Jumatatu, Julai 21, 2014

SOMA SIMULIZI YA MAISHA: USILIE NADIA SEHEMU YA KWANZA UTAISOMA HAPA HADI MWISHO WAKE



SEHEMU YA KWANZA
Mwendo wa kutoka nyumba ya kulala wageni tuliyolal usiku uliopita haukuwa mkubwa sana hadi kuifikia staendi kuu ya mjini Musoma ambayo ujenzi wake ulikuwa unaendelea bado licha ya kwamba ilikuwa imeanza kutumika. Mara yangu ya mwisho kuingia katika mji huo ambao ni makao makuu ya mkoa wa Mara kituo cha mabasi bado kilikuwa kipo katikati ya mji. 

TULIPOFIKA kituo cha mabasi tuliangaza huku na kule huku tukikwepa usumbufu wa ‘wapiga debe’ wa kutuchagulia gari la kupanda huku wakitoa sifa kedekede kuhusu gari wanalolipigia debe.
“Tupande Zacharia Coach” alininong’oneza binti yule huku akinielekeza mahali zilipo ofisi zao. Tukajongea huku kila mmoja akiwa ametundika begi lake mgongoni. Nilimsaidia kubeba kifurushi kimojawapo.

Baada ya kupata tikiti zetu mbili ambazo zilituruhusu kuketi pamoja katika basi lenye hadhi ya V.IP, tulijongea upesi garini japo muda wa kuondoka ulikuwa haujafika. Lakini hatukuwa na jambo lolote la kutufanya tukae nje.

“Naomba nikae dirishani kaka” aliniomba, nikamruhusu nami nikaketi mkono wake wa kushoto, hapa sasa niliweza kumchunguza kidogo kwa macho ya kuibia ibia nywele zake jinsi zilivyokuwa zimenyonyoka, huenda ni kwa sababu ya kukosa matunzo. Uso wake ulikuwa umechujuka na ile rangi yake ya asili ilikuwa imetoweka. Alikuwa na mabaka mabaka yasiyokuwa rasmi na ambayo nilikuwa sijajua sababu yake.

Nikiwa katika kumchunguza mara alinigeukia huku macho yake yakiwa yanalengwa lengwa na machozi. Midomo ikimtetemeka, bila shaka alikuwa anataka kusema kitu, ama la kuna kumbukumbu ilimjia. Ni hicho ambacho nilikuwa nataka kutoka kwake.

Upesi nikafungua begi langu, nikatoa kijitabu changu kidogo na kalamu kisha niitegesha na simu yangu upande wa kunakili sauti. (sound recording).
Badala ya kusema neno alitazama nje pale dirishani, nami nikachungulia na kukutana na wauzaji wa bidhaa ndogo ndogo, sikujua hii inamaaanisha nini.
Binti yule akageuza kichwa na kunitazama sasa alianza kuzungumza

AKAANZIA HAPA. Nami nikamrekodi huku kiuandishi nikinukuu mazingira na muonekano wake ili nisipoteze uhalisia.“Mara ya kwanza kabisa nilikutana naye hapa, alikuwa anauza maji na soda za kopo pamoja na biskuti. Sikuwa na mpango wa kununua chochote lakini ucheshi wake ukanifanya ninunue soda ya kopo, huwa sipendi kula nikiwa safarini. Sipendi kabisa. Sijui nini kilinivuta kwake, nikanunua. Akatabasamu baada ya kuona amefanikiwa kunishawishi, wakati anataka kunipatia chenchi yangu mara gari likaanza kuondoka, nilikuwa nimempatia shilingi elfu mbili tu na alitakiwa kunirudishia shilingi elfu moja. 

Nikamsikia anapiga mayowe ya kuzuia basi lisiende anipatie pesa yangu, nilitamani kupiga kelele kumwambia abaki na ile pesa lakini sikubarikiwa uwezo wa kupiga kelele. Nilikuwa siti ya dirishani kama leo hii hapa, nikachungulia anapotokea ili kama nikifanikiwa kumuona nimpungie mkono na kumuashiria kuwa sihitaji pesa ile. Na kweli sikuwa na haja na pesa ndogo kama ile, nilikuwa na nyingine nyingi. Lakini mara macho yangu yakashuhudia kitu kibaya sana kijana yule alijibamiza katika basi jingine akapiga mweleka chini, maji na juisi zake zikatapakaa huku na huko. Hapo sasa niliweza kupiga kelele huku nikiwa nimetaharuki. Yule kijana alikuwa amepata ajali.

Safari yangu ikaharibika, nikawa namlilia mwanaume nisiyemjua hata jina na ilikuwa mara ya kwanza kuonana naye. Nililia sana bila kukoma, hakuna aliyeweza kunibembeleza maana ni moyo wangu ulikuwa unalia. Walionitazama nje hawakujua lolote. 
Laiti kama ningejua lijalo, nisingethubutu kununua maji yake mwanahizaya mkubwa yule, nisingethubutu kusema naye na nisingedanganyika na ucheshi wake hata kidogo. Yaani nikamlilia nikiwa hat simjui lakini yeye akaja kuniliza huku akiwa ananijua kila kitu nje na ndani. Akiwa anaijua historia yangu, ile siku analifukuza gari ili anipe chenchi yangu kisha akagongwa na gari akaibadilisha na kuja kunifukuza mimi ili anipige. Desmund! Desmund!! Hakufanikiwa kulipata gari alilokuwa akilifukuzia ili anipe chenchi yangu lakini alifanikiwa kunipata Desmund akanipiga, tazama alichonifanya (Hapa akajifunua kidogo blauzi yake upande wa bega…kidonda!! Sijui niite jeraha…nikachukua kamera yangu nikampiga picha.)…..kisha akaendelea tena “Desmund kweli aaargh!.....akanikanyagia chini bila huruma hata kidogo. Siku alipogongwa na gari nilitoa kelele kidogo lakini siku hii nilitoa kelele kubwa, hakukithamini kilio changu Desmund.

 Akanitemea mate kisha akaniita Malaya ninamtia kichefuchefu. Akaenda ndani ya nyumba, akaufunga mlango. Nikalala nje kwa mara ya kwanza. Mvua kali ilinyesha yote ikatua katika mwili wangu. Asubuhi alipoamka aaargh Desmund….hivi hakutosheka kunilaza nje ya nyumba yangu. Hakuridhika kwa mimi kunyeshewa mvua, akaniamkia asubuhi na kipigo, eti namdhalilisha na sikupaswa kuwa katika historia ya maisha yake!! Yaani mimi…mimi niliyeibadili historia mbaya ya maisha yake leo hii anasema sikustahili kuwa katika maisha yake…yaani kwa mambo yote niliyomfaanyia mimi…akaniita mbwa ninayefaa kuishi na kula jalalani.” Hapa akashindwa kuendelea alikuwa anatetemeka sana, uso wake ukawa mwekundu sana, mikono ikawa inatetemeka na kisha akawa anatokwa jasho. Bila shaka alikuwa na hasira iliyopitiliza. Upesi upesi nikahifadhi kamera yangu, ‘kinasa sauti’ na daftari langu vyote pamoja na kalamu nikahifadhi katika begi.

“Usilie Nadia jamani!!” nikamchukua kichwa chake, nikakilaza katika bega langu. Machozi yake yakawa yanatua katika shati langu. Alipokuwa amenilalia niliweza kuyahisi mapigo yake ya moyo. Yalikuwa yanaenda kasi sana. Na midomo ikizidi kumcheza cheza, nikajipapasa na kutoka na leso, nikamfuta machozi yake huku nikikumbuka kuwa binti huyu ana kilio moyoni haya machozi ya nje kwake si tatizo. Nikajikaza sana nisionyeshe udhaifu nami nikatokwa machozi.
Maswali na majibu yalishaanza kurindima katika kichwa changu. 

MOJA. Kumbe jamaa anayehusika na hali niliyomkuta nayo anaitwa Desmund!! 
MBILI. Kumbe alikutana naye stendi akiwa masikini wa kutupwa. Nini kikajiri sasa?
TATU. Baadaye wakaunda mahusiano? Waliunda vipi sasa mahusiano wakati walionana na kuachana pale stendi?.
NNE. Jamaa aliwahi kumpiga? Kisa nini sasa. Tena akamwita mbwa!!!

BAADAYE binti akanyamaza, sikutaka kuwa na papara za kumuuliza maswali katika mfumo wa ‘Swali na jibu la papo hapo’ nilihitaji zaidi maelezo ili nikiandika kitabu kiwe na mashiko ndani yake. Na ili kitabu kiwe hivyo basi ni vyema msimuliaji aamue mwenyewe kusema bila kuulizwa. Ama la mwandishi atumie mbinu zake ili msimuliaji ajibu bila kujua kama ameulizwa.
“Hii barabara yenu imenyooka sana….” Nilimgusia ili asikumbuke machungu ya alichokuwa anasimulia awali juu ya jinsi alivyokutana na Desmund.
Alinijibu huku akiwa amechangamka, lakini sikujua kama swali langu linaweza kuleta athari kwake!!
“Ndio ni nzuri lakini zamani sasa dah! Palikuwa na mashimo mashimo, sikudhani kuwahi kutegemea nitakuja kupita barabara kama hii. Mwaka ule ninakuja huku palikuwa hapapitiki, mimi nilidhani kuwa nilipoondoka kuwa sitarudi tena huku hata rafiki zangu niliosafiri nao kipindi kile walinambia ‘Nadia hutaweza wewe mtoto mayai’ …nilicheka tu huku nikilazimisha kuwa nitaweza. Ilikuwa haki yao kusema kuwa sitaweza, mimi mzee wangu amenidekeza, sio mimi pekee hata dada na kaka zangu wote walidekezwa sana yaani, sijui hata pale nyumbani nilikuwa nakosa nini. Shuleni napelekwa na gari na kurudishwa hivyo hivyo, nilipoingia chuo na kuchaguliwa kusomea Mwanza, sikuwahi kupanda basi kila likizo ni ndege kila likizo ndege tu. Si kwamba sikuyafurahia maisha yale la! Ila kwa kiasi fulani yaliwafanya rafiki zangu wanione mimi mzembe na ndo maana hata rafiki yetu alipofiwa na baba yake huko Mugumu Serengeti nami niliposema kuwa naenda kumsindikiza walinambia kuwa ‘Nadia huko hakuna ndege wala uwanja wa ndege’ baki tu. 

Sikukubaliana nao kirahisi, ule ulikuwa msiba. Nikalazimisha nikaenda, huko Dar es salaam, baba na mama hawajui lolote. Nd’o nikaujua uchungu wa kupanda basi tena barabara mbovu. Kutoka Mwanza hadi Musoma hapakuwa na tatizo lakini kutoka Musoma kuelekea Serengeti, nilifika nikiwa mgonjwa lakini sikutaka kudeka ule ulikuwa msiba nilikunywa dawa za kutuliza maumivu kisha nikalala, nilikuwa msichana pekee mwenye asili ya kiarabu katika msiba ule.
Maisha ya kule yalinishinda lakini nilivumilia, ukarimu wa watu niliowakuta kule ulinipa faraja nikayasahau machungu. Siku tuliyoondoka ndo niliapa kuwa sitakanyaga kule tena kwa namna yoyote. Rafiki zangu walinitania kuwa naweza kupata mchumba kutoka huko itakuwaje niliwajibu kuwa ni heri nisolewe kabisa. Lakini cha ajabu sasa ambacho hadi leo ninakishangaa nilipofika Mwanza nilirudi peke yangu tena kule Musoma, kwa lengo ambalo hadi wakati huu sijui shetani gani alilileta kwangu, nikarudi Musoma kwa ajili ya Desmund. 
Desmund kijana aliyeniuzia maji kisha akapata ajali. Nilishuka pale Musoma na kuanza kuulizia huku na kule, lilikuwa limepita juma moja tu tangu ajali ile itokee, hivyo taarifa zilikuwa zimezagaa. Nikafanikiwa kumwona tena.

Alhamdulilah!! Alivunjika miguu yote miwili, na mwajiri wake alikuwa hayupo tayari kumuhudumia, na tayari alikuwa ametafuta kijana mwingine kwa kazi ileile. Alikuwa amedhoofu sana, na matusi kutoka kwa madaktari kuwa watamfukuza pale hospitali kwa sababu hakuna ndugu anayefanya malipo yoyote. Sikungoja zaidi, nilifanya malipo kama yalivyohitajika, bado alikuwa akinishangaa kuwa mimi ni nani. Huduma ikaboreshwa, nilikesha pale wodini nikizungumza na naye na ni siku hiyo aliponiambia jina lake. Desmund!!

Nilikesha nikiumwa na mbu mimi, nikajitoa kwa moyo wote japo ajali sikuipanga mimi, lakini yeye aliponipiga na na mpini wa jembe akanivunja mguu aliniacha nikilia peke yangu barabarani, yaani kweli Desmund mimi kukuuliza tu yule mwanamke ni nani ukanipiga hadharani aah. Wema wote niliouonyesha kwake, uvumilivu wote nilioufanya kweli akaishia kunikana hadharani kwamba nilikuwaga demu wake tu lakini tumeachana tayari. Watu nisiowafahamu wakaniokota na kunipeleka hospitali nikiwa sina hili wala lile Desmund hakuja kunisalimia, hakuja kulipa bili nilizokuwa nadaiwa. Kale kasimu kangu nikaamua kukauza ili nipate tiba kwa mguu wangu uliokwisha teguka. Nilisaidiwa kurudi nyumbani baada ya kupata nafuu huku nikitumia mpini wa jembe kujikongoja…yaani Nadia mimi nikafikia kumkufuru Mungu sasa. Ndani ya chumba changu kitanda changu ninacholalia na Desmund wangu..nikakuta chupi na sidiria ..havikuwa vya kwangu. Kwa hiyo kumbe Desmund….De…De…” akashindwa kusimulia kilio kikaanza tena wakati huu safari ilikuwa inaendelea. Upesi nikahifadhi vifaa vyangu. Nikamchukua na kumlaza katika mapaja yangu, nikausikia mwili wake wa moto ukizidi kuchemka.
“Usilie Nadia…yamepita hayo mpendwa wangu…USILIE NADIA….USILIE” nilimsihi kwa upole na sauti ya chini…….
Wakati huo kichwani yakifuata maswali kadhaa na majibu.

MOJA. Kumbe Nadia alikuwa mtoto wa familia bora? Sasa kulikoni mbona kachakaa kiasi kile. 
MBILI. Kumbe Desmund alikosa wa kumuhudumia akatunzwa na Nadia, sasa mbona akamvunja mguu? Nadia alikuwa na kasoro gani kwani.

TATU. Halafu Desmund akaleta msichana nyumbani kwake? Hivi ilikuwa maksudi? Mpuuzi sana huyu. Halafu kumbe nd’o chanzo cha kumpiga kisa kuulizwa yule msichana ni nani? Au huyu alikuwa mwingine?

NNE. Hivi Nadia na kuchakaa kote huku kumbe ana elimu ya chuo kikuu tena chuo chenyewe kikuu kwelikweli!!! Sasa mbona hafanyi kazi!!
TANO. Familia yake ilikuwa wapi huyu bwege anamnyanyasa hivi? Na ni mkoa upi huo waliishi?? USIKOSE SEHEMU YA PILI.

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom