Jumanne, Julai 21, 2015

"Hatutarajii kushuhudia kasoro kubwa uandikishaji BVR Dar."


Kazi ya uandikishaji wa wapigakura kwa kutumia mfumo wa kielektroniki (BVR) inatarajiwa kuanza jijini Dar es Salaam kesho na kukamilika kufikia mwishoni mwa mwezi huu. 
 
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), uandikishaji jijini Dar es Salaam utahitimisha kazi hiyo iliyoanzia mkoani Njombe, Februari mwaka huu na kuendelea katika mikoa mingine yote ya Bara na visiwani, Zanzibar.
 
Sisi tunaitakia NEC mafanikio mema katika kufanikisha kazi hii jijini Dar es Salaam, tukiwa na matumaini makubwa kuona kuwa hakutakuwa na vikwazo vikubwa kiasi cha kuathiri shughuli hii ambayo ni mwanzo wa hatua muhimu za kuelekea Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu.
 
Kati ya mambo tusiyotarajia kuyashuhudia kuwapo kwa kasoro zilizowahi kuripotiwa katika mikoa mingine. Ni imani yetu vilevile kuwa NEC ingali na taarifa za kutosha juu ya jiji la Dar es Salaam na hivyo imejipanga vya kutosha kuhakikisha kuwa hakuna changamoto isiyopatiwa suluhisho kungali mapema. 
 
Kwa mfano, taarifa iliyotolewa jana ilieleza kuwa NEC inatarajia kuandikisha watu milioni mbili jijini Dar es Salaam. Idadi hii ya watu wenye sifa za kupiga kura ni kubwa kuliko mikoa mingine yote ambayo tayari kazi hii imeshakamilika. Kwa sababu hiyo, tunaamini kuwa tayari NEC imeshajipanga kuandikisha kila mwananchi mwenye sifa jijini Dar es Salaam.
 
Ni imani yetu vilevile kuwa NEC wanatambua kuwapo kwa changamoto ya foleni za magari barabarani zinazoathiri usafiri wa kutoka sehemu moja ya jiji hadi nyingine. Kwa kutambua hilo, siku zote maafisa wao watalazimika kujihimu mapema ili hatimaye wafungue vituo kwa muda uliopangwa, ambao ni saa 2:00 asubuhi hadi saa 12:00 jioni. 

Tunaamini kuwa NEC wamejipanga vya kutosha pia kukabiliabna na watu wengi watakaokuwa wakijitokeza kila uchao katika vituo vya uandikishaji huku kila mmoja akitaka ahudumiwe yeye kabla ya wengine. Hili linatarajiwa kutokea kwa vile uelewa wa watu wa jiji la Dar es Salaam kuhusiana na masuala ya uchaguzi mkuu, na hasa umuhimu wa kujiandikisha kwa ajili ya kupiga kura, ni mkubwa kuliko ilivyo katika maeneo mengine mengi nchini. 
 
Ni wazi kwamba kwa kutambua hili, ndipo NEC ilipoamua kuwa idadi ya BVR zitakazotumika jijini Dar es Salaam ni mbili kwa kila kituo huku maafisa wa uandikishaji wakiwa zaidi ya 3,300, mgawanyo wake ukiwa ni maafisa 1,144 watakaokuwa katika Manispaa ya Temeke, Kinondoni (1,412) na Ilala maafisa  792. Huu ni mgawanyo mzuri wa vifaa na rasilimali watu kulingana na idadi ya watu katika kila manispaa na hivyo ni dhahiri kuwa uandikishaji utakamilika kwa muda uliopangwa.
 
Inakumbukwa kuwa wakati NEC ikiandikisha wapiga kura katika mikoa mingine, hasa ile ya mwanzo ya Njombe na mengine ya Nyanda za Juu Kusini, kulikuwa na mfululizo wa taarifa za kuwapo kwa kasoro hizi na zile. Na hata walipokuwa katika mikoa ya Arusha, Geita na kwenye visiwa vya Zanzibar hivi karibuni, NEC walikumbana pia na changamoto mbalimbali. Mojawapo ya kero ilikuwa ni mgawanyo usiozingatia wingi wa watu kwenye maeneo na pia kuchelewa kufunguliwa kwa vituo. 
 
Yapo maeneo pia yalikumbwa na tatizo la kuwapo kwa uhaba wa vifaa na kwingineko, vituo vya uandikishaji vilidaiwa kuwa mbali na maeneo ya makazi ya watu. 
 
Ni imani yetu kuwa NEC imeshapata uzoefu wa kutosha kupitia maeneo mbalimbali ilikokamilisha uandikishaji na hivyo kasoro hizi na nyingine nyingi zilizoripotiwa hapo zimeshapatiwa majibu. Kamwe hazitakuwa chanzo cha kukwamisha malengo ya uandikishaji jijini Dar es Salaam.
 
Kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam, ni muhimu kwao kujitokeza kwa wingi ili watekeleze wajibu wao wa kujiandikisha na mwishowe kupata fursa ya kushiriki uchaguzi mkuu, lakini wakitambua kuwa wanapaswa kuzingatia taratibu watakazoelekezwa, huku wakijua kuwa kila mmoja huwa na haraka na angependa aandikishwe mapema kabla ya wengine. 
 
Yote haya yakizingatiwa, ni wazi kwamba hakutakuwa na kasoro kubwa zitakazokwamisha uandikishaji wa wapiga kura jijini Dar es Salaam. 
CHANZO: NIPASHE

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom