Jumamosi, Agosti 15, 2015

YALIYOJIRI MBEYA LOWASA AHUTUBIA MAELFU YA WAKAZI WA JIJI HILO.


Ni kama mgombea urais wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, ametuma salamu kwa jeshi la polisi kutokana na utitiri wa wakazi wa jiji hili ‘waliokaidi’ katazo la maandamano na kuja kumpokea kwa maandamano yaliyosimamisha jiji la Mbeya.
 
Pamoja na askari polisi waliotanda barabara nzima kuanzia uwanja wa ndege Songwe hadi viwanja vya Ruanda-Nzovwe, ambao walizuia msafara wa Lowasa mara tatu, walishindwa kudhibiti waandamanaji.
 
Maandamano ya jana yanatokea siku moja tu baada ya Jeshi la Polisi nchini kutoa amrri inayopiga marufuku maandamano nchi nzima mpaka baada ya uchaguzi mkuu, haikufua dafu wakati mgombea wa urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Edward Lowassa alipoliteka jiji la Mbeya kwa saa kadhaa.
 
Wananchi hao waliandamana kutoka uwanja wa Ndege wa Songwe, walimsindikiza mpaka katika Uwanja Ruanda Nzovwe (Uwanja wa Dk. Slaa) ambako alifanya mkutano wa utambulisho na kuwashukuru wakazi wa Mbeya waliojitikeza kumdhamini katika harakati zake za urais.
 
Polisi walijaribu kuuzuia msafara huo mara tatu bila mafanikio, kwani mbali na waliokuwa wakisindikiza msafara, karibu kila alipokuwa akipita mamia ya wananchi walikuwa wamesimama pembeni mwa barabara wakimshangilia Lowassa na kumtaka awasalimie.
 
Utitiri wa polisi ulianza kuonekana nje ya uwanja wa Ndege wa Songwe, wakiwa nje na silaha yakiwamo mabomu ya machozi.
 
Jaribio la kwanza la kuzuia wafuasi wa Chadema lilitokea eneo la Ifisi baada ya gari ya Lowassa na viongozi waandamizi wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kupita.
 
Lowassa aliambata na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, Mgombea Mwenza, Juma Haji Duni, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, Mwenyekiti wa NLD, Emanuel Makaidi, lilionekana kutozaa matunda kwani wale wenye pikipiki waliufuata nyuma msafara huo mara naada tu ya kuingia kwenye barabara ya Mbeya –Tunduma.
 
Awali ndani ya uwanja wa ndege, yaliruhusiwa kuingia takribani magari 20, ambayo yalipangwa kuwa kwenye msafara huo ili utembee haraka na kufima Mbeya mjini mapema.
 
Msafara ulipofika eneo la Ifisi kilometa chache kutoka uwanja wa ndege Songwe, polisi walilazimika kuziba barabara kwa magari mawili yaliyokuwa na askari wenye silaha za moto lakini waendesha bodaboda waliwapiga chenga askari na kupita mashambani kuunga msafara.
 
Baada ya muda magari yaliyozuiwa pia nayo yalifuata na msafara ukaenendelea kuwa na msururu mrefu wa magari, pikipiki, baisikeli na majaji huku watu wengine wakitembea kwa miguu.
 
Msafara huo ulipofika Mbalizi, wananchi waliuzuia tena wakitaka awasalimie na baada ya kufanya hivyo walishangilia kwa nguvu huku wengine wakiimba, ‘Rais, Rais.’
 
Kutoka na kusimamishwa kila mara, msafara ulifika Lyunga saa 9:36 ambapo pia ulisimamishwa na mamia ya wananchi ambao walijipanga barabarani karibu njia yote hasa maeneo yenye shughuli za kibiashara.
 
Wakati wote msafara ulipotoka Uwanja wa Songwe mpaka uwanja wa Ruandanzovwe, ulipofanyika mkutano, askari polisi walikuwa wakiufuata wakiwa na magari matatu ambayo yalikuwa yakitumika kutawanya wananchi ili msafara utembee haraka.
 
Mbali na magari hayo, kulikuwa vijana wa kikosi cha ulinzi cha Chadema ambao baadhi walikuwa kwenye magari mawili ya wazi huku wengine wakitembea kwa miguu kujaribu kuwatanya wananchi ili msafara huo utembee.
 
Licha ya jududi zote hizo, msafara huo uliwasili uwanjani hapo saa 10:15, ikiwa ni takribani saa tatu zilizotumika kutembea kilomita 21.
 
LOWASSA
Baada ya kukaribishwa na mgombea mwenza, Duni Haji, Lowassa alisema amefarijika kwa mapokezi makubwa na kuwashukuru wadhamini waliomdhamini katika safari yake.
 
Alisema mara ya mwisho kuja Mbeya alikuwa CCM akiomba wadhamini na kulikuwa na umati mkubwa wa wananchi uliojitokeza.
 
Alisema kutoka na umati huo, maasimu wake wa kisiasa walisema amehonga watu hao. “Sasa niulize hapa, kuna mtu amepewa hela?” alihoji Lowassa huku baadhi wananchi wakiitika “Haongwi mtu hapa.”
 
Baada ya kauli hiyo nayo Lowassa alisema “Asanteni sana, walie tu, hawatuwezi.”
 
Lowassa alisema akipata ridhaa ya kuwa Rais, ahadi yake kwa wananchi wa Mbeya ni kuufanya mkoa huo kuwa wa kibiashara.
 
“Nina ndoto na Mbeya, nataka kuugeuza Mbeya uwe mji wa kimataifa uwe kama Nairobi.Nitaanza na uwanja wa Songwe, ndege kutoka sehemu nchi jirani za Zambia na DRC zije kuanzia safari yao hapa,” alisema.
 
Kadhalika, alisema kutokana na idadi kubwa ya vijana aliyoiona; ataunda serikali rafiki kwa masikini hasa waendesha bodaboda, mama ntilie na wamachinga.
 
Kuhusu walimu, wakulima alisema ataunda serikali rafiki kwa masikini na kuwa mtu atakayanya uzembe atamuweka pembeni.
 
Alisema kwenye serikali yake, watu watafanyakazi saa 24 ili kuhakikisha uchumi unakuwa na maendeleo yanapatikana kwa haraka.
 
Alisema lengo lake la kuwania nafasi hiyo kufanyakazi na sio kufanya mchezo.
 
Hata hivyo, alisema wananchi wote wenye sifa za kupigakura wanapaswa kwenda kupigakura na kuzilinda ili wahakikishe ushindi.
 
Wananchi walipomtaka kuzungumzia suala la polisi kuzuia msafara na kuzonga wananchi, alisema polisi wengi wanakabiliwa na hali duni na wanataka mabadiliko lakini baadhi yao wanawarudisha nyuma.
 
MBOWE
Mbowe alisema wanatarajia kuwa na uchaguzi huru na wa haki, lakini akasema wanataka daftari la kudumu la wapiga kura lifanyiwe uhakiki kwa uwazi.
 
Alisema anataka iundwe tume shirikishi itakayojumuisha vyama vya upinzani ili kuona mchakato mzima wa kuhakiki daftari hilo unakuwa wa haki.
 
CHANZO: NIPASHE

Maoni 1 :

Unknown alisema ...

Mmh! Uchaguzi wa mwaka huu unaonekana utakuwa wa kihistoria. Maana upinzani unazidi kushika kasi.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom