Jumatano, Machi 26, 2014

PENDELEA KULA NANASI UPATE FAIDA ZAKE

Nanasi bora ni lile kubwa na lililoiva vizuri. Ni kweli kwamba nanasi kubwa lina nyama nyingi kuliko nanasi dogo lakini hakuna tofauti ya ubora wa virutubisho kati ya nanasi dogo na kubwa, ili mradi lisiwe limeoza au lenye michubuko mingi. Chagua nanasi lilioiva vizuri na lenye kunukia.


Mara baada ya nanasi kumenywa na kukatwa vipande, linatakiwa kuliwa mara moja, iwapo litahifadhiwa kwenye jokofu kwa ajili ya kuliwa baadaye, njia sahihi ya kuhifadhi ni kuliweka kwenye chombo chenye mfuniko (container). Hii husaidia kuhifadhi virutubisho vyake kwa kipindi cha hadi siku tano bila kupoteza ubora wake, ikiwa pamoja na ladha. Unaweza kula vipande vya nanasi au juisi yake, vyote vina faida.
Nanasi linaaminika pia kuwa miongoni mwa matunda yenye Vitamin C kwa wingi ambayo kazi yake ni kuupa mwili kinga dhidi ya ‘wavamizi’ mbalimbali (free radicals), ambao wanapoingia mwilini, kazi yao huwa ni kuharibu chembembe hai za mwili.


Nanasi lina virutubisho vinavyouwezesha mfumo wa usagaji chakula tumboni kufanya kazi yake ipasavyo. Pindi mfumo huu unapowezeshwa kufanya kazi yake vizuri, mtu huweza kupata choo laini na kwa wakati kama inavyotakiwa.

Kwa kuongezea, Vitamin C inaaminika kuwa na uwezo mkubwa wa kuimarisha mfumo wa kinga ya mwili. Mwili huwa na uwezo wa kujikinga dhidi ya magonjwa madogo madogo kama vile mafua, kikohozi, homa na maambukizi mengine. 
Ukilipa umuhimu na ukiliweka nanasi katika orodha ya matunda unayokula mara kwa mara, utajiepusha na utajipa kinga dhidi ya magonjwa mengi hususan ugonjwa wa kuwashwa na kuvimba koo, ugonjwa wa baridi yabisi (Arthritis) na ugonjwa wa gauti (Gout).


Ili upate kinga dhidi ya maradhi hayo kwa kula nanasi, unashauriwa kula tunda hilo kabla au baada ya kula mlo wako. Usile nanasi pamoja na chakula kingine kwa wakati mmoja. Kwa kufanya hivyo, virutubisho vitafanya kazi nyingine tofauti na uliyokusudia. 

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Nanasi linaweza kuwa ni tunda linalopendelewa sana kutokana na asili yake ya kuwa na sukari. Kama ndizi na mafenesi, faida ya nanasi pia ni ile ya kusaidia ubongo kutunza kumbukumbu.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom