Jumanne, Juni 02, 2015

SOMA WALICHOSEMA LOWASA, WASIRA NA MWIGULU NCHEMBA WAKATI WALIPOTANGAZA NIA



Lowassa alisema pamoja na kuwa viongozi waliopita wameliongoza taifa hili vizuri, bado linahitaji kiongozi mwenye uthubutu na uongozi madhubuti unaoweza kufanya maamuzi magumu. 

“Kuamini kama una uwezo na shauku, hakuna budi kwenda sambamba na uwezo wa kusimamia yale unayoyaamini. Na kwangu haya mawili ni dhahiri. Nina ari, nina shauku na nina uwezo, kama rekodi yangu inavyothibitisha,” alisema Lowassa huku akishangiliwa.

“Tunapomtafuta Rais wa Jamhuri ya Muungano ni lazima tukumbuke kwamba tunamtafuta mtu ambaye atakuwa pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama katika nchi yetu. Na kwa Chama cha Mapinduzi tunamtafuta mtu ambaye atakuwa pia mwenyekiti wa chama chetu.
“Naamini kwa vigezo vyote, nina kila sifa ya kubeba dhamana hizo nzito. Katika mambo ambayo najivunia, na sitayasahau katika historia yangu ni kushiriki kwangu kuilinda nchi yetu pale nilipohitajika. Nilishiriki kikamilifu katika Vita vya Kagera nikiwa miongoni mwa askari wa mstari wa mbele wa mapambano.”
Lowassa pia alikumbusha tukio la mwaka 1995 alipojitokeza kugombea urais kwa pamoja na Rais Jakaya Kikwete.
“Wakati ule sote tulikuwa wanasiasa vijana. Pamoja tulikwenda kuchukua fomu na baadaye kwa pamoja tukazungumza na waandishi wa habari. Tulileta hamasa kubwa pale tulipofanya jambo ambalo halikuzoeleka kwa Watanzania kwa kutangaza kwamba yeyote atakayepita kati yetu, mwenzake ambaye hatafanikiwa angemuunga mkono,” alisema na kuongeza:
“Natarajia safari hii, Kikwete ataniunga mkono.”

“Ninachoomba kutoka kwenu, mniamini na mniunge mkono katika hili… nitawavusha. Lakini tukumbuke kwamba kila mmoja lazima atimize wajibu wake katika utendaji kazi ili tufikie huko tunapotaka kufikia.”
Nchemba aliyekuwa ameongozana na mkewe, Neema na watoto wake watatu, Isaack, Grecious na Joshua pamoja na ndugu jamaa na marafiki, alisisitiza kuwa ili kufikia malengo hayo, lazima nchi iwe na mfumo wa uwajibikaji utakaowezesha kulinda rasilimali za Taifa na kuongeza Pato la Taifa.
Huku akitumia kauli mbiu ya ‘Mabadiliko ni Matendo, Wakati ni Sasa’, ambayo ataitumia katika safari yake ya kuelekea Ikulu, Nchemba aliyetumia dakika 115, kuanzia saa 10.10 jioni hadi saa 11.25 jioni, alisema atapambana na tabia za watu kufanya kazi kwa mazoea, rushwa, ufisadi na kwamba Serikali ya Awamu ya Tano atakayoiongoza endapo atachaguliwa, itakuwa ya uadilifu na uaminifu.
Alisema iwapo atachaguliwa, ataifanya nchi kuwa ya kipato cha kati sambamba na watu wake, kujenga Taifa linalojitegemea kibajeti na kuwajengea uwezo wananchi kumiliki uchumi wao wenyewe.
Huku akieleza jinsi atakavyomaliza kilio cha ukosefu wa ajira, wanafunzi, wakulima, wafanyakazi, wafanyabiashara na watu wa kada mbalimbali nchini, Nchemba alianza hotuba yake kwa kuwashukia baadhi ya watu wenye dhana potofu juu ya mtu anayestahili kuwa rais wa nchi.
“Nimeamua kutangazia nia hapa Dodoma kwa sababu ndipo makao makuu ya nchi na kama nikiwa Rais nitaapishiwa hapa. Pia sikutaka kutangazia nia nyumbani Iramba ili kuondokana na umimi,” alisema na kushangiliwa na mamia ya watu waliohudhuria mkutano huo.
Awajibu wanaomponda
“Uzoefu ni mazoea ya starehe. Mtu aliyekaa katika uongozi ni mtu aliyesahau shida za Watanzania.
Jambo la kwanza na la msingi ni kuitambua ajenda ya Watanzania, Watanzania watamuunga mkono kiongozi kwa kuitambua ajenda yake,” alisema.
Alisema wakati akijitathimini kutangaza nia ya kugombea alikuwa akifahamu ajenda ya Watanzania, huku akisisitiza kuwa umaskini hakuusoma katika vitabu, bali amekulia katika maisha ya kimaskini.
“Kwanza ni haki yangu. Raia wote wana haki ya kugombea, ni haki ya kikatiba. Lakini ninayo sababu nyingine ambayo ni kubwa zaidi, naifahamu vizuri Tanzania kwa muda mrefu tangu miaka ya 1970 nimeshirikishwa katika uongozi wa Taifa hili nikiwa na miaka 25,” alisema Wasira akibebwa na historia ya utendaji ya muda mrefu.
Wasira alitamba kuwa iwapo atateuliwa na CCM na kushinda urais, Serikali yake itasimamia uadilifu na kupambana na rushwa na amedhamiria kupandisha viwango vya maendeleo. Aliwaonya Watanzania kutothubutu kuukabidhi urais kwa mla rushwa, kwani kuna siku atauza Ikulu.
“Ili kukabiliana na changamoto hizi kubwa, itakuwa lazima kwa chama chetu kumteua mgombea ambaye hana historia ya kuhusishwa na ufisadi, iwe kwa kutuhumiwa tu au kuhusika kweli. Mgombea anayejua historia ya nchi yetu, pale ilipo na kule inakopaswa kuelekea.”
Akimnukuu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere mara kwa mara, Wasira alisema kiongozi huyo aliwahi kusema kuwa rais wa Tanzania ni lazima achukie rushwa na anatakiwa aonekane kwa vitendo akiichukia... “Siku hizi kila kiongozi anakemea rushwa kama fasheni hata wala rushwa wanaikemea kwa sababu bila kufanya hivyo wanaona mambo yao hayatawanyookea.”
Kauli hiyo ya Wasira iliwafanya wafuasi wa chama hicho kusimama na kumshangilia huku wakiimba ‘Wasira sema usiogope.’
Alisema: “Mwalimu Nyerere aliwahi kuniuliza ninataka nini kati ya utajiri na kuongoza watu, alisema nikitaka utajiri nichague kuwa mfanyabiashara kwani nitanunua kwa bei rahisi na kuuza aghali.”

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom