Jumatatu, Januari 18, 2016

ISOME HII KWA UMAKINI "Machungu Rungu la Magufuli yaanza"


Hatua ya serikali ya awamu ya tano ya kubana matumizi kwa kuzuia wizara, taasisi na mashirika ya umma kukutana katika hoteli kwa shughuli mbalimbali za kikazi, imeanza kuleta athari chungu huku baadhi ya wamiliki wa hoteli wakisema wameathirika kimapato na sasa wako mbioni kupunguza wafanyakazi.

 
Kadhalika, baadhi ya wasomi wamesema licha ya dhamira nzuri ya serikali katika kuhakikisha inabana matumizi ili fedha zitakazopatikana zielekezwe katika miradi ya maendeleo, bado kuna haja ya kuangalia kwa umakini athari zake. Pia wameonya kuwa sekta ya hoteli ikiyumba itaathiri wajasiriamali wengi na sekta binafsi kwa ujumla.
 
Baada ya kuapishwa na kuingia madarakani Novemba 5, mwaka jana,  Rais Dk. John Magufuli ilitangaza hatua kadhaa za kubana matumizi yasiyo ya lazima ili kuipa nguvu ya kuwatumikia wananchi.
 
Miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ni ni kupiga marufuku vikao vya kazi vya taasisi na mashirika ya umma kufanyika hotelini, kufanyika kwa hafla za kupongezana, kuadhimisha wiki mbalimbali zikiwamo za maji na Siku ya Ukimwi, warsha, semina, makongamano, mikutano na mafunzo.     
 
Zingine ambazo sasa zinaelezwa kuathiri baadhi ya wajasiriamali na sekta binafsi ni pamoja na kufutwa kwa sherehe mbalimbali ikiwamo ya Uhuru, maadhimisho ya kitaifa na kimataifa yaliyokuwa yakiwalazimu wageni mbalimbali kutoka nje ya nchi kutua Tanzania au kusafiri kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine. 

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa tangu kutolewa kwa agizo la serikali kuzuia hafla, vikao na shughuli za serikali kwenye kumbi za hoteli, karibu hoteli zote hazijapata mikutano wala shughuli yoyote kutoka kweye taasisi za umma, mashirika wala wizara.
 
CHAMA CHA WENYE HOTELI
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama cha Wamiliki wa Hoteli Tanzania (HAT), Latifa Sykes, alisema sekta ya hoteli ni moja ya maeneo yanayoajiri  watu wengi kwa sababu ya kuangalia wageni na kushughulikia matukio mbalimbali, ikiwamo mikutano.
 
“Kitu kitakachotokea na ambacho kwa sasa kinatokea ni kwamba hoteli za mjini ambazo zilikuwa zikipokea mikutano mingi, sasa zitapunguza wafanyakazi,” alisema.
 
Alisema mbali na kupunguzwa kwa watu  na pato la hoteli hizo kupungua, kutaathiri pia serikali kwa sababu ilikuwa ikipata kodi mbalimbali ikiwa ni pamoja na ile ya ongezeko la thamani (VAT).
 
“Lazima tuwe makini na tujue kila hatua ina matokeo yake. Kwenye hii ya kupunguza mikutano, matokeo yake ni kupungua kwa mapato yaliyokuwa yalipwe serikalini na hakuna tena sababu ya kuwa na wafanyakazi wengi.
 
“Tunamuunga mkono Rais kwenye kubana matumizi mabaya ya serikali lakini ni vyema akaangalia hatua za utekelezaji zisiathiri uchumi na biashara zinazosaidia ukusanyaji wa kodi,” alisema.
 
HALI HALISI
Ofisa Mauzo wa hoteli ya Hyatt Regency (zamani Kilimanjaro Kempinsk), Godlove Mlaki, aliiambia Nipashe kuwa agizo la Rais Magufuli halijawaathiri sana kwa sababu hawategemei mikutano pekee ya serikali na taasisi zake kwa kuwa hoteli yao ni ya hadhi ya kimataifa.
 
Alisema athari ya moja kwa moja waliyopata kutokana na uamuzi wa serikali ni kukosa wateja ambao kwa kawaida huwapata wakati wa maadhimisho ya siku ya Uhuru, Desemba 9 ya kila mwaka.
 
Wakati wa sherehe za kitaifa, ikiwamo Uhuru, wageni mbalimbali ambao hualikwa kutoka nje ya nchi wakiwamo na marais na wafanyabishara,  hufika kwa wingi nchini na kusaidia kuingiza fedha za kigeni kutokana na kulala kwenye hoteli na huduma zingine wanazohitaji katika siku zote wanazokuwapo nchini.
 
Mlaki alisema kutofanyika kwa sherehe za Uhuru kuliwakosesha fedha nyingi kwa sababu awali hoteli yao ilikuwa ikipokea wageni kutoka nje waliokuwa wakialikwa kuhudhuria sherehe hizo.
 
Alisema hoteli hiyo yenye kumbi 10 za mikutano, wateja wake wakubwa walikuwa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na wastani wa mikutano waliyokuwa wakifanya kwa mwezi ilikuwa ikifikia 19.
 
Alisema kuna wakati walikuwa wakipata mikutano ya siku mbili hadi sita mfululizo kutoka serikalini. 
 
“Toka mwaka jana Desemba hadi Januari hatujapata (kuandaa) mikutano yoyote kutoka serikalini,” alisema Mlaki.
 
Mmoja wa wafanyakazi wa hoteli hiyo, alisema mbali na wateja wananaotaka kumbi za mikutano, hata baadhi ya maaofisa wa serikali waliokuwa wakifika hapo ili kupata kifungua kinywa na chakula cha mchana, siku hizi hawapo tena.
 
Akifafanua juu ya ugeni wa marais waliokuwa wakifika kuhudhuria shehere za kitaifa, alisema: “Wakija marais wawili tu kwa mfano, ukiweka na walinzi wao, utakuta umeshafanya biashara ya zaidi ya vyumba 30, hapo hujaweka chakula na vinywaji. Kwa hiyo ile ni biashara kubwa sana kwetu,” alisema.
 
Katika hoteli ya Bahari Beach, Meneja anayehusika na kukodisha kumbi, Robert Vitus, alisema wameathirika kwa kiasi kikubwa kwa kuwa tangu kutolewa agizo la kuzuiwa kwa vikao na mikutano hotelini, hawajawahi kupata wateja kutoka serikalini.
 
Alisema hivi sasa wateja wanaowapata zaidi ni wale wanaotoka katika taasisi na kampuni binafsi pekee.
 
"Kwa ujumla, siku zote wateja wetu wakuu ni wale wanaotoka katika taasisi binafsi na wengine kutoka nje ya nchi. Watu wa serikalini kwa kiasi fulani walikuwa wateja wetu, japo si kama ilivyo kwa hawa wengine. Hivi sasa, hata hao asilimia ndogo ya wateja kutoka serikalini hatuwapati tena," aliongeza.
 
Meneja Masoko wa Hoteli ya Blue Pearl iliyoko  Ubungo, Abdul Sheikh, alisema kutokana na serikali kuacha kufanya mikutano kwenye hoteli yao, baadhi ya wafanyakazi wamekosa kazi za kufanya.
 
“Yaani hakuna kabisa biashara siku hizi kulinganisha na ilivyokuwa awali ambapo kumbi zote zilikuwa zinajaa. Sasa hivi ni kama ulivyotukuta, hakuna kazi, kuanzia asubuhi hadi jioni, ni hivi hivi tu tunakaa” alisema Sheikh.
 
WASOMI WANENA 
Mtafiti wa Uchumi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Haji Semboja, alisema ingawa hoteli kadhaa zitakuwa zimeingia katika msukosuko wa kiuchumi, bado kuna haja kwa serikali kuangalia ushirikiano mkubwa wa maendeleo baina ya sekta binafsi na ya umma katika kukuza pato la nchi.
 
Alisema kadri anavyoona, agizo la Rais Magufuli, moja kwa moja halikulenga kusitisha mikutano mikubwa yenye idadi ya watu zaidi ya 200 hadi 500, bali ile midogo ambayo haikuwa na ulazima wa kufanyika katika kumbi za hoteli kwa lengo la kuokoa rasilimali fedha ambayo inaweza kufanya jambo mbadala.
 
“Kuyumba kiuchumi kwa hoteli hizo huenda kumechangiwa na uelewa mdogo wa tabia za Waswahili, ambao wanajumuisha kila kitu na kusababisha hofu iliyochangia kuyumba kiuchumi kwa sekta binafsi ambayo ni miongoni mwa mihimili  muhimu ya serikali hasa katika uchangiaji wa uchumi wa ndani,” alisema.
 
Mkurugenzi wa Sera wa Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI), Hussein Kamote, alisema katika nchi yoyote serikali ni muhimili wa kwanza wa ununuzi wa bidhaa na huduma, hivyo inavyobana sana matumizi yake itasababisha kuathirika kwa sekta mbalimbali na kusababisha uchumi mkuu kushindwa kukua.
 
“Kubana bajeti ni jambo la kawaida, ila ibane na kuachia ili kutoa ushirikiano mzuri kwa sababu inaweza kusababisha madhara kwa sekta iliyodhamiria kuibana. Tunajua inaweza kubana na fedha zile zikatumika katika sekta nyingine kama elimu au afya,” alisema Kamote.
 
Alisema ni vigumu hoteli nyingi kumudu kujiendesha bila kupata mteja muhimu ambaye ni serikali, hasa kwa sababu serikali imeanza kwenye eneo linalogusa sekta ya utalii ambayo ni kitovu kikubwa cha uchumi.
 
Alisema huenda ajira nyingi kwa wafanyakazi wa hoteli zikapungua huku wengi wasijue la kufanya na kujikuta wakiangukia katika kundi la wazururaji au shughuli haramu kama za utapeli.
 
IKULU YAFUNGUKA
Kaimu Mkurugenzi, Kurugenzi ya Mawasiliano Ofisi ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa, alisema kuyumba kiuchumi kwa hoteli nchini kutokana na agizo la Rais Magufuli si kazi ya serikali na wala agizo hilo haliwezi kubadilishwa.
 
Alisema Rais Magufuli alitoa agizo hilo kwa dhumuni la kupunguza matumizi yasiyo ya lazima kwa serikali na kuwataka Watanzania wote wapenda maendeleo wamuunge mkono katika suala hilo.
 
“Wizara zilikuwa zinatumia pesa nyingi sana kukodi kumbi kwa saa kadhaa wakati kuna kumbi katika wizara zao. Sasa kuyumba kiuchumi au kukosa wateja katika hoteli hiyo si kazi ya Ikulu,” alisema Msigwa.
 
Alisema hoteli zinapaswa kuwa wabunifu wa kupata fedha zaidi na si kutegemea wizara au taasisi kwenda kufanya mikutano katika hoteli zao.
 
Imeandaliwa na Gwamaka Alipipi, Fredy Azzah, Elizabeth Zaya na Efracia Massawe.
 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom