Jumatano, Juni 18, 2014

Mumewe Flora Mbasha kizimbani


Msanii Emmanuel Mbasha (32), ambaye ni mume wa mwimbaji wa nyimbo za Injili, Flora Mbasha, amefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala akikabiliwa na mashitaka mawili ya ubakaji.

Mshtakiwa huyo ambaye ni mfanyabiashara na mwimbaji alisomewa mashitaka yake mbele ya Hakimu Mkazi Wilberforce Luago.Wakili wa Serikali Nassoro Katuga alidai kuwa mshtakiwa alitenda makosa hayo mawili maeneo ya Tabata Kimanga, jijini Dar es Salaam.

Katuga alidai katika shitaka la kwanza kuwa, Mei 23, mwaka huu eneo la Tabata Kimanga, Wilaya ya Ilala, jijini Dar es Salaam,  kinyume cha sheria huku akijua ni kosa alimuingilia kwa nguvu msichana anayedaiwa kuwa shemeji yake (jina limehifadhiwa).

Katika shtaka la pili, ilidaiwa kuwa Mei 25, mwaka huu eneo la Tabata Kimanga, jijini Dar es Salaam, kinyume cha sheria, mshtakiwa alimuingilia kwa nguvu mfanyakazi wake (jina limehifadhiwa).Hata hivyo, mshtakiwa alikana mashitaka hayo.Upande wa Jamhuri ulidai kuwa hauna pingamizi la dhamana.

Hakimu Luago alitaja masharti ya dhamana kwa mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili, mmoja awe mtumishi wa serikali na mwingine kutoka taasisi inayotambulika watakaosaini hati ya dhamana ya Sh. milioni 5.

Mshtakiwa alishindwa kutimiza masharti ya dhamana alipelekwa rumande na kesi iliahirishwa hadi Juni 19, mwaka huu itakapotajwa.

Mbasha akiwa chini ya ulinzi wa askari polisi alisindikizwa katika basi la Jeshi la Magereza kwa ajili ya kwenda kuanza maisha mapya mahabusu ya Keko, jijini Dar es Salaam.
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom