Jumatatu, Oktoba 20, 2014

SIMULIZI YA BADO MIMI SEHEMU YA 35





ILIPOISHIA
 Sauti ilizidi kupaa juu kwa ukali ikiambatana na kicheko cha cha ajabu, Renata alipata hofu zaidi na wakati huu Charito alikuwa ameshikilia kisu kilichokuwa kinatiririsha damu mithili ya maji yaliyofunguliwa bombani, alikuwa akimsogelea Renata ambaye alipiga kelele kuomba msaada “Mamaaaa nakufaaa, nisaidieni jamani nakufaaaaa Mungu wangu nisaidieeeeee mamaaaaaa” Ilikuwa ni sauti kali sana, Kandida aliisikia sauti ya Renata akiwa chumbani na alishtuka moja kwa moja alikimbilia chumbani kwa Renata.JE NINI KITAENDELEA USIKOSE SEHEMU YA 35.

INAPOENDELEA
Nilipofika chumbani kwa Renata, nilimkuta akiwa amejikunyata huku akilia na kutetemeka sana, nilipata hofu  na mwili wangu ulisisimka kutokana na kuogopa nini kitakuwa kimemsibu mdogo wangu, nilimsogelea na kumuuliza “Kuna nini Renata mbona unapiga kelele kiasi hicho, umepatwa na nini wewe?”.

 Renata alinishika na kunikumbatia huku akisema “Dada, nimeota ndoto mbaya sana, shemeji na mchungaji Mkombozi walikuwa wanataka kuniua, Dada naogopa mimi siwezi kulala peke yangu, wameniambia bado mimi, yaani bado mimi watakula nyama yangu” Nilimsikiliza kwa makini bila ya kuzungumza chochote huku moyoni mwangu nikiwaza “Mungu wangu, nyumba hii inamatatizo gani, Renata atakuwa namashetani, kwani amekuwa akiongea sana mambo ya ajabu, mbona mimi sijawahi kuona ubaya wa mume wangu wala mchungaji Mkombozi, eeh Mungu nisaidie kwani kila siku ni afadhali ya jana”.


 Nilikuwa nawaza huku nikimtizama Renata aliyekuwa akiendelea kulia huku akisema “Dada, mimi nakuambia umezungukwa na watu wabaya, mpigie simu mchungaji James aje kunichukua, mimi siwezi kulala huku ndani.” Wakati huo ilikuwa ni majira ya saa tisa usiku, nilimtizama na kusema “Renata hiyo ni ndoto mdogo wangu usiogope, na inatokana na wewe umekuwa ukiwaza mambo mabaya kuhusu shemeji yako, sasa muda huu  unataka nimuite mchungaji ni kitu ambacho hakiwezekani, wewe lala halafu kesho ukitoka tu shule, tunaenda kwa mchungaji James” Nilimbembeleza lakini alikataa kabisa kulala mwenyewe sikuhiyo ilinibidi nilale naye hadi ilipofika asubuhi ambapo mume wangu Charito alikuja chumbani na kutuamsha kwani tayari ulikuwa ni muda wa Renata na Tumaini kujiandaa kwenda  shule.

 Haraka niliamka kwenda kuandaa kifungua kinywa na wakati huo  Renata na Tumaini walikuwa wakijiandaa,  Charito aliwahi kuondoka sikuhiyo, huku akisema “Leo kuna kazi natakiwa niwahi kuifanya, hivyo hata chai sintoweza kunywa, kwani naweza kuchelewa” Aliongea huku akiwa anaondoka, nilimaliza kuandaa kifungua kinywa, na baadaye tulijumuika na kunywa chai pamoja, sikuhiyo Renata alikuwa mkimya sana kwani hakutaka kuzungumza chochote kama ilivyokawaida nilimtizama na kusema “Renata vipi, mdogo wangu unajisikiaje hali yako” Alinitizama nakusema “Mimi mzima dada hakuna tatizo”.

 Aliitikia kwa sauti ya unyonge na ghafla alisimama huku akiwa bado hajamaliza kunywa chain a kulekea mlango wa kutoka nje nilishindwa kumuelewa na kuuliza “Mbona haujamaliza kunywa chai wewe unaenda wapi, subiri nitawapeleka shule pamoja na mdogo wako unanisikia wewe.” Renata aliendelea kuondoka bila ya kugeuka nyuma na hakunijibu chochote. Nilimuacha nakuhisi labda kuna kitu amechukia, na hivyo ameamua kwenda kukaa nje na kutusubiri hivyo niliendelea kunywa chai na Tumaini huku nikiwaza “Huyu Renata sijui anamatatizo gani, jamani mbona Napata wasiwasi sana juu ya huyu mtoto” Baada ya Muda kama dakika tano kupita tokea Renata atake nje, nikiwa najiandaa kunyanyuka na kuondoa vyombo nilisikia kelele za watu nje kwa mbali lakini sikuzitilia maanani.

 Baadaye niliona kelele zinazidi ilinibidi nitoke nje na kutaka kujua nini kinaendelea nilipotoka kwanza nilitizama huku na kule pale barazazni ambapo nilijua Renata angekuwepo lakini sikumuona nilipotizama kwenye geti lilikuwa halijafungwa lipo  wazi moja kwa moja nilitoka nje na kuona umati mkubwa watu wakiwa wamezunguka huku na kule wengine wakisema "ajali, jamani, halafu aliyegonga amekimbia hata namba ya gari hakuna aliyekariri" nilimuona Mama mmoja ambaye nilikuwa nikifahamiana naye pale mtaani alinisogelea huku akisema Kandida, jamani Kandida uwiiiiii jamani….. nilishtuka sana kumuona katika hali ile haraka nilisogea kwenye ule umati na kutizama aliyekuwa amegongwa na gari masikini  alikuwa ni Renata mdogo wangu, nilipiga kelele huku nikiwa nimeweka mikono yangu kichwani sikuamini nilichokuwa nakiona damu zilikuwa zimetapakaa pale chini, nilisogea karibu zaidi na kujikuta miguu yangu yote imeishiwa nguvu huku nikitetemeka sana baadhi ya kina mama walinishika lakini hakikusaidia hatimaye nilianguka chini na kupoteza fahamu. 

Baadaye nilizinduka na kujikuta nikiwa nyumbani ambapo pembeni yangu alikuwepo Charito mume wangu nilijikuta naanza kulia kwa uchungu sana “Masikini mdogo wangu, Renata wangu  jamani, inaniuma sana mdogo wangu, tulikuwa tunakunywa chai pamoja asubuhi, yalaiti ningekushika mkono usitoke nje, mdogo wangu moyo wangu unaumia sana jamani”  Nililia sana kwani nilikuwa siamini kama Renata amefariki, Charito alijitahidi kunibembeleza na kusema “ Nyamaza mke wangu usilie mke wangu, yote hiyo ni mipango ya Mungu, sisi tulimpenda lakini Mungu kampenda zaidi” USIKOSE SEHEMU YA 36 sasa tutaanza kuipeleka haraka hadi mwisho wake.

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom