Jumatatu, Agosti 25, 2014

SIMULIZI YA MAISHA "USILIE NADIA SEHEMU YA 9"



SEHEMU YA TISA

Nadia alivuta pumzi kidogo kisha akanitazama….
“Mwandishi, hivi wanadamu wana roho za aina gani? Yaani watendwe na watu wengine halafu hasira zao wamalizie kwangu….ama hakika walipata pa kupoozea hasira zao. Alianza kijana mmoja kulaumu kuwa mimi ndiye nilikuwa chanzo cha mikosi.

 Mara mwingine akaunga mkono. Wakaanza kunizonga zonga hapo nikiwa sina walau nguo moja mwilini. Nikajaribu kujihami, hapo nikiwa nawaza kitu kimoja tu kuipata nguo yangu, hasahasa ile blauzi yenye pesa zangu ambazo nilipanga kuzitumia katika mchakato mzima wa hapo Musoma mjini nilipokuwa naelekea.

Nilijaribu kumkaba yule msichana aweze kunipatia blauzi yangu, kweli nilifanikiwa kumwangusha chini, sasa nikawa juu yake nikifanya jitihada za kuiondoa nguo.
Mara nikasikia sauti moja ikidai kuwa mimi ni kichaa na nikiachwa naweza kumuua yule binti, hapo sasa kundi la watu shupavu likanivamia. Nilipojifanya mkomavu sana nikaanza kupokea kichapo huku nikiwa uchi wa mnyama. Nilijaribu kujitetea lakini sauti yangu moja haikuwa chochote kwenye umati ule. Nikasukumiwa kichakani, huko napo kipigo kikaendelea, hatimaye sauti haikutoka tena, nikabaki kutazama tu jinsi walimwengu walivyoamua kuikatisha safari yangu hapa duniani katika namna ya kipekee.
Ninakufa nikiwa sijapata haki yangu!!
Iliniuma sana!!

Nilichoweza kukiona kwa uhakika wakati jicho langu likiwa na uhai bado ni mwanaume akija mbio huku akiwa amenyanyua kitu mfano wa jiwe juu juu. Nilifanikiwa kupiga kelele lakini sijui kama ile kelele niliisikia mimi peke yangu ama kila mmoja aliweza kuiskia. Na kama waliisikia mbona wasinisaidie.
Nilipofumba macho kukwepa kumtazama yule mtu, sikuyafumbua tena hadi nilipojikuta mikononi mwa mzee mwenye ndevu nyingi anayezungumza Kiswahili kwa shida sana.
Watoto wake hawakuweza kabisa kuzungumza Kiswahili.
Kitu cha kwanza baada ya fahamu kunirejea ni kuutazama mguu wangu, mguu ambao niliusikia ukiwa mzito sana na sikuweza kuunyanyua.
“Porepore..porepore mona wane.” Aliyasema maneno haya katika lafudhi ambayo nilikuwa naifahamu, lafudhi ya kikurya.
Nilipojitazama, mguu ulikuwa umeunganishwa na vifaa visivyokuwa vya kitaalamu sana. Na hogo lililofungwa lilikuwa limechafuka sana.
“Mama Marwaa uuuuuuh!!” aliita yule mzee, akaitikiwa na sauti ya kike kutoka mbali kiasi fulani. Kisha baada ya sekunde kadhaa akafika mwanamke imara kabisa mbele yangu.
Wakaanza kuongea kikabila!!
Sikujua nini wana maanisha!!
Lakini baadaye mzee yule aliyejitambulisha kwangu kama Marwa kwa kulazimisha Kiswahili alinisimulia jinsi nilivyookotwa hali yangu ikiwa mbaya sana wakidhani nimekufa. 
Katika kusimuliwa ndipo nikaikumbuka taswira niliyoiona mara ya mwisho kabla ya kuzimia. Kumbe yule mtu aliniponda na jiwe katika ugoko wa mguu wangu na hapo nikapoteza fahamu huku nikiuacha mguu ukivunjika.
Mzee Marwa katika kuchunga mifugo yake ndipo akakutana na mwili wangu ukiwa katika hali mbaya, lakini akabaini kuwa bado nilikuwa napumua. Hakuweza kujua nilikaa pale kwa siku ngapi nami pia sikujua lolote kwa sababu sikumbuki ilikuwa siku gani niliyozimia.

Nikayaanza maisha mapya katika familia ya mzee Marwa.
Mwandishi kuna watu wana maisha magumu sana. Wanaishi bila kuijua kesho yao lakini bado wanapata nafasi ya kuonyesha upendo wao wa dhati.
Sijui kwa nini familia ya akina Desmund haikupewa mioyo ya aina ile maana ni kama walilaaniwa wale binadamu. Mwanzoni nilidhani labda ni kila mtu katika kabila lao alikuwa na tabia kama zile lakini sasa nilikuwa nayapata majibu kuwa sikuwa sahihi hata kidogo. Tabia ya mtu hutegemea na mtu mwenyewe na wala sio kabila lake.
Mwandishi, nikikuambia kuwa zamani nilikuwa nakula sana basi huu ulikuwa mwisho, asubuhi tulitazamana tu na kama ikitokea bahati tunapata uji usiokuwa na sukari nilisikia wakiuita ‘litaghata’, mchana tulikula ugali wa mtama, na usiku tulikula ama usiku ulipita hivyo hivyo, nilihangaika sana kuizoea hali ile lakini sikuwa na pa kulalamika, mguu wangu ulikuwa mbovu.

Niliishi pale kwa miezi mine ya mateso, lakini afadhali mateso yale nilikuwa nimeyazoea, baada ya muda fulani nikiwa ninatembea vyema japo nilichechemea kidogo alikuja mtoto wa mzee Marwa, alikuwa ametokea mjini Musoma ambapo alikuwa anasoma. Nilimtambua kwa jina la Mwita japo alipenda sana kujiita ama kuitwa David. Aliichukia asili yake na hakupenda kuzungumza kabila lake, mara zote alipoongeleshwa kikabila alijibu Kiswahili. Elimu yake ilikuwa imemfanya mtumwa wa mambo ya kizungu. Kuingia kwa Mwita kukaanza kunikosesha amani kutokana na tabia zake za kupenda kunitazama kwa macho fulani yaliyoonyesha matamanio, na mara nyingine alikuwa akinikonyeza. Nilimkanya kuwa sitaki hicho anachokitaka lakini hakutaka kujirekebisha, nilitamani kumshtaki kwa baba na mama yake lakini niliona kuwa haina haja mimi ni wa kupita tu pale.

Wakati huo nilikuwa naweza kuhudhuria shambani na kulima kwa bidii. Iliniwia ngumu sana kuamini kuwa Desmund na penzi lake haramu wameniharibia maisha yangu kiasi kile. Lakini yote sikutaka yaendelee kujikita katika kichwa change nikaacha maisha yaendelee. 

Ulipotokea msiba, mzee Marwa na mkewe wakahudhuria ni hapa nilipoianza safari nyingine ya kuhaha kuitafuta amani bila kusahau haki yangu. Nyumbani tulibaki mimi, Mwita na watoto wengine wawili wadogo. Majira ya saa tatu usiku Mwita anayejiita David alinifuata katika nyumba ya majani ambayo nilikuwa naishi kwa wakati huo.

Hapakuwa na umeme katika mji ule wala majirani hivyo kiza kilikuwa kimetanda haswa. Mwita alikuwa peke yake mwanzoni. Alianza kunieleza mambo ambayo ninayaita ya kipuuzi, alilalamika kuwa kulikuwa na baridi sana, sikumjibu niliendelea na shughuli yangu ya kushona nguo yangu iliyokuwa imechanika.
Aliongea mengi lakini nilimweleza kuwa sipo tayari kwa jambo lolote lilena iwapo akiendelea kunilazimisha nitamshitaki kwa baba yake.
Huenda jibu hili lilimkera sana Mwita, akaondoka na kisha baada ya nusu saa hivi akarejea akiwa na kikundi cha wanaume wanne wote walikuwa wanaongea kikabila na sikuweza kuwaelewa walichomaanisha.

“We demu unajifanya mjanja sio.” Alinikoromea kijana mmoja, lafudhi yake ikifanana kabisa na ile ya Desmund kabla hajajanjaruka. 
Niliwatazama sikusema neno, wakasemezana kikabila tena. Mara mmoja wao akanishika mkono nakutaka kuninyanyua. Mwandishi wale watu wana nguvu balaa!! Nilijaribu kujitoa lakini haikuwezekana, wakaanza kunivuta kuelekea walipojua wao. Giza lilikuwa limetanda haswa. Niliendelea kupambana lakini hali haikuwa shwari. Hatari mbele yangu.
“Mwita nipo katika siku zangu!!!” nilimlilia yeye ambaye nilikuwa nikimfahamu kwa jina, lakini hakutaka kunisikiliza alikuwa amekasirika.
“Acha ujanja wa kizamani we demu, mbona hukusema mapema.” Alinikaripia kijana mwingine. 
Sasa tulikuwa tumekifikia kichaka fulani, wakanisukuma huku na kule, wakafanikiwa kuitoa kanga yangu.
Nikaiona dalili ya kubakwa. Sikuwa tayari kwa jambo lile. Nikafurukuta hukuna kule lakini ushindi ulikuwa upande wao.

“Haya nimekubali naomba nilale mimi mwenyewe.” Niliwasihi, wakanielewa. Nikajilaza chali, wakaitoa nguo yangu ya mwisho.
Hakika nilikuwa katika siku zangu na ndio kwanza nilikuwa nimeanza, lakini wale vijana walionekana mshipa unaosaidia kuona kinyaa kwao haukuwepo. Hawakujali ile damu!!!
Mwita akajiteua kuwa wa kwanza. Mimi nilikuwa nikiombea wafanye kosa lolote niweze kutimua mbio. Lakini wakati huo huo nikajiuliza iwapo nitakimbia ni wapi naelekea sasa, kulikuwa na giza nene sana.
Mwita akaondoa nguo zake na kunivamia pale chini tayari kwa kuniingilia kimwili.
Wakafanya kosa!! 
Kosa ambalo walipaswa kujutiana hawakuupata muda huo wa kujutia.
Kijana mmoja aliyekuwa ameshika panga kali kabisa alilichomeka chini. Akaanza naye kuvua nguo zake ili zamu yake ikifika imkute akiwa tayari tayari.
Hilo likawa kosa ambalo nililisubiri bila kujua kama litatokea.
Mwita alikuwa amejiweka kimjini mjini na hakuwa shupavu kama wenzake. Hata mimi kukaa kwangu kijijini kwa muda mfupi niliweza kumuhimili. Alipokuwa juu ya kifua changu akitaka kunibaka, nilimuhesabia mara tano tu kuwa atakuwa katika ulimwengu mwingine.

Kweli nikahesabu kisha kwa nguvu zangu na kujitetea kwangu kwa mara ya mwisho, chuki ikinitawala juu ya wanaume, nilimrusha mbali nami, kisha upesi nikasimama na kukimbilia lile panga, nikalitia mkononi.
Nikashukuru kwa sababu nilikuwa mzoefu tayari katika kukata kuni kila kukicha hivyo nililimudu panga.
Nikaanza na yule aliyekuwa uchi nikamfyeka mgongoni akaangukia pembeni huku akipiga yowe kikabila, nikamrukia Mwita, sikutarajia kama nitamkata shingoni lakini panga lile kali lilitua shingoni.
Mwita hakupiga kelele, kijana mmoja aliyebakia akawahi kutimua mbio. nami nikatimua mbio baada ya kuikwapua kanga yangu , panga mkononi, mbio kuelekea popote penye njia. 
Kwa sababu nilikuwa nakuja kukata kuni mara kwa mara nilijikuta naizoea njia!!!
Nilijua tayari nimezua balaa na sitakiwi tena hapo kijijini.
Nikaendelea kukimbia hadi nilipoifikia barabara ya lami…..
Lami ya kuelekea Musoma!!!
Musoma kwa akina Desmund.
Nilikuwa na panga langu bado kwa ajili ya kukabiliana na hatari yoyote usiku ule.
Mvua kali ilinikuta barabarani!! Nikiwa sijui lolote la kufanya kujiepusha na balaa ambalo lilikuwa linanikabili.
Mvua ilinipiga, nikaanza kujiuliza kuwa mimi nanyeshewa, Desmund aliyenidhulumu mali zangu na kisha kuupondaponda moyo wangu alikuwa amelala ndani, amemkumbatia mkewe na wamejifunika blangeti….tena bila shaka walikuwa wameahidiana kuamshana asubuhi wawahi kazini.
Kazi ambayo ni jasho langu mimi Nadia, nikapandwa na hasira kisha hapo nikaikumbuka simulizi marehemu Jadida baada ya kuja Musoma katika kunisaidia kudai haki yangu!!! USIKOSE SEHEMU YA KUMI

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Jamani..haya maisha haya. Ahsante da Adela lkn unachelewa kuweka.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom