Jumatatu, Aprili 27, 2015

Embu soma Makala hii kwa umakini (Ukitaka kujua tunda bivu au limeoza unafanyaje ? )


Na. Freddy Macha
Kuna siku nilikuwa dukani nikikagua nazi kwa ajili ya kula. Nikawa nikiitikisa tikisa na kuidonoa kwa fedha, kuufahamu mlio wake. Wazungu watatu kando walinitazama wakiona kama muujiza. Nikawaambia ule ni ufundi rasmi wa Kiafrika. Sasa wakaniomba niwasaidie kukagua nazi zao. Moja ya sifa za mzungu ndiyo hiyo. Kama hajui, hataona aibu kuuliza. Utamwona mjinga mjinga kumbe mwenzio, yuko shule. Iko siku utamshangaa hata kitabu atakiandika kuhusu elimu ile. Wewe utabaki vile vile. Waafrika tuna tatizo la kutoweka kumbukumbu na taarifa. Mambo yetu mengi yameishia tu vichakani. Elimu na busara za zamani Afrika zinaanza kupotea kutokana na siye kuwa wavivu kuhimiza kumbukumbu, kimaandishi.


Wajukuu wetu watajifunza wapi?

Mwaka 2007 Rais Jakaya Kikwete alihutubia Watanzania hapa London akagusia kadhia ya wanajeshi, maana yeye kitaaluma ndiko alikoanzia. Akasema huwa jeshi huchagua vijana kwa kuwa bado wana moto na afya. Ujana ni wakati muhimu sana. Ndiyo maana ukichunguza hawa magaidi, wote hunasa vijana. Ukitazama wakimbizi wanaofia majini kwenye Bahari ya Mediterranean, takriban wote ni vijana. Waafrika walioshambuliwa na wenyeji kule Afrika Kusini, wengi wao vijana.

Kawaida mtoto asipokuwa na wa kumwongoza, hugeuka mwizi au yatima. Vijana ndiyo wanaoongoza mabadiliko (au maasi) ya kijamii duniani. Hivyo matatizo yanayoonekana ni dalili ya tu ya tunda au nazi kutokuwa sawa ndani. Kujua chanzo cha dalili ni kulifahamu tunda. Askari wanapotumwa kupiga au kuua, hupalilia tu hasira, chuki na uhasama.


Mwanzo wa wiki hii msemaji wa Shirika la Uhamiaji la Kimataifa (IOM), mjini Geneva, Uswisi, Joel Millman alisema hadi sasa Waafrika na Waarabu 1,727 wamefariki wakivuka Bahari ya Mediterranean kuingia Ulaya. Akasisitiza idadi hii ni mara 10 zaidi ya mwaka jana. Mwaka 2013 ni watu 600 tu waliokufa maji; wakafikia 4,000 mwaka 2014. Makisio ya Millman ni vifo 30,000 mwisho wa 2015. Iko kazi.

Ingawa lawama kwa Jumuiya ya Ulaya kutofanya zaidi kuwaokoa wakimbizi zimekuwa nyingi, ilitangazwa kuwa kiasi cha wakimbizi 11,000 walifaulu kutua Italia. Walipokewa na askari, wasamaria wema, wanahabari na hata mfanyabiashara mmoja aliyejitolea kuigeuza hoteli yake kuwa stara ya muda mfupi. Miongoni mwa wakimbizi hawa wanaokimbia vita, umaskini na tafrani (kutoka ukanda wa Sahel, Arabuni na Afrika Mashariki) ni kina mama waja wazito, wasichana vigoli, watoto wadogo, vijana, wanaume kwa wanawake.

Oktoba 2014, mwandishi na mkalimani maarufu wa Kiitaliano, Aldo Busi, alisema ameacha kula samaki. “Siku hizi sinunui tena samaki kutoka Bahari ya Mediterrenean shauri naogopa samaki hawa wamekula maiti za Walibya, Wasyria, Wasomali na Wairaki. Mimi si mla watu. Ninakula samaki waliofugwa au kutoka Bahari ya Atlantic.”

Wiki iliyopita BBC ilimwonyesha mwanahabari wake mweusi, Reggie Yates, akishiriki maandamano ya kundi la weupe linalopiga wageni nchini Urusi. Yates alionyesha namna moja ya makundi haya yanavyofanya mazoezi ya viungo na visu. Mkimbizi wa Kikongo aliyehojiwa alikiri kukatwa tumboni, bahati nzuri hakufariki. Na nchini Ugiriki, chama cha mafashisti, Golden Dawn, kimekuwa kikipiga na kuua wahamiaji tangu kilipoundwa miaka 30 iliyopita. Mwaka 2012 Golden Dawn ilishambulia sehemu wanayoishi Watanzania mjini Athens.

Juma lililopita eneo la Durban, Afrika Kusini, lilikuwa na makonzi kwa wageni. Kati ya waliohasimiwa walikuwa Watanzania wawili. Baada ya rabsha hizi, Rais Jacob Zuma aliahirisha ziara yake barani Asia kusimamia tatizo. Hadi makala hii ikiandikwa wageni 5,000 walitazamiwa kuondoka Afrika Kusini, huku jeshi la nchi likitoa ulinzi.

Siyo mara ya kwanza kwa wenyeji kuwahasidi wageni Afrika Kusini. Mwaka 2008, mashambulizi ya wahamiaji kwenye jimbo la Alexandria, kaskazini mashariki ya Johannesburg, yalisababisha vifo vya watu wawili na majeruhi 40. Hatimaye wenyeji 200 walitiwa nguvuni kwa hatia za kubaka, wizi, kuua, na uharibifu wa mali ya umma.

Wiki jana, Waziri Mkuu wa Ethiopia, HaileMariam Desalegn alilalamika kwa niaba ya Waafrika wote. “Tulichangia harakati za Afrika Kusini dhidi ya makaburu, hivyo ni vyema uwepo uhuru wa kila Mwafrika kwenda popote atakako ili mradi havunji sheria.”

Ama kweli shukrani ya punda ni mateke.

Tukija Afrika Mashariki.

Baada ya mauaji ya Garissa, serikali ya Kenya ilitangaza kufunga kambi ya wakimbizi wa Kisomali iliyoko Daadab, mpakani na Kenya. Msemaji wa shirika huria la kuhudumia na kutibu bure duniani, Medecines Sans Frontiers, Bw Kenneth Lavelle alilaumu kufungwa kwa kambi hiyo kuwa kutawaathiri sana maskini na wanaohitaji msaada. Mpigania haki za binadamu toka Kenya Onyonga Oloo naye alikashifu kitendo akasisitiza lazima Kenya itimize masharti ya kanuni za kimataifa na kibiashara.

Tunafahamu kwanini kambi imefungwa. Ni jitihada za serikali ya Kenya kupambana na ugaidi wa Al Shabaab. Jitihada nyingine zimekuwa ni kufunga mpaka wake na Somalia kwa kujenga ukuta mrefu utakaozuia magaidi hao kuua Wakenya.

Mifano hii michache inatufanya tujiulize kwanini watu hukimbia kwao kwenda kuishi kwingine?

Tunajuaje kuwa tunda limeoza ndani? Nini dalili za mvua?

Kundi la Al Shabaab lilitokana na hali ya uasi na serikali dhaifu baada ya aliyekuwa Rais wa Somalia, Siad Barre, kung’olewa mwaka 1991; akafariki 1995.

Tukio la wananchi wa Kilombero wiki jana kufichua waliokisiwa kuwa wafuasi wa Al Shaabab kwenye msikiti wa kata ya Kidatu na kumpiga mmoja wao (kama mwizi) kumeshangiliwa sana hasa na watoa maoni kutoka Kenya, gazeti la The Citizen.

Watanzania tuna historia ya kuunga mkono mapambano ya haki na kutetea wakimbizi duniani. Mbali na wapigania uhuru, tulisaidia kumnyofoa nduli Idi Amin mwaka 1979.

Mtoa maoni Maina: “ Kazi nzuri Tanzania. Pambana na mdudu huyu mharibifu kabla ya imani zake za enzi za watu wa mawe hazijazagaa.”

Mtoa maoni, Oluoch :“Kazi njema jamaa zangu. Na hawa viumbe watumiwe kuwataja wenzao wanaojificha misikitini.”

Kitendo cha wananchi wa Kilombero ni mfano wa kuigwa na wote. Ikiwa kila mwananchi atakuwa na msimamo thabiti kulinda nchi yetu tutaendelea kudumisha Tanzania ya amani. Hata tukiwa maskini kiasi gani, tusisahau tunaheshimika miaka mingi kwa maarifa ya kulijua tunda.

-London, 21 Aprili, 2015  Bpepe: gmacha52@gmail.com CHANZO MWANANCHI

Maoni 1 :

Amor alisema ...

Wow sijui nisemaje. Nahisi kama nimepelekwa shule. Kweli watanzania tuendelee na kazi ya kulitambua tunda.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom