Alhamisi, Novemba 06, 2014

SIMULIZI YA MAISHA USILIE NADIA SEHEMU YA 21

ILIPOISHIA
Baada ya hapo nikabeba kilicho changu na kuingia katika mitaa ya Tukuyu nikiwa na shilingi elfu tano tu!!
Pesa niliyoipata baada ya mama Aswile kuiangusha akijaribu kukabiliana na mimi!!
Jonas mgongoni, kibegi kidogo mkononi!!
Nikaingia katika mitaa yenye baridi kali. Sina ndugu wala rafiki!!.........USIKOSE SEHEMU YA 21
 
INAPOENDELEA
Sikuwa nafahamu ni wapi natakiwqa kwenda muda huo, na hapo nikaanza kuona muda ukienda kwa kasi sana. Ilikuwa asubuhi mara ikawa mchana, bado nilikuwa katika kiza kinene bila jibu sahihi.Mida ya saa nane mchana Jonas akaanza kulia huku akiwa mgongoni.
 
Njaa!! Nikawaza. Nikamgeuzia kifuani na kuanza kumbembeleza lakini hakubembelezeka, nikatamani angeweza kusema nini kinamtokea nitafute njia ya kumtibia lakini hakuweza kusema na badala yake alikuwa analia tu. Nikalazimika kuingia katika banda la mama lishe, nikaomba huduma ya chakula, nikapatiwa wali na maharage. Jonas akakataa kula badala yake akaendelea kulia kwa fujo na kuwa kero kwa wateja wengine.


 Hapa nikalazimika kutoka naye nje huku ule wali nikiulipia bila kuula hata kidogo, ningeanza vipi kula wakati Jonas alikuwa analia? Yule mama alinifuata nje na kuniuliza nini kimemsibu mtoto, nikamweleza kuwa nilihisi ni njaa lakini ajabu hataki kula hata hicho chakula. Yule mama akampima joto kwa kutumia mikono yake na kisha akanieleza kuwa mtoto alikuwa amechemka sana nijaribu kumpeleka hospitali ama la nimpatie dawa za kutuliza maumivu.

Hilo la hospitali lilikuwa zito sana kwa sababu nilikuwa na shilingi 5000 tu, sasa ingetosha vipi gharama za hospitali tena kwa mgonjwa asiyefahamika magonjwa yake. Nikaamua kushika la pili, nikanunua dawa za kutuliza maumivu, nikazikoroga katika maji kishas tukasaidiana na yule mama kumywesha Jonas, alisumbua sana lakini alimeza.

Baada ya saa zima Jonas hakuwa akilia tena na alikuwa amejilaza katika mikono yangu. Mama wa kufikia ambaye hajui hata kesho yake na sasa ana mtoto mikononi mwake.
Ngoja ngoja, tafakari tafakari  hatimaye usiku ukafika akili ikiwa imeganda tu nikishindwa kufikiri hata kidogo ni kitu gani natakiwa kufanya.

Si kwamba hawakuwepo watu ambao ningeweza kuwakabili na kunipa hifadhi ya siku mbili tatu, hofu yangu ilikuwa usalama wangu katika wilaya hiyo. Hao watu niliokuwa nafahamiana nao walikuwa wakimfahamu mzee Aswile na familia yake, hivyo ilikuwa kazi nyepesi sana kuweza kuzisikia tetesi za shambulio langu dhidi ya familia ile. Na ningejuaje huenda nilikuwa natafutwa??

Ningekuwa mimi kama mimi ningejitoa muhanga lakini Jonas!! Jonas aliniumiza sana kichwa. Laiti kama ningeamua kujisalimisha huko kisha nikakamatwa, bila shaka Jonas angebaki katika familia ya mama Aswile! Familia ambayo inamuita yeye mwanaharamu. Angeishi vipi, kama wakati mtetezi wake nilipokuwa naye waliweza kumuita mwanaharamu na kumzaba vibao, je wakati ambao sipo kabisa nini kingejiri kama sio kumuua kabisa.

Hapana!! Siwezi kurudi nyuma. Nikafikia uamuzi huo. Nikasimama na kuelekea stendi ya mabasi ya pale Tukuyu, nikatafuta kona moja nikajiegesha huku Jonas akiwa salama kifuani kwangu.Sijui hata nilikuwa nawaza nini hadi kufika pale stendi. Lakini ni sehemu pekee ambayo niliamini kuwa hapatakuwa na bughuza za hapa na pale, maana nikiwa na begi langu ningeweza kusingizia kuwa mimi ni abiria.
 
Baridi ilikuwa kali sana majira ya saa tatu usiku, meno ya Jonas yakawa yanagongana mdomoni, matumbo yake yakawa yanaunguruma. Nikajisemea nafsini kuwa yule mtoto yupo katika mateso makuu, alinikumbatia kwa nguvu sana lakini sijui kama alipata alichokuwa akikitafuta.
Joto!! Hakulipata joto kwani mwili wangu wote ulikuwa wa baridi pia. Nilimsikitikia sana, nikajaribu kujiuliza tena na tena ni kitu gani naweza kufanya kupambana na hali hii. Nilitazama huku na kule, kisha nikavamiwa na wazo moja kuwa iwapo nitaleta lelemama Jonas atanifia kifuani.

Wazo la kifo likanigutusha kutoka pale chini, nikasimama wima, nikampigapiga Jonas mgongoni, akakohoa kisha akasema neno moja likaniumiza.
“Ataaka babuuu!!”
Chozi likanidondoka, nikaujua uchungu anaopitia Jonas kwa kumkosa mzee Aswile lakini nami pia nilikuwa katika uchungu mkubwa kwani laiti kama mzee Aswile angekuwepo ningekuwa natabasamu tena. Na ningekuwa nimemkumbatia Jonas huku tukiwa tumejifunika blangeti zito.
Lakini sasa nilikuwa stendi na mawazo yangu yakiwa yameganda.
Suala la kifo cha Jonas likanichangamsha na kunitia hofu kwa wakati mmoja. Na hapa nikakumbuka sehemu moja ambapo naweza kujaribu kukimbilia. Nikamkumbuka Stephano.” Nadia akasita kuzungumza kisha akanitazama na kuniuliza swali.
“Stephano…jina zuri eeeh!!” nikatikisa kichwa kukubaliana naye.
“….ni heri uwe na jina baya lakini matendo yako yawe mazuri kuliko kuwa na jina baya linaloficha matendo yako….alikuwa anaitwa Mchungaji Stephano na wengi walimuita mtu wa Mungu. Alikuwa anajitolea sana kwakweli, alikuwa akihubiri basi watu wote kimya na alikuwa anagusa samba nafsi. Mara yangu ya kwanza kumfahamu nilienda na akina Monica watoto wa mzee Aswile, ujue pale nyumbani ni mimi peke yangu nilikuwa muislamu, tena muislamu jina tu maana sikuwa nakumbuka hata mwezi mtukufu ni upi, sikumbuki mara ya mwisho kukanyaga msikiti ni lini. Kwa kifupi nilikuwa muislamu wa kale, hivyo ilipotokea familia ile inaenda katika ibada nami nilijumuika nao mara moja moja ninapokuwa najisikia, sikuwahi kulazimishwa kubadili dini hata siku moja. Na pia hakuna aliyewahi kuniuliza kwanini siendi msikitini.

 Nilipohudhuria kongamano hili ndipo nilimfahamu mchungaji Stephano, alikuja kuisalimia familia nzima ya mzee Aswile na hapo akatambulishwa kwangu. Alikuwa mchangamfu tena mwenye utani sana, haukuwa utani wa kukera, nilipomwambia mimi ni muislam akaniambia tushindane kuomba dua, aisee yule ni zaidi ya muislamu yaani kila aya ninayoifahamu mimi na yeye anaijua. Lakini mbaya zaidi alikuwa anazijua hata nisizozifahamu mimi. Ukaribu wetu ukaanzia hapa.

“Mariam wakristo na waislamu ni watoto wa baba mmoja, usisite kuhudhuria ibada kisa wewe ni muislamu, hakuna anayeutukana uislamu katika ibada na vilevile hakuna mwenye haki ya kuutukana ukristu misikitini sisi ni watoto wa baba  mmoja Mariam, usibaki nyumbani mpweke.” Mchungaji aliniambia maneo yale yakaniingia na tangu wakati ule nikawa nikipata hamu ya kusikiliza kwaya nahudhuria kanisani, na kila nilipohudhuria mchungaji Stephano alikuwa akizungumza nami.
Sikuwahi kujutia hata siku moja kuhudhuria katika ibada zao.
Kanisa lao lilikuwa maeneo ya Uyole! Na siku ya kutimiza miaka miwili tangu awe mchungaji tulipata nafasi ya kwenda kwake kusheherekea na familia yake nyumba yake ilikuwa jirani na maeneo ya Uyole. Nilipakumbuka vyema.

Jina la mchungaji huyu likawa jina sahihi kabisa kwa wakati ule, kama aliweza kunielewa vyema tangu nikiwa kwa mzee Aswile na kwa kuwa alikuwa mtu wa kujitolea basi huyu alikuwa mtu sahihi kabisa wa kumweleza matatizo yangu.
Nikaingia stendi, sasa nilikuwqa abiria kweli.
“Mbeya mjini ya mwisho, Uyole Sai, Ilomba, Mama John, Soweto……mbeya mjini ya mwisho gariii..” nilisikia sauti ya mpiga debe akiinadi gari aliyokuwa anasimamia.
Nikaingia garini nikiwa nimembeba Jonas aliyekuwa usingizini nusu na nusu macho!!
Gari likapakia kwa takribani nusu saa, na hapo likaondoka kwa mwendo wa kusuasua likiokota abiria hapa na pale.
Saa tano usiku tulikuwa Uyole, nikashuka baada ya kulipa nauli.
Sasa nikabakiwa na shilingi elfu mbili tu!
Giza lilikuwa limetanda na bado baridi iliendelea kupiga, mji ulikuwa umetulia sana. Lakini niliendelea kusonga mbele hadi nikaifikia nyumba niliyoamini kuwa aliishi mchungaji Stephano. Niligonga geti mara nyingi sana, na hatimaye nikamsikia mtu akiligusagusa.
“We nani?” sauti inayounguruma kutoka usingizini ilisema nami. Nikajitambulisha lakini hakunielewa, nikasema mimi ni muumini wa kanisa la mchungaji Stephano, hapo sasa aliweza kufungua geti.
“Unamtakia nini usiku huu.”
“Mtoto amezidiwa nahitaji huduma yake…” nilidanganya, hapa mlinzi akatilia maanani na kunikaribisha ndani. Kwa jinsi tulivyokuwa tunatetemeka hata angekuwa nani lazima angeamini nilichokuwa nasema. Mlizi akaelekea mlangoni, akanyanyua mkonga wa simu akaanza kusikiliza nikaisikia ikiita kwa ndani maana ulikuwa ni usiku ilisikika vyema. Simu ikapokelewa wakazungumza kwa dakika kadhaa kisha akaushusha mkonga chini na kungojea.
Baada ya kama robo saa akatoka mchungaji kijana, Stephano. Nikamkimbilia na kumwangukia kifuani mimi na Jonas, akaizungusha mikono yake nikalipata lile joto la upendo.

Akanikaribisha ndani sebuleni, nikaingia huku nikiwa nalia kilio cha kwikwi, akaniuliza kulikoni.  Huku akiwa ananitazama katika hali ya kutia matumaini na upendo mkuu.USIKOSE SEHEMU YA 22
 

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom