Jumatatu, Septemba 29, 2014

SIMULIZI YA BADO MIMI SEHEMU YA 34

ILIPOISHIA
Wakati huo mchungaji alikuwa akiendelea kusali sana “Nasema utatoka tu, muachie huyu mtoto uondoke zako, sasa hivi natuma moto, ukutokomeze kabisa toka kwenda zako, huu ndiyo mwisho wako nimesema toka katika jina la Mungu Baba muumba Mbingu na Nchi. Tumaini aliendelea kutapatapa na mara ghafla alinyamaza na kutulia kimya kabisa, nilikuwa na hofu sana huku nikitetemeka lakini mchungaji James alinisihi nisiwe na hofu na kunitaka niketi, kwani kuna mambo ambayo alikuwa akitaka kuniuliza kuhusu maisha yangu. JE NINI KITAENDELEA USIKOSE SEHEMU YA  34

INAPOENDELEA
Bado nilikuwa nikimtizama  Tumaini, akiwa amelala chini kwenye zulia, huku nikiwa na wasiwasi sana, lakini mchungaji aliendelea kunisisitiza nisiwe na hofu “Usiogope Kandida Tumaini amepumzika kutokana na uchovu, wa shetani aliyekuwa ndani yake, sasa akiamka atakuwa hana tatizo kabisa kwani shetani amekwisha ondoka na sasa atakayezinduka atakuwa ni Tumaini mdogo wako,usiwe na hofu kabisa kwani Mungu ni mwema na ametenda maajabu yake.

Jambo nililokuwa  nataka kufahamu ni kuhusu maisha ya familia yenu  kwa ufupi, kwani inavyoonekana kuna mambo mengi ambayo yanahusisha nguvu kali za giza” Aliuliza mchungaji huku akinitazama, nilishusha pumzi kidogo na kuanza kumsimulia maisha yangu yote tangu  kufariki kwa wazazi wangu, pamoja na maisha niliyokuwa nikiishi na Mama Bilionea, na pia sikusita kumueleza kilichonisibu nilipoenda kwenye hekalu la Bibi Bilionea.

 Mchungaji alinisikiliza kwa umakini sana huku akiwa anatikisa kichwa akasema “Inamaana huyo Bibi bilionea aliyekuwa anatajwa wakati namuombea Tumaini wewe unamfahamu? Mungu wangu, Umeishi na nguvu za giza sikunyingi sana Kandida, sasa huyo mchungaji ambaye amekuwa akiwasaidia siku zote mlikutana naye wapi? Aliuliza mchungaji kwa masikitiko makubwa “ Mchungaji Mkombozi nilikutana naye siku niliyokuwa nakimbia pamoja na wadogo zangu kutoka katika nyumba ya Mama Bilionea, ndipo nilipoanza kupata msaada kutoka katika kanisa lake, na nikiwa katika kanisa hilo nilikutana na Charito ambaye ndiye mume wangu aliyekuwa ameongozana na Tumaini muda mfupi uliopita”.


Mchungaji alinisikiliza na baadaye alinyanyuka na kisha akamtizama Renata aliyekuwa ameketi huku amemshika Tumaini, na moja kwa moja akamuuliza “Kwanini ulikuwa unasema Mchungaji Mkombozi, pamoja na shemeji yako siyo watu wazuri, je kuna kitu chochote kibaya ulishawahi kukiona?” Renata bila ya kusita akaanza kusema “Ndiyo, Mchungaji Mkombozi alinijia kwenye ndoto akiwa ameshika kitambaa chekundu kinachovuja damu, huku akinitizama kwa hasira na kusema kuwa zamu yangu ikifika atanichukua, na ndoto hii imekuwa ikijirudia mara kwa mara, vivyo hivyo kwa shemeji Charito amekuwa akinijia na kutaka kuniua, lakini kila nikishtuka simuoni na kitu  ninachokiona ni mbwa, hali hii inanitisha sana Mchungaji kwani wakati mwingine mimi huwa naona shemeji anabadilika na kuwa kama mbwa kabisa, nimekuwa nikimueleza dada Kandida lakini aniamini  kile ninachomueleza”.

  Renata akiwa anazungumza nilimtizama  huku nikiwaza “Hivi huyu mtoto anajua anachokizungumza kweli, yaani Charito awe mbwa, na tena mchungaji Mkombozi atake kumuua mmmh sijui jamani haya ni mauzauza gani?” Haraka nilimtizama mchungaji na kusema “Hapana mchungaji hizo ni ndoto tu, kwani mimi hata sikumoja  sijawahi kumuona mume wangu akibadilika na kuwa mbwa….na pia…” 

Mchungaji alinikatisha kabla sijaendela kuzungumza na kusema “Kandida, kandida, kandidaaaaa,, fungua macho yako, mkaribishe Mungu katika maisha yako, kumbuka ndoto mara nyingi huelezea ukweli wa mambo ambayo yanaweza kutokea, ama yamekwishatokea, na siyo kila jambo ni la kupuuzia, vilevile inawezekana wewe usione chochote kwasababu tu huamini na moyo wako umefungwa, na macho yako ndiyo kabisa hayaoni mbele wala nyuma, hivyo usiseme Renata ni muongo kwani huwezi kujua ukweli bila ya kumshirikisha Mungu wetu wa kweli ambaye ni Muumba wa mbingu na nchi, ni wakati wako sasa kusali sana, huku ukichunguza kile anachokueleza mdogo wako, pia nakukaribisha kanisani uje pamoja na wadogo zako ikiwezekana mlete na mume wako, kwani njia pekee ya kuepuka nguvu za giza ni kusali tafadhali usiache kusali hata maramoja”.

Alisisitiza Mchungaji, Baada ya Muda Tumaini alishtuka huku akiwa anashangaa huku na kule alinifuata huku akisema “Dada Kandida, njaa inaniuma, naomba chakula” Mchungaji alimtizama  huku akitabasamu na kusema “Kandida ni vyema ukampa mdogo wako chakula sasa, huyu ndiye Tumaini wa kweli” Renata alikuwa akifurahi na mimi nilinyanyuka na kwenda jikoni kuchukua chakula, Baadaye mchungaji aliondoka huku akiendelea kusisitiza tusali sana.

Kwa wakati wote ule, Charito hakurudi nyumbani hadi ilipofika majira ya saa mbili za usiku ambapo alifika akiwa ameongozana na mchungaji Mkombozi, alipoingia alitukuta tukiwa tumeketi sebuleni moja kwa moja mchungaji Mkombozi alianza kuzunguka huku na kule bila ya kuketi akiwa anasema “Kandida kwanini unamjaribu Mungu wetu, nimepata taarifa zako kuwa umemleta mchungaji mwingine kuja kuwaombea hapa nyumbani, inamaana huniamini mimi? Aliuza mchungaji huku akinitizama kwa kunikazia macho, Renata kama kawaida yake alikuwa wa kwanza kujibu kabla ya mimi kuzungumza chochote “Samahani mchungaji, mimi sioni tatizo la Mchungaji James kuja kutuombea, kwani yeye pia ni mtu wa Mungu, hata na hivyo kila mtu anaruhusiwa kusali na kumuomba Mungu wakati wowote?”

 Aliuliza Kandida huku akimtizama mchungaji. Ghafla nilishangaa Charito alimsogelea Renata na kumpiga kibao katika paji la uso wake “Mjinga mkubwa wewe, nilishakueleza kuwa ujifunze kufunga bakuli lako, mtoto mdogo unajibizana na watu wakubwa kama wanalingana na wewe, kaa chini na nisikusikie ukiongea chochote” Nilishtuka sana kuona kile kitendo na wakati huu nilipata ujasiri wa kuzungumza, na sasa sikumjibu mchungaji bali niliamua kupambana na mume wangu Charito kwa kitendo chake cha kumpiga mdogo wangu Renata “Sijapenda ulichokifanya Charito, sipendi kabisa mdogo wangu anyanyasike, unawezaje kumpiga kiasi hicho, tena mimi sijaona kosa lake alichokizungumza ni kitu cha kawaida”.

 Charito alinitizama na kusema “Kumbe wewe ndiye unayemfundisha Renata tabia mbaya aliyonayo, sasa sikiliza mimi ni mume wako, kile ambacho nakiona hakipo sahihi na sipendezwi nacho lazima nikiweke sawa, huyu mtoto hana adabu ndiyo maana nimempiga, na pia usitake kujibizana na mimi wakati leo umenikera sana kuleta mtu nisiyemfahamu hapa nyumbani, huyo anayejiita mchungaji James, au ni hawara yako unaficha” Aliongea Charito kwa kujiamini nilinyamaza kimya bila kujibu chochote huku moyoni mwangu nikisema “Mungu naomba unipe ujasiri, niepukane na haya majaribu” Mchungaji Mkombozi alinigeukia tena na kusema “Nimekuuliza  swali Kandida,”.

 Nilimtizama kwa dakika chache na kisha nilimjibu “Namuamini Mungu pekee aliyejuu, mchungaji mimi naweza kusali popote alimradi Mungu wetu ni mmoja ambaye tunamtumikia kwa nguvu zote na si kwamba kwasababu nimeombewa na mchungaji James, basi nitashindwa kusali katika kanisa lako hapana, mimi naamini Mungu yupo nasi popote pale tulipo na sioni tatizo kuombewa na mchungaji James.” Mchungaji alinyamaza kimya kidogo kana kwamba kuna jambo anatafakari kisha akasema.

  “Sawa Kandida, lakini kumbuka kuwa makini, kwani unaweza kujiona upo sahihi lakini, madhara yake ni makubwa sana” Aliongea mchungaji huku akiniaga na kusema “Mimi naondoka, lakini nakusisitiza tena kuwa makini, kwani jambo ulilolifanya ni kosa kubwa sana katika kanisa letu, nakutakia usiku mwema” Aliondoka mchungaji na kutuacha. Siku hiyo Charito alikuwa amekasirika sana, niliwasindikiza wadogo zangu kwenda kulala, na mimi nikarudi chumbani kwangu kupumzika Charito alikuwa amenyamaza kimya bila ya kunisemesha kwa usiku huo.

Kwa upande wa Renata akiwa amelala usiku majira ya saa nane alimuona mchungaji akiwa ameongozana na Charito, wakiwa chumbani kwake huku wakiwa wamevalia mavazi ya rangi nyekundu, Renata aliwauliza “Mnataka nini chumbani kwangu?” Charito alicheka sana huku akimwambia “Bado wewe, Bado wewe Renata” Kwa hofu kubwa Renata alijikunyata pale kitandani na kuuliza tena “Bado Mimi, Bado mimi wapi? Kwenye nini? Aliuliza huku akitetemeka “Tumekula nyama ya Baba yako na Mama yako, pamoja na nyama ya Mtoto wa dada yako akiwa tumboni sasa ni zamu yako, Bado wewe Renata, Bado weweeeeeeeee”.

 Sauti ilizidi kupaa juu kwa ukali ikiambatana na kicheko cha cha ajabu, Renata alipata hofu zaidi na wakati huu Charito alikuwa ameshikilia kisu kilichokuwa kinatiririsha damu mithili ya maji yaliyofunguliwa bombani, alikuwa akimsogelea Renata ambaye alipiga kelele kuomba msaada “Mamaaaa nakufaaa, nisaidieni jamani nakufaaaaa Mungu wangu nisaidieeeeee mamaaaaaa” Ilikuwa ni sauti kali sana, Kandida aliisikia sauti ya Renata akiwa chumbani na alishtuka moja kwa moja alikimbilia chumbani kwa Renata.JE NINI KITAENDELEA USIKOSE SEHEMU YA 35.





Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Ooh jamani Renata

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom