Jumamosi, Septemba 06, 2014

SIMULIZI YA MAISHA USILIE NADIA SEHEMU YA 11

Desmund alinishangaa sana hadi nami nikaanza kujishangaa kuwa huenda ni kweli nimemfananisha. Nikaanza kugwaya na kumsikililiza kwa makini kila neno alilokuwa anasema.
Lakini kutokana na kuduwaa kule niliishia kuona tu mdomo wake ukichezacheza bila kusikia ni kitu gani alikuwa akisema. Pia macho yangu yaliishuhudia hasira kali kutoka machoni mwake. Macho yalikuwa mekundu na alinyesha chuki ya waziwazi, sijui kwanini niliendelea kuamini yule ni Desmund na wala sijamfananisha, japo nilikuwa naelekea kukata tamaa sikufikia hatua ya kumkwepa niliendelea kumkabiri. 

Ile hali ya kuamini kuwa yule aliyepo mbele yangu ni Deus ilinifanya nishikwe na donge zito kooni, donge ambalo lilinikera na kunifanya nisipumue vizuri. Nilipojaribu kumeza mate ili kulilainisha, uso wangu ukachafuka kwa machozi. 
Macho yakaikosa nuru na nikashindwa kabisa kuona mbele kulikoni. Nikawa naona kama ukungu na mara badala ya kuwa kiwiliwili kimoja cha Desmund, sasa vikaongezeka na kuwa viwili. Sikujua kile kingine ni cha nani.

Kile kiwiliwili kipya kikaanza kunisogelea huku kikiwa katika mavazi ya kanga. Kabla sijakitambua kikanibamiza na kitu kizito usoni. Maumivu niliyoyapata hayasimuliki, nikapangusa machozi na mara nikakutana ana kwa ana na yule mke wa Desmund. Mwanamke aliyejifanya ni dada yake Desmund, nikamheshimu na kumtunza vyema jijini Mwanza lakini baadaye nakuja kugundua ni mke wa mume wangu!!
Desmund!!

Mshtuko nilioupata ukanifanya damu ichemke sana na mara nikahisi mchuruziko puani, nilipojishika na kutazama nilikuwa natokwa damu. Yule mwanamke alivyonibamiza na kitu kizito usoni, kisha nikakumbwa na mshtuko.
Sasa nilikuwa natokwa damu!! Yule mwanamke kuna maneno aliyokuwa anaongea kwa kikabila, baadhi niliyatambua kuwa ni matusi, kwa sasa hayana haja ya kukweleza maana nitakuwa kama nakutukana mwandishi katika kabila usiyoijua.

Niliyavumilia yote lakini akavuka mipaka akanitukania na mama yangu wa kunizaa, yule mama aliyezikwa tayari huku akiniachia laana kuwa hanipendi. Sasa watu waliosababisha niuone uchungu wa laana wanamtukana marehemu mama yangu.
Mwandishi!! Kama nilivyokueleza awali kuwa huenda Jadida aliniachia roho yake ya ujasiri na ukatili. Nilimvamia yule mama mwenye mwili kunipita mimi, hakutarajia ujio ule, nilimshika nywele zake ndefu, nikazivuta. Alipiga yowe kubwa. Nadhani unafahamu maumivu yanayopatikana ukivutwa nywele. Desmund akanivamia pale na kuanza kunipiga ngumi mgongoni lakini sikumwachia mkewe yule, nikazidi kuongeza nguvu.
Naam! Nikaridhika hatimaye, nywele zikakatika!!
Nikawa nimemnyoa bila kutumia mkasi. Nikamwachia akaanguka chini kama mzigo.
Mwandishi, nikiwa sijui hili wala lile, mara niliona kundi la watu lililokuwa likishuhudia ugomvi ule likitawanyika. Mara nikamwona mbwa mkubwa aklielekezwa kunishambulia. Si mbwa aliyenifadhaisha la! Ni mtu aliyekuwa anamwelekeza kufanya vile.
Ni mama yake Desmund!! Yule mama aliyeugua sana Desmund akakata tamaa kuwa lazima mama yake atakufa, nikachukua ada yangu ya chuo kwa penzi langu kwa Desmund na familia yake nikaamua kumuhudumia mama hadi akapona. Desmund na mama yake wakasema mimi ni Mungu wao, nikakataa wasiniite hivyo. Mama yule akadai kuwa hatanisahau kamwe katika maisha yake, nikafurahi kuwa nimepata mama mkwe anayenipenda kwa dhati, kisha akaongezea kwa kumkanya Desmund akimwambia kuwa ‘ole wake aje kuniacha siku moja’. Sasa yule mama ambaye nilishatambua kuwa alikuwa mnafiki mkubwa alikuwa ameshikilia mbwa na akiielekeza kuja kwangu. Anaielekeza kuja kunifanyia shambulizi mimi Nadia Mungu wake katika shida iliyomkumba. Sasa ni adui yake nikiwa mimi nina shida.

Mwanadamu!! Usimtendee mtu wema ukatarajia atakulipa wema vilevile, moyo wa mwanadamu una siri nzito. Mdomo wake unadanganya na sura yake inashawishi na anaweza kutokwa machozi, sauti yake ya upole ikikulaghai kuwa ana uchungu sana nawe ukasema huyu ndiye sahihi!! Kumbe ule moyo usioonekana unakukejeli na kukutukana matusi mazito!! Eeh! Mwenyezi Mungu ungenionyesha muujiza.
Hapo nikajikuta nimefanya kosa kubwa kupindukia, nilisimama na kujaribu kukimbia. Yule mama aliyekuwa na uso wenye hasira kali alimuachia yule mbwa!!
Mbwa akatii amri ya bosi wake!!
Desmund badala ya kumzuia yule mbwa yeye akamsisistiza, yaani Desmund akafurahia mimi kukimbizwa na mbwa! Desmund akatoa tabasamu kali mimi kudhalilika katika kijiji nisichokijua. 
Sijui kwanini Mungu aliniruhusu kugeuka na kumtazama Desmund jinsi alivyokuwa ananicheka!! Maana nilizidisha chuki dhidi yake, badala ya kumkimbia mbwa nikataka kumkimbilia Desmund! Kabla sijamfikia yeye mara mbwa akanirukia na kunitupa chini.
Neno la mwisho kulisikia tena kwa sauti ya Desmund!!!
“Huyu Chokoraa sijui katoka wapi maskini wee!!”
Desmund akaniita mimi chokoraa na hatambui wapi nilipotoka!!
Huenda alikuwa sahihi kabisa, kama marafiki zangu niliosoma nao hawakunikubali tena wakadai nina majini, familia yangu ilinikataa na mama akanilaani.
Naam!! Hakik nilikuwa chokoraa, lakini kuwa chokoraa mbele ya Desmund ni uongo uliotukuka. Sikuwa chokoraa, alijua kabisa maovu aliyonifanyia.

Mara yule mbwa akakutanisha meno yake makali katika paja langu!! Na hapo ndipo kiza kikatanda, kabla nuru haijatoweka nililiona tabasamu la dharau kutoka kwa Desmund!!
Kilio cha mbwa nacho kikasikika, bila shaka alikuwa anafurahia paja!
Kisha kimya!! Sikujua nilipoteza fahamu kwa muda gani.
Nilipozinduka nilikuwa nina pingu mkononi. Kila mmoja alikuwa ananizomea, lazima kuna kitu walikuwa wameambiwa aidha na Desmund ama mama mkwe wangu yule mnafiki. Walinizomea huku wakicheka haswa!!
Wakati huu nilikuwa katika mkeka, mtu pekee ambaye nilimwona kuwa mkarimu alikuwa ni nesi, ambaye bila shaka ndiye aliyenifunga bandeji katika kovu langu pajani.
Kovu la kung’atwa na mbwa!!
“Samahani dada nahitaji kuondoka hapa.” Nilimweleza yule nesi.
“Oooh!! Huwezi kuondoka dada wanadai hapo kabla umewahi kuwa na kichaa cha mbwa ni vyema twende hospitali kwanza, halafu na hawa polisi wanahitaji kuzungumza na wewe.” Aliniambia kwa upole sana.
“Nesi, sijawahi kuugua ugonjwa wa hivyo mimi.”
“Usijali dada utakuwa salama muda si mrefu!!”
“Na mbona wananizomea viumbe hawa sasa.”
“Eti ulivua nguo zako ndipo wakakushikishia mbwa maana ulitaka kuleta hatari msibani, ulitaka kufukua kaburi. Yawezekana ukichaa ulipanda, lakini usijali mrembo kila kitu kitakuwa sawa mama eeh!” nesi aliendelea kunieleza vitu ambavyo vilikuwa kama simulizi tu maana nilikuwa na akili zangu timamu na nilikuwa najua chanzo cha yote yaliyotokea.
“Nesi mimi ni mzima tafadhali niamini!!”
“Hapana binti, usingeweza kumng’oa yule mama nywele zake kwa kutumia mikono. Na kama hiyo haitoshi yule mbwa usingeweza kumvunja miguu yake kwa nguvu za kawaida.
Alipoongelea mambo haya nikakumbuka kile kilio cha mbwa kabla sijapoteza fahamu, kumbe hakuwa akilia bure. Katika tapatapa yangu nilimkamata miguu yake, hatimaye nikaivunja. Lakini eti haya yote ni kwa ukichaa wangu.
Mimi Nadia baada ya kuzushiwa kuwa nina majini, sasa Napata kesi kuwa nina ukichaa wa mbwa!!
Baada ya muda likafika gari la wagonjwa, nikakimbizwa Musoma mjini hospitali.
Kama utani vile, ile hospitali ambayo ilishindwa kumtibu Desmund alipovunjika miguu nami nikaingizwa humo.

Baada ya juma moja la matibabu. Nikahamishiwa katika jengo jingine la serikali.
Rumande!!
Nikashikiliwa kwa kosa la kufanya vurugu msibani kisha nikajeruhi na baadaye kutishia kuua. Aliyelalamika kutishiwa kuuwawa alienda kwa jina la Desmund!!
Maajabu!! Huyu Desmund aliyenikataa kuwa hanijui, akachekelea niking’atwa na mbwa sasa anadai tena mimi nimetishia kumuua!! Desmund!! Sikutaka kuamini kama familia yao ilikuwa na roho za kawaida, kila baya wananirushia mimi!!
Kila nilipotaka kuilaani familia yao nikakumbuka kuwa laana ya mama ilikuwa inaishi. Laana ya mama ikanifanya niishi kama kivuli, kivuli kisichopata muda wa kupumzika. Kila dakika kila sekunde nikawa mtu wa majanga!!
Nilipokelewa rumande majira ya saa moja usiku, tangu nesi anipatie chakula ile asubuhi nilikuwa sijapata chakula tena. Nikapokelewa katika selo ya wanawake, nikakutana na wababe. Usiku ule nikalazwa mbele ya mlango wa choo. Choo kichafu na kinachonuka, kumbuka ile bandeji ilikuwa haijatolewa na nilikuwa na maumivu bado lakini yote haya hakuna aliyejali. Nikaingizwa kule, katika siku nilizohisi kuwa dunia nzima imenilalia ni hiyo!! Nilijaribu kutoa machozi yanifariji lakini hata yenyewe hayakutoka.
Kidonda, njaa, kisha nalazwa chooni!!

Mungu msamehe Desmund! Msamehe mama yake, lakini Mungu usisahau kukilaani kizazi chake, ishushe laana yako Mungu! Ni wewe ulisema tusihukumu lakini hebu nipe nafasi ya upendeleo, nihukumie kizazi hiki..kiteseke kisha kimlaani Desmund, mama yake na yule mwanaharamu mkewe!!”….hapa Nadia akasita kidogo kusimulia, akajifuta machozi, alikuwa anatetemeka haswa, bila shaka ni hasira. Maana kwa simulizi yake hii hata mimi nilijikuta namchukia mtu nisiyemjua hata sura yake. Desmund!! Hakika nilimchukia mwanaume huyo, kisha nikajilaani kwa sababu hata mimi nilikuwa mwanaume!!. 
Nadia alipomaliza kujifuta machozi na kupenga kamasi akaendelea kusimulia.

“Nikabaki rumande nikiingoja siku yangu ya kusomewa mashtaka. Hakuna mtu aliyeniletea chakula, nilikuwa mtu wa kudowea vya wenzangu kila leo. Majira ya saa tisa nakula ugali na maharage mabovu!!
Mwandishi!! Hakuna kitu kama uhuru, ni heri uwe na mateso mtaani lakini usifungwe mahali kama nilipokuwa uukose uhuru. Mbaya zaidi sikuwa na kosa lolote sasa. Lakini nani atanitetea, sina ndugu wala rafiki!!
Ukimya wangu nikaona hauna maana hata kidogo. Katika kusoma kwangu niliwahi kusikia kuhusu haki za mahabusu. Nikaamua kunyanyua mdomo wangu na kuanza kumuita kila afande anayepita.
Nilipoona sisikilizwi nikaanza kupiga kelele kila sekunde!! Nilitaka kuijua hatma yangu. 
Hatimaye kelele zangu zikasikiwa na askari mpelelezi aitwaye Daniel ama walivyozoea kumuita kwa jina la afande Dany.” Nadia akakaa kimya kwa muda kisha akasema neno lililoniacha njia panda na kugundua kuwa binti huyu amepitia mengi, 
“Mungu amsamehe Dany kwa maovu yake, ampe kibali kwa mema aliyotenda na kama itabidi basi alazwe pema peponi!!......Dany maskini yaani alikuwa bado hata hajapata mtoto jamani, dah!! Sijui mama yake alijisikiaje baada ya kifo chake, yaani haya maisha haya. Mwandishi naomba nilale siwezi kusema zaidi kwa wakati huu.” Nadia akanyamaza na hakuendelea kuzungumza.
Nikabaki kujiuliza maswali magumu.

MOJA. Kama Nadia alikamatwa kwa kesi ile, ilikuwaje akatoka?
MBILI: DANNY ni nani na mbona Nadi anadai kuwa ni marehemu tayari..
TATU: Harakati za Nadia kudai haki yake ziliishia wapi?? 

 USIKOSE SEHEMU YA 12. Wadau mniwie radhi kwa simulizi kuchelewa kutokana na mattizo kidogo ambayo yapo nje ya uwezo ila kwasasa mtaendelea kupata uhondo hadi mwisho wa simulizi.



Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom