Alhamisi, Septemba 25, 2014

SIMULIZI YA MAISHA "USILIE NADIA SEHEMU YA "14"


“Chris baba nimekwambia chukua maamuzi kwanza.”
“Nadia chukua nguo zako na uiache nyuma hii. Huyu ni mke wangu na kila kitu kwangu” alisema Chris kwa sauti yenye kitetemeshi, bila shaka moyo ulikuwa unamsuta!!.
Wanawake wanne na mwanaume mmoja wakawa wananipinga mimi!! Unadhani ningejiteteaje? Nilikuwa pake yangu katika hii dunia!!

Na hapo nikaulaani moyo wangu!! Moyo uliodanganyika, uliodanganywa na mwanaume. Mwandishi bado nakuambia nyie wote ni sawa unakataa, unapata chuki unataka kuondoka chumbani bila kuaga unaleta hasira kwa kuambiwa ukweli. 

Unakataa nini sasa unakataa nini nakwambia nyie wote ni walewale!! Haya ondoka, endelea na hasira hizohizo, endelea ondoka mlango upo wazi, niache nilie mwenyewe, nenda hata Desmund alienda, hata Chriss aliniacha, Danny naye aliniacha, Jadida aliniacha, mama alinikataa akanilaani, baba na ndugu zangu wote walienda na wewe nenda…nenda si nd’o ulichoamua…niache!!.....ne…ee…” hakuweza kuendelea Nadia. Maneno yake yakanichoma, sikuweza kujizuia kulia, nikamkimbilia Nadia na nikaweka uandishi pembeni nikalazimika kumuomba msamaha Nadia. Haikuwa kazi ndogo!!

NADIA alilia sana kwa sauti ya juu huku machozi yake yakiishia katika bega langu, niliendelea kumkumbatia labda ndo faraja pekee aliyokuwa anahitaji kwa wakati ule. Sikujua nini nimwambie maana alikuwa kama ananihukumu mimi pia kwani nilikuwa mwanaume pia. Mara nikajikuta nauchukia sana uanaume japo sikutamani kuzaliwa mwanamke kisha kuteseka kama Nadia.

Hatimaye Nadia alinyamaza kulia lakini hakutaka hicho kilichomkaba kooni kiishie hapo!! Aliketi akanitazama usoni!!Ama!! Alikuwa amevimba macho yake haswa!! Na yalikuwa mekundu, kama ilikuwa mara ya kwanza kumuona lazima utetereke na uhisi kuwa huenda ni mgonjwa mahututi!! “Mwandishi, nilisimama wima nikataka kutembea niondoke zangu bila kumtazama Chriss machoni lakini kizunguzungu kilinishika, nikaanguka chini kama mzigo, ule mwili uliokuwa umepigwa sana sasa nikawa nimejitonesha tena!!

Chris alinisogelea lakini nikasikia akipewa onyo kali sana kutoka kwa yule mama. Ni hapo nilipogundua kuwa Chriss alikuwa anawekwa kinyumba na yule mama nd’o maana alitakiwa kutii kila alichokuwa anaambiwa!!
“Mletee chochote kilichokuwa chake atoke humu ndani.” Sauti ya mwanamke iliamuru. Kimya kikatanda kisha nikaisikia tena ile sauti, “Hizo nguo amezinunua yeye ama umemnunulia.” Nikawa nimetega masikio nimsikie Chriss.

“Amezinunua yeye, sikuwahi kumnunulia chochote!! Naapa.” Alidanganya Chriss bila shaka alifanya vile kwa sababu ya masalia ya upendo aliokuwanao kwangu. Yule mama akasonya, Chriss akanifikishia lile begi pale chini kisha akaninong’oneza jambo Fulani.
Nikasimama tena sasa nikajikongoja nikatoka nje.
Nilipogeuka kumtazama Chriss kwa mara ya mwisho, ukungu wa machozi ulikuwa umenitanda sikuweza kujua kama alikuwa anatabasamu ama alikuwa ananisikitikia.
Lakini nilichoweza kukiona kwa uhakika, ni saa ya ukutani.
Ilikuwa saa kumi kasorobo usiku!!
Naenda wapi mimi Nadia!! Nilijiuliza sana na sikuyapata majibu, nilitarajia walau wale wanawake wenzangu watapatwa na huruma na kuniita walau nilale hadi asubuhi lakini haikuwa hivyo hakuna aliyenionea huruma hata kidogo.
Nilikuwa nimetengwa tena na dunia!! Chriss aliyekuwa kila kitu kwangu alikuwa amenisaliti. 
Naam!! Nikayafuta rasmi yale mawazo kuwa huenda mama yangu alikuwa ameifuta ile laana aliyonipa akiwa Saudi Arabia, ile laana ilikuwa inaishi bado!!
Nilikuwa nimelaaniwa!!
Kutoka pale Kariakoo ya Musoma hadi barabara ya lami hapakuwa na umbali sana, nilijikongoja taratibu hadi nikaifikia barabara huku nikiwa sijui nini cha kufanya. Na magari yalikuwa yameipumzisha lami!! Kimya kikuu!!

Hakika Chriss alikuwa ameninunulia nguo nyingi, ni kama kuna kitu fulani alikuwa akiwaza juu yangu, labda kuwa mkewe siku moja ama kuwa nami milele. Lakini sasa sikuhitaji kujua hayo. Zile nguo zikaniwia nzito sana, ukiongezea na yale maumivu makali katika mwili wangu lile begi lilikuwa adhabu!! Nikaamua kulitua chini. Nikajisogeza katika kichaka kidogo nikaliweka hapo!! Kisha nikaondoka peke yangu hadi barabara ya lami!!

Hapo sasa uoga ukaanza tena!! Uoga mkuu. Nikahofia watu wabaya wangeweza kunidhuru usiku ule. Ni hapo ndipo nikayakumbuka maneno ambayo Chriss alininong’oneza wakati akinipatia lile begi. “Kwenye zipu ya kushoto!!”…naam aliniambia juu ya zipu ya kushoto.

Nikatimua mbio huku nikichechemea kurejea kule ambapo niliacha lile begi. Dakika kadhaa nilizotoweka pale hazikuleta tofauti. Nikalikuta lipo salama, upesi nikapekua katika zipu ya kushoto. Pesa!! Nikakutana na burungutu la pesa!! Machozi ambayo sikujua kama ni ya uchungu ama furaha yakanitoka huku nikijikuta nakosa maamuzi sahihi juu ya hukumu gani alikuwa anastahili Chriss, je? Nimsamehe ama ni lipi la kufanya!! Nikaamua kumsahau Chriss huku nafsi ikisema nami kuwa Chriss alikuwa ananipenda lakini tatizo alikuwa chini ya uongozi wa mwanamke. Chris alikuwa amewekwa kinyumba!!!

Nguvu zikarejea tena, nikalitwaa lile begi, pesa nikazisunda katika kifua changu. Nikajikongoja hadi katika nyumba ya kulala wageni.
Nikapata chumba pale!!
Nikapumzika!!!

Ulikuwa usiku wa aina yake ambao hakika sikuutarajia, kutoka katika penzi mwanana na kuangukia katika ukimbizi tena.” Nadia akasita kisha akaniambia kwa upole, “Mwandishi haya maisha hayana ramani….na kama ipo basi Nadia mimi siwezi kuisoma ramani vizuri.” Akasita kisha akaendelea, “ningeweza vipi kukubali kubaki Musoma wakati nilikuwa nimetengwa tayari…ningekubali vipi huruma ya wananchi wakati niliamini kuwa huruma hizo zimeniponza na moyo wangu mwepesi umenigharimu!! Nilikuwa mjinga sana kubakia Musoma, lakini si mjinga wa mwisho labda hata Desmund naye alikuwa mjinga vilevile. Cha muhimu ninachoweza kusema kwa asilimia kadhaa kubaki kule kulinisaidia lakini kosa kubwa nililofanya ni kuhitaji huruma kutoka kwa wananchi wa ardhi ambayo ilikuwa imenisaliti. Mwisho wa jina la Nadia na kuzaliwa kwa jina la Mariam kulinisaidia kidogo, lakini afadhali yale magumu aliyoyapitia Nadia kuliko huu mkasa ambao Mariam alikumbana nao!!!” Nadia akanitazama akanikonyeza kisha akasema, “Yeah ni hivyo ule ulikuwa mwisho wa u Nadia nikabadilika kuwa Mariam. Lakini kubadilika kwa jina hakukumaanisha kuwa ule ulikuwa mwisho wa mateso yangu wala haikumaanisha mimi kuwa Mariam ilimaanisha mama Nadia ataifuta laana….laana ile ingefutika iwapo tu kama Nadia ningeuwawa. Naam asingekuwepo wa kunirithi mateso yangu. Lakini sasa ningekufa vipi iwapo kuna mtu namdai mali zangu, nife vipi wakati Desmund anaishi??” kauli za Nadia ziliniacha njia panda, nikashangaa sana maana kweli siku ya kwanza aliniambia anaitwa Mariam tulipokutana katika mazingira tatanishi, nikatambua kuwa ni mambo ya wasichana tu kupenda kudanganya majina lakini sasa nilikuwa nimelipata jibu lakini halikuwa jibu sahihi. Kivipi sasa anaitwa Mariam wakati alikuwa akiitwa Nadia??
“Kwa hiyo wewe ni Maria mama Nadia?” hatimaye nikajikuta namuuliza swali kwa mara ya kwanza kabisa tangu nianze utafiti wa kisa hiki cha aina yake.
Badala ya kunijibu aliniangalia kwa makini kama anayeisoma akili yangu. Kisha akaanza kusimulia kwa sauti ya chini.
“Ilifikia kipindi nikakimbilia vituo vya watoto yatima wakanambia kuwa hairuhusiwi na hawapokei mtu juu ya miaka kumi na nane nikakataliwa, nikakimbia huku na kule kama kichaa. Mwisho nikakimbilia katika shule ya sekondari ya wasichana Songe! Sijui unaijua??.....shule moja hivi Musoma ni ya wasichana, nikalazimika kuwa napita mchana wakati wa chakula cha mchana na majira ya jioni kuokota mabaki ya ugali na maharage wanayobakiza, mwanzoni walinishangaa lakini mwisho wakanizoea nami wakaniunganisha katika kundi maarufu kwa jina la ‘waloko’. Hayo yakawa maisha yangu!!
Naam! Nilikuwa katika kutimiza lile neno alilosema Desmund kuwa mimi ni chokoraa. Tena chokoraa mzoefu.
Nilikula mabaki na kulala popote!! Sasa nikakibariki rasmi kifo changu maana nilijua lazima nitakufa tu!! Nikaamini kuwa laana ni kitu kimoja kibaya sana, laana ya mzazi haikwepeki. Nilikonda sana na mwili kuwa kama motto mdogo, sikuwa na nywele kichwani. Hakika nilikuwa nimekongoroka!!

Nilikuwa nalia moyoni nikiwaona wasichana waliokuwa wanasoma shule ile wakitoroka na kuchukuliwa na wanaume wenye pesa zao huku wengine wakichukuliwa na wanafunzi wenzao wa shule jirani ya Musoma ufundi. Nilitamani kuwahadithia maisha yangu ili wajifunze kitu lakini ningeanzia wapi mimi!! Nikabaki kuwasikitikia tu bila kuwaambia lolote. Na maisha yakaendelea.

Nilidumu pale kwa miezi kadhaa huku nikiwa nimeizoea ile hali na hatimaye nikasahau kile kisa matata kilichonifanya mimi kupoteza ramani na kujikuta nikiangukia katika uchokoraa rasmi!! Nikiwa sina ndugu wala rafiki!!.......hatimaye ukafika ule muda wa kupata rafiki mpya aliyesababisha nibadilike kutoka katika u Nadia na kuingia katika u Mariam.”

Akasita akatwaa maji na kunywa kisha akaendelea!! “Kipindi cha mitihani hakuna asiyekijua, kipindi hicho kila mwanafunzi hutingwa na mambo yake akijaribu kujikwamua aweze kufaulu. 

Kila mtu huwa na mbinu zake za ufaulu lakini mbinu maarufu ni kuangaliziana ama kuingia na majibu katika chumba cha mitihani, siku hiyo mchana kama kawaida tulikuwa tunarandaranda huku na kule katika ile shule, tukingojea muda wa chakula cha mchana ufike. Ndipo nilipokutana na Jesca, niliwahi kuwa mwanafunzi hivyo nilijua kila kitu, Jesca hakuwa na nia ya kuja chooni lakini nia yake ilikuwa kufuata majibu aliyokuwa ameyahifadhi chooni, nilimuona alipoyahifadhi na hata alipoenda kuyachukua nilimuona pia. Lakini licha ya kumuona yeye pia kuna kitu nilikigundua, kuwa kuna mwalimu alikuwa ameyaona yale majibu na alikuwa anategea amwone aliyeyaweka, nilimtambua mwalimu Temba maana alikuwa anaogopwa sana na kuna wakati alikuwa akitugeuzia kibao hata sisi ambao aliamini tunaokota mabaki ya chakula kile kwa ajili ya bata nyumbani, hakujua mimi nilikuwa nakula chakula kile.

Yule binti alivyotoka darasani nami nikasimama ilimradi tu nipishane naye, nikajifanya namuulizia kitu, akanitazama kwa hasira kali. Bila shaka hakuvutiwa na ombi langu!! Sikutaka apige hatua mbele zaidi, “dada mwalimu Temba amekutegea ameyaona majibu yako!! Usiende!” nilimwambia na kuhakikisha amesikia kisha nikachukua hamsini zangu nay eye nikamwacha bila kumtazama tena……sikujua nini kiliendelea lakini jioni Jesca alinitafuta!! Huo ukawa mwanzo wa urafiki wetu, urafiki ulioniingiza katika jina jipya na MATESO MAPYA!!

MATESO MATAKATIFU!!! MATESO NISIYOTAKA KUYAKUMBUKA!!.....Usiku mwema Gerlad!!” Nadia alinikatisha ghafla wakati nilikuwa nimejiweka makini sasa kusikiliza ni kitu gani kilitokea.
Kukatishwa huko kukaniacha katika njia panda. Nikabaki na maswali ambayo hata ungekuwa wewe lazima ungejiuliza.

MOJA: Nadia alilala gesti siku alipofukuzwa nini kilijiri sasa?

MBILI: Nadia akabadilika kuwa MARIAM…nini chanzo.

TATU: JESCA anahusika vipi katika mkasa huu?

NNE: Nadia anadai mateso ya MARIAM ni makali kuliko haya ya NADIA…..inawezekana vipi? Na ilikuwaje?

TANO: Nini hatma ya Desmund maana Nadia hajawahi kumsamehe!!

Ni maswali hayo yaliyoniumiza kichwa lakini sikuwa na jinsi nikalazimika kumjibu Nadia, “USIKU MWEMA PIA”…kisha nikaondoka na kuufunga mlango!!!

Hakuna maoni:

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom