikuta naisikiliza sauti yake tena na tena huku nikizitazama picha zake nilizowahi kumpiga.
Mwisho nikaibuka na kitabu kikubwa cha simulizi nilichokipa jina la USILIE NADIA…kitabu kilichokuwa maalumu kwa msichana aliyesota ulimwenguni kupigania haki yake na mwisho akatoweka akiwa amelipiza kisasi!!!
NADIA BARGHASH!!! Aliyeishi pia kwa jina la MARIAM  na baadaye MAMA JONAS huku akiamua kufa kwa jina la NADIA GERLAD!!!!
  
MWISHOOO!!! 
WADAU MAONI YENU NI MUHIMU SANA ILI TUWEZE KUBORESHA UWANJA HUU




Maoni 3 :

Saki alisema ...

Kazi nzuri sana, simulizi ni tamu sana. ni vizuri ungetoa kitabu ili kila mtu asome inafundisha sana. Asante sana mwandishi

emu-three alisema ...

Mhh Nadia,...kwanza nikushukuru kwa kutupa simulizi hili na mwengine, kwani muda na kufikiri ni gharama, pili nikupo hongera, kwani pamoja na hayo umeweza KUCHAPA vitabu kitu ambacho wengine bado kinatupa shida, narudia tena kusema HONGERA MPENDWA, na TUPO PAMOJA

mamlious alisema ...

hongera della kwa story nzr, inahuzunisha sana, kama unaweza tafuta wasanii wakubwa wa hapa tz watengenezee filam ya ii stor yako mana ina mafundisho mazuri,
asante sana, tupe na nyngne ila zisiwe za kichawi bana

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom