Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo SIMULIZI ZA KUSISIMUA. Onyesha machapisho yote
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo SIMULIZI ZA KUSISIMUA. Onyesha machapisho yote

Alhamisi, Januari 17, 2013

MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA ........11........

 
ILIPOISHIA“Jamani za siku nyingi.” Aliendelea kumsemesha Julieth. Mwanzo Julieth hakumtambua lakini alivyozidi kumwangalia akamkumbuka.
“Oh! Kumbe Zubeda! Mambo vipi rafiki yangu? Nimefurahi sana kukuona habari za hapa?” Zubeda alikuwa ni rafiki yake Julieth, kwani walikuwa wakiuza chapati pamoja wakati Julieth akiwa Arusha. Domina alianza kulia, haraka Zubeda alimchukua Dominiki ili Julieth amnyonyeshe Domina. USIKOSE SURA YA 11
 
INAPOENDELEA 
“Habari za hapa ni nzuri kiasi.” Aliongea Zubeda huku akimshika vizuri mtoto.
“Nzuri kiasi!” Alihamaki Julieth huku akimkazia macho Zubeda.
“Ndiyo! Nzuri kidogo.” Alisisitiza Zubeda huku akiyakwepa macho ya Julieth.
 “Vipi mwenzangu mbona ulikuwa kimya sana? Wakati mama yako akiwa anaumwa tulikupigia simu mara nyingi lakini haikupatikana na …”
“Ehe! Sasa anaendeleaje?” Julieth alimkatisha Zubeda na kuuliza akiwa katika hali ya kushtuka.

 Zubeda aliwachukua watoto wa Julieth na kukaa nao pembeni wakati yule dereva akiondoka. Julieth alitaka kuingia ndani moja kwa moja lakini Zubeda alimzuia.
 “Julieth wadogo zako na mama yako hawapo hapa.” Zubeda alianza kueleza.
Kama nilivyokudokeza mama yako aliugua sana, tulikutafuta kwenye simu yako ili utume fedha za matibabu bila mafanikio. Kwa vile mama yako alikuwa hana pesa ikabidi auze simu yake ili apate pesa za matibabu.”
“Oh! Samahani sana. Simu yangu iliharibika nikawa na simu nyingine. Lakini namba ya mama ninayo, ila nilishawahi kumpigia lakini haikupatika.  Labda ndo kipindi alipoiuza. Aliongea Julieth kwa masikitiko.”

Jumatatu, Januari 07, 2013

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA .....10......

 
 
ILIPOISHIA “Wewe! Wewe! John! Muogope Mungu ulinichukua kwetu Arusha na kunidanganya kuwa unanipenda leo hii unaniona sifai. Eti kichaa! Baada ya kunidanganya na kuniharibia maisha yangu leo unaniona kichaa. Ungeniambia ukweli haya yote yasingetokea, kumbe ulikuwa una mke na mtoto. Sawa! mimi nitaondoka ila Mungu ndiye atakayenisaidia nakutakia maisha mema.” Alifoka Julieth kwa mfululizo bila hata kumpa John fursa ya kujibu huku akibubujika machozi.USIKOSE SURA YA ...10......
 
 
INAPOENDELEA 
Wakati akizungumza maneno hayo mama Philipo alibaki kimya akitafakari kisha akaungana na John kumshambulia Julieth; “Hebu tuondolee kilio hapa ufanye uhuni wako upate mimba halafu uje hapa na vitoto vyako nani akupokee, kamtafute baba wa watoto wako. Unataka kunigombanisha na mume wangu toka mjinga wewe.” Alitamka mama Philipo huku akimsukumiza Julieth na watoto wake nje. Julieth alitoka akiwa analia sana.

Julieth alirudi kwa mama Janeth na kumwelezea yote aliyokutana nayo. Mama Janeth alisikitika sana na hakuwa na namna nyingine ya kumsaidia zaidi ya kumpa nauli na pesa kidogo za matumizi ili arudi kwao Arusha; “Julieth wewe nenda tu nyumbani ukamweleze mama yako hali halisi kwani ukiendelea kuishi hapa utateseka sana na ipo siku huyo John atakutafuta. Nakutakia kila la heri Mungu atakusaidia utawalea watoto wako vizuri.” Mama Janeth alishauri.

 “Nashukuru sana mama Janeth kwa msaada wako, tangu siku nilipoumwa uchungu hadi sasa. Umekuwa msaada mkubwa sana kwangu. Mimi nitakwenda nyumbani na hata huko nyumbani sijui wanaendeleaje kwani sijawasiliana nao kwa muda mrefu. Kuna siku nilimpigia mama simu ikawa haipatikani sijui wana hali gani.” Mama Janeth akampa simu ajaribu kumpigia tena mama yake lakini haikupatikana. Julieth  aliwaza  moyoni mwake; “Jamani mama atakuwa ana matatizo gain? Labda simu itakuwa imepotea au imeharibika.”

Jumatano, Januari 02, 2013

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA ......9.... NAWATAKIA HERI YA MWAKA MPYA NA MUENDELEE KUPATA UHONDO WA SIMULIZI


Ilipoishia: Alipofika alikuwa na wasiwasi mkubwa akifikiria jinsi atakavyokabiliana na uso wa John baada ya kuachana kwa takribani miezi mitatu. Alisogea jirani, akagonga taratibu na kusubiri afunguliwe. Mara mlango ulifungulwa na mwanamke mwenye uso wa kujiamini kisha akaanza kumsemesha Julieth: “Habari za leo dada! Alisalimia. “Salama dada yangu! Habari za hapa?” Alijibu na kuuliza Julieth. “Karibu dada nikusaidie nini?” Aliuliza bila hata kujibu swali aliloulizwa.Julieth alishtuka sana na kuingiwa na hofu kubwa kumwona yule mwanamke aliyefungua mlango. USIKOSE SURA YA 9...........

INAPOENDELEA
“Samahani namuulizia John.” Yule mwanamke alimwangalia Julieth kuanzia kichwani hadi kwenye vidole vya miguu, kisha akamkaribisha: “Karibu ndani.” Alimkaribisha Julieth huku akitangulia ndani haraka bila hata kuangalia nyuma. Julieth aliingia na kukaa katika sofa lililokuwa jirani kabisa na mlango huku moyoni mwake akijiuliza: “Huyu mwanamke ni nani?” Wakati huo yule mwanamke alikuwa amekaa katika sofa lililokuwa karibu na mlango wa kuingia chumbani, huku mtoto wa kiume mwenye umri kati ya miaka mitano na sita hivi akichezea kijigari kidogo.


Kwa takribani dakika tatu au nne hivi walibaki kimya huku kila mmoja akimwangalia mwenzie kwa kuibia. Ghafla yule mwanamke alivunja ukimya kwa kutaka kujua Julieth alikuwa na shida gani; “Samahani dada unamtaka John wa nini?” Aliuliza yule mwanamke. Julieth alitaka kumjibu lakini alisita. Baada ya dakika moja hivi Julieth alijipa ujasiri mkubwa na kumweleza kilichomleta pale ndani, wakati huo John alikuwa yupo chumbani asiyejua chochote juu ya nini kinachoendelea pale sebuleni:

Alhamisi, Desemba 13, 2012

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SEHEMU YA .........8..........



ILIPOISHIA
Baada ya siku kadhaa kupita hakukuwa na mabadiliko yoyote ila matatizo yalizidi kila siku ilikuwa ni ugomvi. Miezi kadhaa ilipita bila Julieth kuwa na mawasiliano na wazazi wake kwani alikuwa hana simu, hivyo ilikuwa vigumu kujua hata wazazi wake walikuwa wanaendeleaje. Kwa kweli maisha yalikuwa magumu sana. Wakati huo mimba ilikuwa na umri wamiezi saba lakini John alikuwa hajali. 

INAPOENDELEA

Siku moja John alimwambia Julieth kwamba siku zake za kuondoka zinahesabika. Ilikuwa ni yapata kama saa mbili usiku wakati Julieth akiandaa chakula cha jioni. John alifika na kumwita Julieth. “We mwehu si ulikuwa unataka uende nyumbani kwenu sasa muda wako umefika unaweza ukaondoka muda wowote nakupa wiki mbili tu.” Aliongea John kwa maneno ya kutukana. “Lakini si ulisema tutakwenda wote? Hebu niangalie na hali hii kweli ndiyo niende nyumbani mwenyewe. Afadhali nisubiri hadi nijifungue ndiyo niende nyumbani.

 “Wewe una kichaa nini hivi hapa ni kwako? Tena sikiliza kwa makini nataka uondoke uende popote unapopajua hata ukifa shauri yako. Kwanza hata hiyo mimba si yangu. Kwa hadhi yangu siwezi kuwa na mke kama wewe. Kwa taarifa yako mimi nina mke na mtoto na siku si nyingi anarudi sitaki aje akutane na kinyago kama wewe humu ndani.” John alitukana na kuongea kwa kebehi na dharau. Akiwa amejiinamia Julieth alisikiliza yale maneno na kuhisi kama ni ndoto.

Kabla hajazungumza lolote John aliondoka na kumwacha akiwa na mawazo sana na kushindwa kuelewa mwenziwe ana matatizo gani. Baada ya wiki moja kupita tokea John alalame na kutukana wakati Julieth akiwa amekaa sebuleni mara John aliingia na kupita pale sebuleni kama hajamwona kisha aliingia ndani na kurudi na mabegi ya nguo na kumtupia huku akimfukuza Julieth aondoke na kwenda kwao.

“Kuanzia muda huu ninavyoongea sitaki kukuona katika nyumba yangu tena. Kama kuna kitu nimesahau kukitoa ukakitoe sasa hivi sitaki kukuona hapa mke wangu karibu atarudi.” Aliongea John kama mtu aliyepagawa. “Jamani mimi nitakwenda wapi na hii mimba? John uliniambia unanipenda kweli leo unanifanyia hivi? Nakuomba kama nimekukosea unisamehe unajua hali halisi ya maisha yangu nitafanyaje mimi kama unanifukuza? Je, maisha yangu yatakuwaje? Aliuliza Julieth kwa uchungu huku machozi yakimtoka kama mtoto mdogo.

Jumanne, Desemba 11, 2012

SIMULIZI YA MAMA MDOGO SURA YA .....18.......





ILIPOISHIA
Akasogea karibu na baba yake akapiga magoti mbele yake huku machozi yakimtoka. “Baba nimekukosea sana! Nimetenda dhambi kubwa mbele za Mungu pia. Nisipotubu dhambi hii sitapona nitateseka maisha yangu yote…”
Jamal aliongea kwa huruma na huzuni kubwa. Baba yake alimsikiliza Jamal kwa makini na huku mama yake mdogo akimwangalia na kuwaza moyoni mwake ni nini anataka kusema Jamal. Aliingiwa na hofu kubwa sana. JE NINI KINAENDELEA USIKOSE SURA YA .......18..........

INAPOENDELEA:
“Baba unakumbuka wakati ule mama mdogo alipokupa ule ujumbe ambao ulionyesha kuwa nimeandikiwa na msichana anaitwa Mary na ukanichukia sana hadi ukakataa kunipeleka shule.” Alieleza Jamal. “Ndio nakumbuka Jamal lakini nilishakusamehe mwanangu.” Alijibu baba Jamal. “Baba haikuwa kweli zilikuwa ni njama za mama mdogo kwani alikuwa akinitaka kimapenzi nilipokataa ndipo akanitafutia sababu nyingi ili unichukie.” Aliongea Jamal huku akimwangali mama yake mdogo.

“Hivi wewe Jamal una kichaa au! Unasema nini?” Alihamaki na kufoka mama mdogo huku akisimama kumfuata Jamal kwa hasira. Baba Jamal alimtaka anyamaze ili Jamal aendelee kuzungumza. Jamal alisimulia matukio yote yaliyotokea kuanzia mwanzo hadi mwisho. “Naomba unisamehe baba haikuwa kusudio langu. Kibaya zaidi baba…” Jamal alishindwa kuendelea baada ya mama yake mdogo kumkonyezakuashiria asiseme.
“Eleza yote mwanangu. Eh! Kibaya zaidi nini?” Aliuliza baba yake. “Kibaya zaidi hata huyu mtoto Rama si…” Mama mdogo alimziba mdomo Jamal.

Jumamosi, Desemba 01, 2012

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA .....7.......

MTUNZI ADELA DALLY KAVISHE
Baada ya mapenzi na raha kushamiri, Julieth alipata ujauzito ambao hakugundua kama ana mimba. Aligundua baada ya kwenda hospitali kupima afya yake kutokana na kutojisikia vizuri ikiwa ni pamoja na kusikia kichefuchefu. Suala la mimba lilimfurahisha sana Julieth. “Huu ndio wakati mwafaka wa kufunga ndoa, najua John atafurahi sana nikimzalia mtoto. Akija leo nitamwambia tufanye haraka tufunge ndoa.” Aliwaza Julieth. USIKOSE SURA YA ......7.........


INAPOENDELEA
Ilipofika jioni aliandaa chakula cha usiku mapema huku akiwa anamsubiri mpenzi wake arudi ampe taarifa kuhusu mimba aliyonayo. John alirudi na kumkuta Julieth anafuraha sana. “Kulikoni leo mpenzi mbona unaonekana una furaha sana kuna nini?” Aliuliza John. “Mpenzi leo nimetoka hospitali kupima nina ujauzito wako na sasa nadhani utakuwa muda mwafaka tufanye haraka tufunge ndoa.” Aliongea Julieth huku akitabasamu na kujichekeshachekesha.

”Ni vizuri Julieth lakini kwanza ukisha jifungua ndio tutafunga ndoa.” Alijibu John akionyesha kutofurahishwa na taarifa ya Julieth kuhusu ujauzito. “Jamani John ni muda mrefu tumekuwa pamoja kwa nini isiwe mapema kabla sijajifungua?.” Alisisitiza Julieth huku akimsogelea na kuweka mikono yake mabegani kwa John. “Sikiliza Julieth nikwambie; ndoa ina mipango mingi sana kwa hiyo wewe nisikilize mimi.” Alisema John huku akiwa anainuka na kuelekea chumbani.

John alikuwa kama mtu ambaye hajafurahia habari alizopewa na Julieth, basi Julieth alinyamaza kimya lakini aliendelea kufikiri na kutafakari hali aliyoonyesha John baada ya kupewa taarifa ya ujauzito. “Mbona John amebadilika ghafla kuna nini? Ngoja nimwache nitamwambia kesho vizuri.” Aliwaza Julieth huku akimfuata John .Kesho yake asubuhi kama kawaida waliamka mapema sana, Julieth aliandaa chai. Walipokuwa wanakunywa Julieth alimwambia John kuwa angependa kwenda Arusha kuwaona mama na wadogo zake kwani ilikuwa ni muda mrefu.

Alhamisi, Novemba 29, 2012

SIMULIZI YA MAMA MDOGO ........SURA YA ...17.......


MTUNZI ADELA DALLY KAVISHE
Baada ya muda mfupi baba yake akiwa ameongozana na mama yake mdogo walifika pale hospitali na kuingia ndani katika chumba alichokuwepo Jamal. Baba yake alipomwona katika hali ile roho ya imani ilimjia. “Masikini kijana wangu ndiyo amekuwa hivi siwezi kuamini dokta naomba umsaidie apone.” Baba Jamal alimwambia daktari. Wakati huo mama yake mdogo machozi yalikuwa yakimtoka kwa uchungu. “Daktari fanya lolote na kwa gharama yoyote Jamal apone.” Alisisitiza  mama mdogo.

INAPOENDELEA “Hakuna shaka kijana atapona wala msijali tatizo lake ni dogo sana. Vipimo vinaonyesha Jamal ana matatizo mawili. Moja anatatizo la kisaikolojia na la pili ni utumiaji wa dawa za kulevya. Matatizo haya yote yanatibika bila wasiwasi. Ila naomba ushirikiano.”Alieleza daktari. “Sawa daktari!” Waliitikia kwa pamoja Baba Jamal na mama mdogo. “Naona mnaitikia tu, je mmeelewa maana ya ushirikiano?” Aliuliza daktari. Baba Jamal na mama mdogo walitazamana kwa sekundi kadhaa, kisha baba Jamal alijibu kuwa inaeleweka na kumwomba daktari aendelee kumtibu Jamal wamejiandaa barabara.

Jamal aliendelea kutibiwa na alipozinduka na kujikuta yupo hospitalini alitaka kutoroka lakini madaktari walimshika kwa nguvu na kumfunga kamba. Jamal alilia sana pale kitandani na kuomba wamfungue. Baba yake alifika na kumsogelea huku akimshika usoni. “Mwanangu una matatizo gani? Nakuomba utulie upate matibabu.” Baba Jamal alimsihi Jamal. Jamal kumwona tu baba yake akasema kwa uchungu.

“Baba nisamehe! Baba naomba unisamehe! Nimekukosea sana baba!” Alilia Jamal na kupiga kelele. “Nimeshakusamehe mwanangu wewe tulia kwanza upone halafu twende nyumbani nakupenda sana mwanangu.” Alijibu baba Jamal. Daktari alifika na kumchoma Jamal sindano ya usingizi akalala. Siku ya pili Jamal alikuwa amepata nafuu kidogo ingawa bado alikuwa anashtuka na kuongea mambo yasiyoeleweka. Baba yake na mama mdogo walifika kumwona na kufurahi sana kusikia maendeleo mazuri ya afya ya Jamal. Baada ya wiki moja Jamal alikuwa ametulia. Siku moja baba yake alipokwenda hospitali Jamal alimwomba baba yake kuwa ana maongezi naye ya faragha kwani kulikuwa na mambo anataka kumwambia.

Jumapili, Novemba 25, 2012

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA .....6.......



ILIPOISHIA“Mimi mama nipo tayari kuolewa naye kwani kwa kipindi cha wiki tatu tangu nimfahamu ameonyesha moyo wa kutusaidia.” Alijibu Julieth huku akimwangalia John kwa macho ya kusisitiza.

“Sawa! Kwa sababu yeye ameridhia hata nikimkatalia ni kazi bure. Ila nawaomba mfuate taratibu zote za kimila na kufunga ndoa rasmi ili mpate baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwa wazazi pia.” Alishauri mama Julieth. USIKOSE SURA YA ......5........


INAPOENDELEA
“Huo ni ushauri mzuri mama, lakini namwomba niende naye Mwanza nikamtambulishe kwa wazazi wangu halafu atarudi ili tufanye taratibu hizo kama ulivyoshauri.” Aliomba John. “Kumbe kwenu ni Mwanza?” Aliuliza Mama Julieth. “Ndiyo mama.” Alijibu John. “Na je maisha yenu yatakuwa wapi?” Aliuliza mama Julieth. “Baada ya taratibu zote za kufunga ndoa kukamilika tutakwenda kuisha Mwanza.” Alijibu John. “Sasa baba kama mtaishi mbali na mimi nani atanihudumia, maana Julieth ndiyo alikuwa akinisaidia. 

Mimi mwenyewe hali yangu si nzuri sana naumwa mara kwa mara na Julieth anajua.” Alihoji mama Julieth. “Hapana mama usijali mimi na mwenzangu tumekwisha jipanga namna ya kukusaidia. Kwanza nataka uondoke hapa uhamie kwenye nyumba nzuri nitakayokupangishia. Pia nitakuachia pesa ili uweke msichana wa kazi ambaye atakusaidia kazi mbalimbali. Kuhusu pesa isiwe tatizo kabisa mambo yote yatakaa sawa.” John aliongea na kuahidi kwa kujiamini huku akimwangalia Julieth ambaye alikuwa akitabasamu muda wote wa maongezi.

“Sawa mimi nashukuru kama mmejipanga hivyo. Mungu akubariki sana mimi sina kipingamizi tena alimradi mmependana na kufuata taratibu za kufunga ndoa ili mpate baraka za Mungu. Pia ninaomba mkishaanza maisha muwe mnakuja huku kutusalimia mara kwa mara.” Mama Julieth alishauri huku akimkazia macho Julieth na baadaye John. “Hilo halina tatizo kabisa mama hapa ni nyumbani tutakuja bila shaka kwani nyumbani ni nyumbani, hata hivyo kwa sasa akishawaona wazazi wangu tu atarudi ili kukamilisha mambo ya ndoa kama ulivyoshauri.” Alijibu John.

********************************************************************
Mikakati ya kuondoka ikaanza, mama Julieth akahamishwa kutoka nyumba waliyokuwa wanakaa na kuhamia katika nyumba kubwa ambayo ilikuwa na kila kitu ndani. Kisha alitafutwa msichana kwa ajili ya kazi za ndani. Halafu nje ya nyumba alimfungulia duka dogo ambalo mama Julieth alikuwa akiuza bidhaa ndogondogo kama sabuni, sukari, unga na vinginevyo. Mwisho John alimnunulia mama Julieth simu kwa ajili ya mawasiliano ili kukitokea tatizo lolote atoe taarifa mapema. Mama Julieth alifurahi sana.

Jumatano, Novemba 21, 2012

SIMULIZI YA MAMA MDOGO SURA YA .........16.........




ILIPOISHIA:“He! we Jamal una kichaa nini? Yaani unataka kumwambia nini baba yako? Sasa naona unataka kuuwasha moto ambao kuuzima hutaweza. Ehe! na ukisha mwambia unatarajia nini?” Aliongea mama mdogo kwa kufoka. “Natarajia vyovyote itakavyokuwa, liwalo na liwe.” Alijibu Jamal. Mama yake mdogo alishindwa kuelewa Jamal amepatwa na maswaibu gani akasema.


INAPOENDELEA:“Kwani kuna nini kilichokufanya ukafikia uamuzi huo mpenzi wangu?” Alihoji mama mdogo. “Sikiliza kwa makini sana. Mimi siwezi kuendelea kuwa mjinga kiasi hiki. Haya mambo lazima niyaweke wazi. Nitaishi kwa wasiwasi hadi lini?” Aliongea Jamal kwa uchungu na kuondoka. “Hivi Jamal anataka kuwa kichaa au? Yaani amwambie Mzee Said kuwa mimi na yeye ni wapenzi na tumezaa mtoto? Sidhani kama atakuwa mzima hili ni tatizo.” Aliwaza mama mdogo. Siku zilivyozidi kwenda Jamal alikuwa akiota ndoto za kutisha sana. 

Mara nyingi alikuwa akimwona mama yake akimwambia aseme ukweli wa mambo yote yaliyotokea. Aliishi kwa shida sana, kwani hata usingizi alikuwa hapati. Hatimaye alianza kuwa mlevi ili asahau ndoto anazoota hivyo alianza kunywa pombe sana na kutumia dawa za kulevya kama bangi kwa nia ya kupoteza mawazo. Kumbe ndiyo alikuwa akizidi kuharibikiwa.

Baada ya kuwa mtumiaji wa vilevi alianza kufeli sana katika masomo yake ya chuo na baadaye akiwa mwaka wa tatu aliacha chuo na kuanza kuzurula mitaani. Kutokana na hali yake ya kutumia dawa kukithiri, baba yake alihuzunika na kuchukia sana baada ya kupata taarifa ya matatizo aliyopata mtoto wake. Huko nyumbani mama yake mdogo alikuwa na mawazo sana kwani alikuwa anatamani sana kumwona Jamal na hasa alipopata taarifa za kuwa anavuta bangi.

Jumatatu, Novemba 19, 2012

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA ......4.......



MTUNZI ADELA DALLY KAVISHE
ILIPOISHIA “Mmh jamani huna hela ndogo kaka au kuna kitu kingine unataka kununua dukani nikakuchukulie, asubuhi hii chenchi zinasumbua kweli.” Alisema Julieth kwa kulalamika. “Usijali Julieth nipe hizo chapati na fedha inayobaki ni zawadi yako.” Alijibu John. “Mh we kaka, hela yote hii nibaki nayo kuna usalama kweli? Hapana kaka ngoja nikutafutie tu chenchi.” Alisema Julieth huku akinyanyuka kwenda dukani. USIKOSE SURA YA .....4.....

INAPOENDELEA
“Julieth usiogope mimi sina nia mbaya na wewe chukua tu hiyo hela itakusaidia usijali.” Alitamka John huku akimzuia kuondoka. Julieth aliamua kukaa chini na kumsikiliza John hatimaye wakafahamiana. John alikuwa ni mkazi wa Mwanza na alikuwa ni mfanyabiashara wa samaki. Julieth alimweleza hali halisi ya maisha yao. Baada ya kufahamiana kwa siku kadhaa walianza kuwa marafiki na baadaye John alimtaka Julieth awe mpenzi wake. Mwanzoni Julieth alikataa sana kuhusu urafiki wa kimapenzi na John. 

Lakini baadaye alikubali wakawa marafiki. siku moja Julieth akiwa amekaa nje ya nyumba yao John alipita pale na kufanya maongezi na Julieth. “Julieth tumekuwa marafiki kwa muda wa wiki tatu sasa naona nikwambie ukweli. Kutoka siku ya kwanza nilipokuona nilitamani sana uwe mpenzi wangu. Naomba unipe nafasi ndani ya moyo wako. Nakupenda Julieth zaidi ya urafiki tulionao.” John alimwambia Julieth.

“Haiwezekani John! Mimi ni masikini sana unaiona familia yetu inanitegemea sana mimi, halafu nianze tena mapenzi! Hapana! Tena sitaki! Wewe tafuta tu mwanamke atakayekufaa anayeendana na wewe.” Alikataa Julieth kwa msisitizo mkubwa. “Sikiliza nikwambie Julieth, mimi na wewe tukiwa pamoja hata familia
yako itakuwa yangu pia, tutasaidiana sana katika maisha. Mama yako atakuwa hana matatizo tena. 

Alhamisi, Novemba 15, 2012

SIMULIZI YA MAMA MDOGO SURA YA .......15.....




ILIPOISHIA
Maisha yaliendelea kuwa mazuri na baba Jamal hakuwahi kugundua chochote kinachoendelea kati ya mkewe na mwanawe Jamal. Hatimaye muda wa kujifungua kwa mama mdogo uliwadia, alijifungua mtoto wa kiume na kumpa jina la Rama. Wakati huo Jamal alikuwa akimaliza Kidato cha Sita na alimpenda sana mtoto wa mama yake mdogo. Alipokuwa nyumbani alitumia muda mwingi kucheza na yule mtoto kiasi kwamba hata mama yake mdogo alifurahi sana.USIKOSE SURA YA ........15..........

INAPOENDELEA

Hatimaye Jamal alimaliza Kidato cha Sita na matokeo yalipotoka alikuwa amefaulu vizuri sana. Baba yake na mama mdogo wote walifurahi sana na matokeo mazuri ya kijana wao kisha walimtaka aendeleze juhudi zaidi katika masomo ya chuo. Jamal Alijaza fomu za kujiunga na Chuo Kikuuu cha Dar es Salaam. Aisha alikuwa amemaliza Darasa la Saba na sasa alikuwa akisoma Kidato cha Kwanza katika Shule ya Sekondari ya Jangwani.

Jamal aliamua kwenda kuishi hosteli za mabibo. Lakini alikuwa akija nyumbani mara kwa mara hasa siku za Jumamosi na Jumapili. Uhusiano wa kimapenzi na mama yake mdogo uliendelea kila walipokutana. Jamal alishazoea kabisa kuwa na mama yake mdogo na hata baba yake alipoona jinsi Jamal alivyo karibu na mama yake mdogo alikuwa akifurahi sana bila kujua nini kimewaweka karibu.

********Baada ya miezi mitatu********

Siku moja Jamal alipomaliza tu kufanya mtihani wa moja ya masomo anayosoma alikwenda moja kwa moja chumbani kwake hosteli za mabibo. Baada ya kuoga aliamua kwenda katika kiwanja cha mpira wa miguu ambako alikaa peke yake akiwaza na kutafakari juu ya uhusiano na mama yake mdogo.

“Nimekuwa na uhusiano na mke wa baba yangu kwa muda mrefu sana sasa. Kibaya zaidi nimezaa naye ingawa baba hafahamu. Kila ninapomwona baba, nafsi yangu inanishtaki na ninaogopa sana, sina raha dunia hii kila ninapokumbuka kuhusu mama mdogo. Sijui hatima ya jambo hili, kwani baba anajua Rama ni mdogo wangu. Lakini haya yote yasingetokea isingekuwa ni umalaya wa mama mdogo sijui nitafanya nini.

Hili ni kosa kubwa sana na ni dhambi mbele za Mungu. Na baba akigundua ataniua tu! Lazima ataniua.” Aliwaza Jamal. Jamal alijiuliza maswali mengi ambayo majibu yake hakuwa nayo. “Nadhani nimwambie mama mdogo ili tujadili na kuamua nini cha. Hivi hadi lini nitaendelea kukosa raha?” Aliwaza Jamal. Baada ya kukaa takribani saa tatu pale uwanjani, Jamal aliamua kurudi chumbani kujisomea kwani siku iliyofuata alikuwa na mtihani. Ulipofika muda wa usiku Jamal alikwenda kulala huku akiwa na mawazo mengi sana kuhusu mama yake mdogo na uhusiano walianao. 

Jumanne, Novemba 13, 2012

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA ....3.....

ILIPOISHIA 
“Pole sana mama mwili wa mumeo upo katika chumba cha …..? Kabla ya kumaliza kusema mama Julieth alianguka chini na kupoteza fahamu. Haraka wale askari walimbeba Mama Julieth na kumwingiza katika chumba maalumu ambako alipata huduma na kupata fahamu baada ya saa 3. Kisha daktari aliwaomba wale askari kumsindikiza mama Julieth nyumbani kwake.

INAPOENDELEA

Majirani zake mama Julieth walikwisha kusanyika nyumbani huku mmoja wao akienda shuleni kuwafuata watoto. Baada ya kufika mama Julieth vilio na kelele za kila aina vilitawala huku mama Julieth akianguka chini nakukosa nguvu kabisa. Mipango ya mazishi ilifanyika na kuamua kuzika siku iliyofuata. Siku ya mazishi watu walijaa sana huku simanzi na masikitiko vikitawala katika eneo lote la Kaloleni kwani Mzee Magesa alikuwa maarufu sana.

Mwili wa Mzee Magesa ulizikwa kwa taratibu zote huku viongozi wa dini na serikali kutoka Kaloleni wakihudhuria na kutoa nasaha zao. Huo ndio ulikuwa mwisho wa maisha ya Mzee Magesa ‘Muuza mboga’ sokoni. Wiki mbili baada ya mazishi Mama Julieth alikuwa bado hajapata nguvu za kuanza kufanya chochote. Siku moja alikuwa amekaa katika ngazi amejiinamia kama mtu ambaye amekata tamaa ya maisha, akiendelea kulia kwa uchungu. Julieth alitoka ndani akiwa ameshika kikombe cha chai na kumpa mama yake huku akimfariji.

“Mama usilie, sisi tupo na wewe Mungu atatusaidia.” Julieth alimfariji mama yake huku akimpa chai. “Mwanangu baba yenu alikuwa nguzo ya familia na sasa hayupo tena. Kumbuka mnatakiwa msome nani atawasomesha? Hivi ni kwa nini Mungu amemchukua mapema hivi?” Alijibu mama Julieth huku akibubujikwa na machozi. “Mama tusikate tamaa hata baba kabla hajafariki alisema tuwe na mshikamano na upendo katika familia yetu. Mama mimi nitakuwa nawe bega kwa bega kukusaidia.” Julieth aliendelea kumfariji mama yake.

Jumatatu, Novemba 12, 2012

SIMULIZI YA MAMA MDOGO SURA YA ........14.......


ILIPOISHIA:
Usiku mama mdogo alianzisha tena mazungumzo na baba Jamal kuhusu kumpeleka Jamal shule. Alimsifia Jamal kwamba amebadilika sana na kwamba sasa ni mtoto mzuri, hana kiburi, anajituma katika kazi na ameacha kabisa mambo ya mapenzi. Hivyo alisisitiza kwamba apelekwe shule ili akasome kwa faida yake na mdogo wake. Baada ya kufikiria sana baba Jamal alikubali na kumtaka mama yake mdogo aende shule ya Sekondari ya Jitegemee ili akatafute nafasi na kisha Jamal aanze kusoma mara moja.

INAPOENDELEA:
Siku iliyofuata baba Jamal alikwenda  kazini kama kawaida yake. Jamal aliamka saa tatu siku hiyo, kwani hakupata usingizi vizuri usiku kutokana na kuwa na mawazo mengi. Alikwenda sebuleni na kumwita mama yake mdogo aliyekuwa chumbani. Mama mdogo alipofika tu alimrukia Jamal shingoni na kumbusu shavuni. “Jamal kazi nimemaliza.” Alitamka mama mdogo huku akimwangalia Jamal.

“Kweli mama mdogo? Mbona siamini, umetumia mbinu gani hadi analainika?” Alihoji Jamal kwa furaha isiyo na kifani. “Mimi nilikwambia ilimradi tuko pamoja sasa basi utasoma. Kunywa chai haraka unisindikize Jitegemee Sekondari. Jamal alifurahi sana kupata nafasi ya kwenda shule. Maisha yalibadilika sasa Jamal alianza shule huku akijihusisha kimapenzi na mama yake mdogo. Kadiri siku zilivyozidi kwenda ndiyo mapenzi yao yalizidi kupamba moto. Baba Jamal akisafiri walikuwa wakilala pamoja bila kujali wala kuogopa. Mwanzoni Jamal alikuwa mwoga sana kufanya mapenzi na mama yake mdogo lakini baadaye alizoea na kuona kitu cha kawaida.

Siku moja baba Jamal alisafiri, na alitegemewa kurudi baada ya miezi miwili. Mke wake alifurahi kwani pale nyumbani walibaki wawili tu. Waliutumia muda huo kufanya mapenzi kwa uhuru. Jamal alitunzwa kama mume kila kitu alikuwa akipata, akitoka shule alikuta mama yake mdogo amempikia chakula kizuri na amefua nguo zake zote na kuzipiga pasi.

Alhamisi, Novemba 08, 2012

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA ....2.....



MTUNZI:  ADELA DALLY KAVISHE

ILIPOISHIA: “Baba Julieth naona tumalize maongezi kwani kesho asubuhi na mapema unatakiwa uwahi sokoni kufungua biashara. Na wewe Julieth kesho ni shule, hebu tukalale.” Alishauri mama Julieth. “Haya Julieth nenda kapumzike ila ukae nayo kichwani yote tuliyozungumza leo.” Alisisitiza Mzee Magesa huku akisimama kuelekea chumbani. “Sawa baba.” Alijibu Julieth.

INAPOENDELEA: Kesho yake asubuhi waliamka mapema sana. Julieth alijiandaa haraka na kunywa uji na kuwahi shuleni. Mzee Magesa aliweka mboga zake kwenye mkokoteni na kuelekea sokoni. Mama Julieth tayari alikwishaanza kupika chapati kama kawaida yake. “Mke wangu leo nitachelewa kurudi kwani nikifunga tu biashara itabidi niende kuchukua vitunguu na nyanya. Ninaomba leo usiku unipikie ugali na matembele.” Aliomba Mzee Magesa huku akiondoka na toroli lake kuelekea sokoni.“Haya baba kazi njema ila sio ndiyo uchelewe sana, halafu usisahau kuleta matunda.” Aliongea mama Julieth huku akimsindikiza kwa macho.

****************************************************************
Mzee Magesa alipofika karibu na sokoni akiwa anavuka barabara, ghafla lilitokea gari likiwa katika mwendo wa kasi ya ajabu na kumgonga. Mzee Magesa aliumia sana sehemu za kichwani na sehemu mbalimbali na kusababisha kutoka damu nyingi mdomoni, puani na masikioni.Wasamaria wema walimkimbilia Mzee Magesa ili kumwahisha Hospitali ya Mkoa lakini alikufa palepale hata kabla ya kuondoka. 

Mashuhuda wa ajali walijaribu kuchukua namba za gari lakini haikuwa rahisi kwani halikusimama. Walipiga simu polisi na askari walifika baada ya muda wa kama dakika ishirini hivi. Baada ya kuwahoji walioshuhudia ajali ile waliuchukua mwili wa Mzee Magesa na kuondoka. Baada ya askari kuupeleka mwili wa marehemu Hospitali ya Mkoa askari wawili walikwenda kutoa taarifa nyumbani kwake. Walipofika walimkuta mama Julieth katika biashara yake ya chapati. “Habari yako mama.” Askari mmoja alisalimia. “Nzuri tu karibuni.” Alijibu mama Julieth na kuwakaribisha akidhani ni
wateja wake wa chapati.

“Asante mama sisi ni maofisa usalama tumekuja kukupa taarifa kwamba mume wako amepata ajali.” Wale askari walizungumza moja kwa moja kitu ambacho kilimpa mshtuko mama Julieth na kushindwa kuamini alichoambiwa na kabla hawajaendelea mama Julieth aliwakatisha. “Nini? Jamani mbona siwaelewi, mume wangu amepata ajali wapi? Na ya nini? Je, hali yake inaendeleaje?” Aliongea mama Julieth maneno mengi kama mtu aliyechanganyikiwa. “Amegongwa na gari na kwa bahati mbaya gari halikusimama.” Askari alifafanua.

Jumatano, Novemba 07, 2012

SIMULIZI YA MAMA MDOGO SURA YA .....13.....



KITABU  MALIPO NI HAPAHAPA
MTUNZI  ADELA DALLY KAVISHE

ILIPOISHIA Baada ya maongezi hayo Goodluck aliaga na kuondoka kuelekea kwao akimwacha Jamal akiwa na mawazo mengi kuhusu mama yake mdogo. Siku iliyofuata yapata saa nne asubuhi wakati babake akiwa kazini Jamal alimfuata mama yake mdogo sebuleni ili azungumze naye kuhusu swala la kupekekwa shule. Alipoingia tu alimkuta amekaa katika sofa akifuma kitambaa.


INAPOENDELEA: 
“Habari za asubuhi mama mdogo? Alisalimia Jamal. “Nzuri Jamal umeamkeje? Ah! Salama kabisa” Alijibu Jamal. “Vipi Jamal mbona unaonekana mnyonge sana, unaumwa?”Aliuliza mama mdogo. “Hapana mama mdogo, nina shida na wewe.” Alisema Jamal. “Heeh! Makubwa na wewe huwa unashida? Haya hebu sema unashida gani?” Alishangaa na kuuliza mama mdogo kwa kebehi. Unajua mama mdogo mimi napenda sana kusoma, baba anaonyesha hataki tena kunisomesha. Lakini ninauhakika nikikutumia wewe anaweza kubadili msimamo wake. Tafadhali naomba unibembelezee.” Alitamka Jamal. “Jamal tatizo siyo baba yako hataki kukupeleka shule. Ila tatizo ni wewe mwenyewe hutaki kwenda shule.” Alisema mama mdogo huku akiweka kitambaa juu ya meza na kusogea kwa Jamal.

“Hapana mama mdogo mimi shule napenda sana.” Alijibu Jamal. “Hapana kama unapenda shule usingekuwa unanikatalia ombi langu siku zote hizi.” Aliongea mama mdogo huku akirembua macho. “Jamal mimi nakupenda sana na unajua fika kwa nini unakataa ombi langu? Hivi huoni kama unateseka bure kwa ujinga wako?” Aliuliza mama mdogo. Jamal alinyamaza kimya kidogo huku wakiangaliana na mama mdogo.
Mama mdogo alitabasamu kimahaba kisha akaangalia chini kwa aibu. “Unajua mama mdogo hilo ni jambo la hatari sana, baba akigundua ataniua.” Alitahadharisha Jamal.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom