Jumatatu, Aprili 14, 2014

SIMULIZI "RAFIKI WA MWANAMKE"

ILIPOISHIA
Mmoja kati ya wale kidada aliyekuwa anaitwa Subira alisimama nakusema "Lakini jamani pamoja na yote twendeni tukamsaidie mwenzetu" Wote walimcheka na kunyanyuka huku wakiondoka na kumuacha Subira akielekea katika kile chumba alichokuwa akisikia sauti ya Mwanadodo Aligonga mlango bila ya mafanikio, akiwa ameendelea kusimama pale mlango ulifunguliwa na mume wake Mwanadodo alitoka bila ya kuzungumza chochote na kubamiza mlango kisha kuondoka na kumuacha Subira akiwa ameduwaa. 

INAPOENDELEA
Akiwa chumbani Mwanadodo alikuwa akiendelea kulia kwa uchungu kutokana na maumivu aliyokuwa akiyasikia, Subira alifungua mlango na kuingia ndani “Pole sana Mwanadodo, yaani huyu mume wako hana hata huruma jamani, kwani umefanya kosa gani?” Aliuliza Subira huku akimtizama Mwanadodo ambaye kwa sauti ya unyonge akasema “Sijamkosea chochote, amekuja na kuanza kunilaumu kuwa mimi nina mdharau, kwasababu akirudi nyumbani usiku nachelewa kumfungulia mlango, sasa nilipomuhoji kwanini anarudi usiku, muda ambao unakuta mimi na watoto tumekwishalala fofofo, alikasirika na kuanza kunipiga yaani nateseka sana rafiki yangu”. Subira alisikitika sana huku akimsihi kama ataendelea na tabia hiyo ni vyema akawashirikisha na wazazi.

Maisha yaliendelea huku Mwanadodo akiwa anavumilia matatizo yote anayoyapata kutoka kwa mume wake anayeitwa Bundala , akiamini ipo siku atabadilika na kuacha tabia ya kumpiga.Siku moja akiwa nyumbani baada ya kumaliza kupika chakula cha usiku alikuwa ameketi mezani na kumuita mume wake ili wajumuike na kula chakula pamoja. Alipofika mezani alifunua bakuli la mboga na kupakua huku Mwanadodo akiwa anamtizama. Akiwa anaaanza kula ghafla alisimama na kuanza kusema “Wewe mwanamke umeniwekea nini kwenye hiki chakula?” Mwanadodo alibaki akishangaa na kusema hee! Kwani kuna nini? Mbona umekuwa mkali hivyo mume wangu?”


Bundala alisimama akiwa ameshikilia bakuli la mboga “Wewe  mwanamke ni mchawi yaani unataka kuniloga mimi? Sasa leo nitakuonyesha”  Alizungumza Bundala na kisha alichukua lile bakuli lilokuwa na mboga na kumwagia mke wake kwa bahati ilimwagikia kwenye nguo, hakuishia hapo aliendelea kumpiga huku akisema “Leo nitakuua mchawi mkumbwa wewe” Mwanadodo alikuwa akilia kwa uchungu alijaribu kujitoa mikononi mwa Bundala na haraka alifungua mlango na kukimbilia kwa jirani ambapo aliwakuta akina dada wawili waliokuwa wakimfahamu mmoja wao akamuuliza “Haya tena kulikoni, mbona mbio mbio kama mtu aliyechanganyikiwa” Mwanadodo huku akiwa ameweka mikono yake kichwani akasema “Naombeni mnisaidie mume wangu ananiua jamani, ananipiga bila sababu”.

 Wale wanawake walicheka na kugonganisha mikono yao “Hee, ni maajabu mtu kukupiga bila sababu, na wewe hata ukipigwa ni sawa kabisa, mara ngapi watu wanakushauri uachane na huyo bwana lakini wewe bado upo naye, halafu unataka tukuasaidie embu kwenda zako huko. Aliongea Yule mwanamke huku akimtizama Mwanadodo kwa dharau, Bundala alitoka nje na kumkuta akiwa amesimama maeneo yale aliendelea kumtukana “Wewe mchawi, njoo hapa yaani unataka kuniloga mimi, leo nitakumaliza” Wale kinadada wakawa wanasemeshana “Makubwa haya, inawezekana kweli huyu mwanamke ni mchawi” Mwanadodo alikuwa anatetemeka kwa hofu lakini wale kina dada walimuacha na kuondoka Bundala alimvuta hadi chumbani huku akiendelea kumpiga”

Maisha ya Mwanadodo yalikuwa ni magumu sana pale mtaani, kwani wale kinadada walianza kumtangaza kuwa ni mchawi ndiyo maana mume wake anampiga kila siku, hali hiyo ilimpelekea Mwanadodo kuanza kutengwa na baadhi ya watu alikuwa akijisikia vibaya sana, kwani mume wake alikuwa akimfanyia ukatili  huku akiwa hana msaada wowote.Pale mtaani Mwanadodo alikuwa na rafiki mmoja tu ambaye ni Subira na alikuwa akimsikiliza na kumuone huruma sana. Sikumoja Subira aliamua kuwaalika wanawake wa pale mtaani nyumbani kwakwe kwaajili ya chakula cha mchana, walifika wanawawake wengi sana, na Mwanadodo naye alifika huku taratibu akiwa anaelekea kuketi, mmoja kati ya wale wanawake alisimama na kusema “Hee! Na huyu mchawi amealikwa? Sasa si tunalogana tu hapa, mimi naondoka zangu”.

 Mwanadodo alikuwa amejiinamia kimya huku machozi yakiwa yanamlenga lenga, Subira alisimama na kumfuata huku akimshika mkono na kusema “Jamani wanawake wenzangu, acheni kumtenga mwanamke mwenzetu, huyu ni rafiki yetu, hivi hata mmoja wenu alishawahi kufikiria mateso anayoyapata Mwanadodo, kama ingelikuwa ni wewe ungefanyaje, huyu mwanamke anahitaji msaada wetu, mume wake anamfanyia ukatili kila siku anampiga na sasa amemtangaza kuwa ni mchawi ili watu wamchukie, lakini chakushangaza hata nyinyi wanawake ambao mngeweza kumsaidia kupambana na huu ukatili mnamdharau na kumcheka na zaidi ya yote mnamtenga.Kumbukeni hakuna anayefurahi kuishi maisha ya namna hii, wanawake tupendane na tuungane kumsaidia mwenzetu” Wanawake wote walikuwa makini sana huku wakimsikiliza Subira, kila mmoja alianza kuingiwa na moyo wa imani na kwa pamoja walimuomba msamaha Mwanadodo na sasa alijumuika nao pamoja.


 Kesho yake kama kawadia mume wake alirudi nyumbani na kuanza kumtukana na kumpiga mke wake huku akimuita mchawi, wale majirani wanawake siku hiyo walijikusanya pamoja na kwenda hadi nyumbani kwa Mwanadodo kumsaidia, Walimsukuma Bundala na kumchukua Mwanadodo.  Mama Mmoja kwa ujasiri mkubwa akasema “Wewe Bundala, kwanini unamtesa mke wako kiasi hiki? Wewe ni binadamu gani ambaye hauna huruma, sasa sikiliza wanawake wote tumeungana kupambana na ukatili huu wa kijinsia tutakupeleka polisi, jichunge sana, ukirudia tabia yako lazima tukupeleke katika mkono wa sheria” Siku hiyo ilikuwa ni patashika nguo kuchanika.

Bundala alibaki ameduwaa kuona umoja ule wa wanawake, Alikuwa mpole sana, na sasa alimtizama mkewe na wale wanawake walimwambia aombe msamaha, na kama ilivyo kawaida umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu,  Bundala aliomba msamaha na kuahidi hatorudia kosa lile. Baada ya hapo Mwanadodo alirudi nyumbani huku akiendelea kuishi vizuri na mume wake. Bundala alibadilika na sasa alimuheshimu na kumsikiliza mkewe. Subira alikwenda kumjulia hali Mwanadodo walizungumza sana na kufurahi pamoja huku Subira akisema Ama kweli “Rafiki wa mwanamke ni mwanamke, tukiungana pamoja tunaweza kuteteana katika kila jambo siku zote wanawake tupendane. 

.********************MWISHO*************

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom