Jumanne, Aprili 02, 2013

SIMULIZI TAMU YA KUSISIMUA..... BADO MIMI ......SURA YA ....3......



 ILIPOISHIA:
Niliondoka pale Hospitalini huku machozi yakinibubujika kwa wingi,  nilifika nyumbani nikiwa nimechoka sana lakini Baba alikuwa bado hajarudi kutoka kazini. Baada ya muda alirudi hali aliyokuwa nayo ilinishangaza kwani alionekana mtu mwenye wasiwasi  sana. Moyoni mwangu mimi nilichokuwa nakiwaza  ni je! Baba atakuwa amefanikiwa kupata hela kwa ajili ya matibabu ya Mama niliamua kumuuliza “Baba umefanikiwa kupata chochote? Kwani nimetoka hospitalini  kumpelekea Mama chakula hali ya Mama….”

INAPOENDELEA  
Kabla sijamalizia kuzungumza Baba alinikatisha “Usijali mwanangu nimepata pesa  za matibabu, kesho asubuhi na mapema tutakwenda  pamoja hospitalini” Naomba  uniwekee maji bafuni nikakoge, kwani  nimechoka sana” Moyoni mwangu nilijisikia faraja,  baada ya Baba kusema amepata pesa wa ajili ya matibabu ya Mama. Nilinyanyuka haraka na kwenda  kumuwekea Baba  maji bafuni. Wakati Baba akiwa amekwenda kuoga mimi  niliingia jikoni nikachukua chakula na kumuandalia  mezani.

  Nilikuwa najisikia amani moyoni  mwangu nilijua sasa Mama yangu atafanyiwa upasuaji, na haliyake itakuwa nzuri na mimi nitaendelea kwenda shule kama kawaida. Kwani tokea Mama alipoanza kuumwa, na kuzidiwa ghafla, nilishindwa kwenda shule. Kwasababu  kulikuwa hakuna mtu mwingine wa kumuhudumia. Baadaye Baba alikula chakula na  alikwenda  kupumzika .Usiku huo sikupata usingizi kabisa  nilitamani kupambazuke ili niwahi kwenda Hospitalini.

Nilizungumza na nafsi yangu “Mama akipona nitafurahi sana, eeh Mungu msaidie Mama apone tunamuhitaji sana, wadogo zangu wamekuwa wakilia kila kukicha kwasababu hawamuoni Mama, na mimi nashindwa kuwaeleza ukweli kuhusu hali ya Mama.Naomba umsaidie Mungu wangu” Baadaye nilipitiwa na usingizi na kulala fofofo.

Kesho yake asubuhi na mapema Baba aliamka na kuja kuniamsha tuanze safari ya kwenda hospitalini.  Niliamka na kuanza kujiandaa, nilibandika chai jikoni na kuwawekea wadogo zangu ambapo wakiamka wangekunywa chai  kwanza na kwenda shule. 

Baada ya kumaliza shughuli mbili tatu ambazo nilikuwa nazifanya sasa nilikuwa tayari  kwa kwenda Hospitalini. Baba alichukua mkoba wake na tukaanza kuondoka, kabla ya kutoka mlangoni alisikika mtu akibisha hodi, huku kukiwa na kama malumbano yanaendelea huko nje. Nilitaka kufungua mlango Baba alinikataza na kunishika mkono kwa nguvu nisifungue mlango. “Mwanangu sikiliza nikuambie, chukua huu mkoba ndani kuna kiasi cha shilingi milioni nne na nusu, Shikilia kwa umakini mwanangu. Chukua taksi  nenda hospitalini utampa Daktari milioni nne kwaajili ya matibabu  ya Mama yako.Kiasi cha pesa kitakachobakia  kitawasaidia hapa nyumbani”.


 Nilishangaa kumuona Baba katika ile hali ya kuchanganyikiwa “Lakini Baba situnaondoka pamoja mbona sikuelewi kuna nini?” Baba alinisisistiza na kunitaka niondoke haraka kwa mlango wa nyuma na yeye angefika baadaye .
Niliondoka haraka na kuelekea kupanda gari tayari kwa kuelekea hospitalini, nikiwa njiani nilijiuliza maswali mengi sana. “Wale waliokuwa wanagonga mlango ni kina nani? Mbona Baba ameonekana   kuwa na wasiwasi mwingi. Sijui kutakuwa na matatizo gani nyumbani". Nilifika hospitalini na kuelekea   chumba (wodi ya wagonjwa)alipolazwa Mama “Kandida mwanangu” Ilikuwa ni sauti ya upole  ikiniita nilimsogelea karibu na kumsalimia “Shikamoo Mama pole Mama nimekuja na hela utafanyiwa upasuaji utapona usijali Mungu atakusaidia”. Mama alikuwa akitokwa na machozi bila kuongea chochote.
 Alifika muhudumu (nesi)” Hujambo binti” niligeuka na kumsalimia “Sijambo shikamoo” Yule nesi aliniangalia huku akiwa amenikazia macho na hata nilipomsalimia hakuniitikia “Hivi wewe kwani huoni mgonjwa amejisaidia haja kubwa,  msaidie kumbadilisha nguo chumba chote kinatoa harufu kali sana na humu ndani kuna wagonjwa wengi”. Alizungumza yule nesi bila ya huruma, nilijisikia vibaya lakini sikumjibu chochote nilinyanyuka na kumsogeza Mama taratibu nilimbadilisha nguo zake.  Alikuwa hawezi kutoka pale kitandani ilinibidi nichukue maji na ndoo nakuanza kumfuta kwa kitambaa nilikuwa nalia kutokana na kumuona Mama yangu alivyokuwa anateseka”  Daktari alikuwa  akiwahudumia wagonjwa wengine kwa wakati huo.

Baadaye Daktari aliniita, nikaenda katika ofisi yake huku nikiwa nimeshilikilia ule mkoba uliokuwa na pesa za matibabu kwa umakini. “Hivi wewe mtoto si nilikuambia ukamwambie Baba yako afanye utaratibu wa pesa ili Mama yako afanyiwe upasuaji mbona umekuja peke yako?” Aliniuliza Daktari “Baba yangu anakuja yupo njiani, lakini pesa za matibabu amenipa nikuletee” Daktari alicheka kidogo “ Yaani  Baba  yako anakupa pesa  wewe! je ungevamiwa na vibaka, hajui kama ni hatari sana” Aliendelea kuongea “Amekupa kiasi gani cha pesa”? Nilijikuta nimepata nguvu ya kuzungumza “Daktari hizi hapa pesa zote zimekamilika kwaajili ya matibabu ya Mama yangu, naomba umsaidie Mama apone” “Kuna karatasi ambazo Baba yako anatakiwa kuweka sahihi kabla ya kumuingiza mgonjwa katika chumba cha upasuaji”.

 Niliwaza haraka nini cha kumjibu “Mimi nitaweka sahihi Baba atachelewa kufika kwani kuna matatizo kidogo nyumbani” Yule Daktari alikubaliana na mimi kutokana na hali ya Mama akaamua kumuandaa kwaajili ya kufanywiwa upasuaji kwa siku hiyo. Baadaye ilinibidi mimi niondoke kwani nilimsubiri kwa muda mrefu Baba bila mafanikio.

Nilipofika nyumbani niliwakuta wadogo zangu wakiwa wamekaa nje, Renata ambaye alikuwa darasa la tatu na Tumaini alikuwa darasa la kwanza. Waliponiona walinikimbilia huku wanalia “Dada Kandida,, Dada Kandida Baba , baba, baba”Alikuwa akilia Renata huku akinivuta katika gauni langu nilishindwa kuelewa Baba amepatwa na kitu gani? “Renata Baba yuko wapi? Mnalia nini? Baba amefanyaje” Nilimuuliza mdogo wangu wa kike “Baba amechukuliwa na watu, wamempiga Baba” Nini kinaendelea usikose ......sura ya .....4........

Maoni 5 :

Bila jina alisema ...

hongera sana Adela unastahili pongezi uko juu story inasisimua sana

Bila jina alisema ...

mmmmmmh jamani sijui Baba kandida kapatwa na maswaibu gani

Bila jina alisema ...

hongera Adela simulizi ni nzuri sana . uitucheleweshee nina hamu ya kujua nini kitatokea.

Bila jina alisema ...

hongera Adela simulizi ni nzuri sana . uitucheleweshee nina hamu ya kujua nini kitatokea.

Unknown alisema ...

Dah maskini usichelewe kupost basi.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom