Jumatano, Januari 02, 2013

SIMULIZI YA MALIPO NI HAPAHAPA SURA YA ......9.... NAWATAKIA HERI YA MWAKA MPYA NA MUENDELEE KUPATA UHONDO WA SIMULIZI


Ilipoishia: Alipofika alikuwa na wasiwasi mkubwa akifikiria jinsi atakavyokabiliana na uso wa John baada ya kuachana kwa takribani miezi mitatu. Alisogea jirani, akagonga taratibu na kusubiri afunguliwe. Mara mlango ulifungulwa na mwanamke mwenye uso wa kujiamini kisha akaanza kumsemesha Julieth: “Habari za leo dada! Alisalimia. “Salama dada yangu! Habari za hapa?” Alijibu na kuuliza Julieth. “Karibu dada nikusaidie nini?” Aliuliza bila hata kujibu swali aliloulizwa.Julieth alishtuka sana na kuingiwa na hofu kubwa kumwona yule mwanamke aliyefungua mlango. USIKOSE SURA YA 9...........

INAPOENDELEA
“Samahani namuulizia John.” Yule mwanamke alimwangalia Julieth kuanzia kichwani hadi kwenye vidole vya miguu, kisha akamkaribisha: “Karibu ndani.” Alimkaribisha Julieth huku akitangulia ndani haraka bila hata kuangalia nyuma. Julieth aliingia na kukaa katika sofa lililokuwa jirani kabisa na mlango huku moyoni mwake akijiuliza: “Huyu mwanamke ni nani?” Wakati huo yule mwanamke alikuwa amekaa katika sofa lililokuwa karibu na mlango wa kuingia chumbani, huku mtoto wa kiume mwenye umri kati ya miaka mitano na sita hivi akichezea kijigari kidogo.


Kwa takribani dakika tatu au nne hivi walibaki kimya huku kila mmoja akimwangalia mwenzie kwa kuibia. Ghafla yule mwanamke alivunja ukimya kwa kutaka kujua Julieth alikuwa na shida gani; “Samahani dada unamtaka John wa nini?” Aliuliza yule mwanamke. Julieth alitaka kumjibu lakini alisita. Baada ya dakika moja hivi Julieth alijipa ujasiri mkubwa na kumweleza kilichomleta pale ndani, wakati huo John alikuwa yupo chumbani asiyejua chochote juu ya nini kinachoendelea pale sebuleni:


“Mimi ni mchumba wa John, nilikuwa naishi hapa na nimetoka hospitali nimejifungua hawa watoto mapacha.” Alijieleza Julieth kwa ujasiri wa kuigiza. Yule mwanamke alishtuka na kusimama ghafla huku ameshika kiuno na kunyoosha shingo yake kama fisi aliyesikia harufu ya mzoga. “Wewe dada! Unajua unachoongea? Una uhakika ni nyumba hii au umekosea nyumba? Aliuliza na kuhoji yule mwanamke. “Dada yangu sijakosea kabisa ni hapahapa.” Alijibu Julieth akiwa katika hali ya kujiamini kidogo.

Yule mwanamke alimuangalia Julieth, akainama chini akitafakari jambo kisha akaendelea kufoka; “Hapa ni nyumbani kwangu, na huyo John unayemsema ni mume wangu.” Huku akimnyooshea kidole yule mtoto aliyekuwa anachezea kijigari. “Na yule pale ni mtoto wetu anaitwa Philipo. Je, huo uchumba wenu mliufanyia mbinguni? Mbona wewe dada unanishangaza sana?” Aliendelea kufoka. “Kama wewe umezaa naye mtoto, mimi nimezaa naye watoto, nakuomba niitie John niongee naye.” Alifoka Julieth huku akionyesha kujiamini zaidi kuliko mwanzo.

Baada ya kuona Julieth anavyoongea kwa kujiamini yule mwanamke alisimama haraka na kuingia chumbani akimwacha Julieth na watoto wake pale sebuleni. Julieth aliinama na kuwaza kitu; “Nakumbuka siku John aliponifukuza alisema mke na mtoto wake wanakuja je, atakuwa ndio huyu? Nahisi kama naota. Lakini ni kweli yamenikuta nitafanya nini mimi?” Julieth aliendelea kuwaza na kujiuliza maswali yaliyokosa majibu. Ni dhahiri yule mwanamke alikuwa ni mke wa John kwani alikuwa akiishi Dar es salaam akiwa masomoni katika moja ya vyuo vikuu vilivyoko huko.

John alikuwa akisafiri mara kwa mara kumtembelea na sasa alikuwa amerudi baada ya kumaliza masomo. Wakati huo wote John alikuwa anaishi na Julieth huku akimdanganya kuwa alikuwa anasafiri kikazi kumbe tayari alikuwa na mke aliyefunga naye ndoa pamoja na mtoto sasa sijui Julieth atafanya nini. Julieth aliendelea kukaa pale sebuleni akimsubiri John. Alitumia fursa hii kukagua sebule yote. Alitazama ukutani na kuona picha kubwa ya harusi iliyomwonyesha John akiwa na yule mwanamke aliyemkaribisha. Alishtuka na kuishiwa nguvu huku machozi yakimtoka asiamini anachokiona.

Mara mlango wa chumbani ulifunguliwa ghafla huku yakisikika maneno kama vile watu wanafokeana. John alitokeza huku yule mwanamke akimfuata kwa nyuma na kumkuta Julieth; “Nani kakuruhusu kuja hapa kwangu wewe mbweha mkubwa?” John alifoka na kutukuna bila hata salamu. Kisha akamgeukia mama Philipo; “Hivi mama Philipo umeanza kukaribisha vichaa humu ndani?” Aliendelea kufoka John.

“Hapana mume wangu mimi huyu amekuja anakutafuta wewe kwani unamfahamu vipi? Alihoji mama Philipo kwa upole tofauti na alivyokuwa akiongea na Julieth. “Huyu mwanamke ulipokuwa Dar es Salaam mke wangu, alikuwa ni mfanyakazi wangu wa ndani hapa nyumbani. Mimi nilipokuwa nasafiri alikuwa analeta wanaume hapa nyumbani taarifa nikawa nazipata. Baadaye alikuja akapata mimba na kuanza kusambaza maneno mimi ni mume wake nilimfukuza na nashangaa anataka nini tena hapa na pesa yake nilishampa siku nyingi” Bila ya aibu na hata huruma alisema John huku akimtaka Julieth na watoto wake waondoke na asirudi tena.

“Wewe! Wewe! John! Muogope Mungu ulinichukua kwetu Arusha na kunidanganya kuwa unanipenda leo hii unaniona sifai. Eti kichaa! Baada ya kunidanganya na kuniharibia maisha yangu leo unaniona kichaa. Ungeniambia ukweli haya yote yasingetokea, kumbe ulikuwa una mke na mtoto. Sawa! mimi nitaondoka ila Mungu ndiye atakayenisaidia nakutakia maisha mema.” Alifoka Julieth kwa mfululizo bila hata kumpa John fursa ya kujibu huku akibubujika machozi.USIKOSE SURA YA ...10......


Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom