Jumatatu, Novemba 10, 2014

SIMULIZI YA MAISHA USILIE NADIA SEHEMU YA 22


ILIPOISHIA

 Baada ya kama robo saa akatoka mchungaji kijana, Stephano. Nikamkimbilia na kumwangukia kifuani mimi na Jonas, akaizungusha mikono yake nikalipata lile joto la upendo.

Akanikaribisha ndani sebuleni, nikaingia huku nikiwa nalia kilio cha kwikwi, akaniuliza kulikoni.  Huku akiwa ananitazama katika hali ya kutia matumaini na upendo mkuu.USIKOSE SEHEMU YA 22

 INAPOENDELEA

Ningeweza kusita kumweleza mtu yeyote yule juu ya maisha yangu lakini si mtu ambaye anaaminiwa na maelfu kama mtu wa Mungu, na alishiriki katika kuijenga imani yangu. Na alinifanya kila jumapili niione kuwa ya thamani kwa sababu tu alikuwa akiniambia maneno mazuri, Stephano alichangia kwa kiasi kikubwa kurejesha ushirikiano kati yangu na Mungu ambaye niliwahi kusema kuwa amenisahau ama anashiriki katika kunisulubu.
  
Nikamweleza historia yangu ngumu kwa ufupi sana, nikamweleza jinsi nilivyofika nyumbani kwa mzee Aswile na kisha nikagusia kiundani juu ya taarifa ya tetesi aliyonipa shamba boi juu ya hisia za mama Aswile kwangu mimi kuwa nina mahusiano na mumewe. Mchungaji akaduwaa, lakini nikafikia hadi hatua ya kumweleza kuwa nahisi mama Aswile anahusika katika kumuua mumewe.


 Hapa akaungana nami kwa hisia hiyo, akatazama juu akawa kama anayenena kwa lugha nisizozijua. Bila shaka alikuwa kiroho zaidi. Pia nikamgusia juu ya Jonas ambaye mama Aswile alidhani ni mtoto wa mume wake, hapa nikamtaja Jesca kwa mara ya kwanza baada ya muda mrefu na nikamweleza mchungaji nkuwa nina tatizo la uzazi na sijawahi kuwa na mtoto. Akanipa pole!!

“Mchungaji! Mimi nimeondoka katika familia ile kwa sababu nachukiwa, na mbaya zaidi nimefanya fujo pale nyumbani. Nipo hapa kwa kitu kimoja tu…uwezo wangu kiakili umefika mwisho, sijui nini cha kufanya na nimechanganyikiwa kabisa. Naomba unisaidie kutatua jambo hili, ni wewe pekee uliyebaki katika maisha yangu, ni wewe waweza kusema neno nami nikajiona ni mwanadamu tena. Tafadhali baba mchungaji!!” nilimsihi kwa sauti ya chini. Na hapo nikayangoja majibu yake.
“Mariam!! Bwana ni mwema na humulika taa kwa watu wake na kamwe hawatajikwaa, malaika wamewazunguka na kuwalinda kwa mabawa yao. Mungu yu pamoja nawe, haujayapita hayo yote kwa uweza wako. Sijisikii vyema sana usiku huu baada ya taarifa hii, sasa nakuomba ulale, mimi ninaingia katika maombi, na nitakesha kukuombea usiku mzima na asubuhi bwana ninayemuamini atatoa majibu.” Aliniambia huku kama kawaida akirusha mikono huku na kule kisha kunena kwa lugha za kigeni.
Mwisho akanipeleka katika chumba maalumu kwa ajili ya wageni.
“Watoto na mama yao wamesafiri nimekuwa mpweke sana, angekuwepo Suzan ungelala naye humo. Lakini hayupo sasa.” Aliniambia kwa kusihi, sikujali., nikaingia chumbani, nilitamani kuoga lakini ile baridi ikanisaliti nikaghairisha na kujitupa kitandani.
Blangeti zito likamfunika Jonas, sasa alitabasamu kidogo, kisha akapotea usingizini. Nami nikawa katika kusinzia. Lakini si hoi kama Jonas, baada ya muda kidogo nikiwa sijasinzia bado nikasikia sauti ikiniita, alikuwa ni mchungaji. Nikajifanya sisikii vyema, akaita tena bado sikuitika. Sijui kwanini sikutaka kuitika, labda ni msongamano wa mawazo kuwa mchungaji ameingiwa tamaa za kimwili ama vipi. Hatimaye akaondoka. Nami nikasinzia kweli.

Nilikuja kushtuka usingizini Jonas alikuwa analia, kilio chake kilitaka kufanana na kile cha usiku ule kisha asubuhi mzee Aswile akafariki. Nilitaka kupuuzia baada ya Jonas kusinzia tena kwani kilio kile hakikudumu. Lakini nikakumbuka kuwa mimi ni Nadia niliyelaaniwa, Nadia mwenye mwonekano wa mwanadamu lakini nikiishi kama kivuli, Nadia mwenye hofu wakati wote. Nadia asiyeaminika, Nadia asiyetakiwa kumwamini mtu.
Nikasimama na kuufungua mlango kisha nikajongea katika sebule, nikijifanya naenda kutafuta maji ya kunywa katika friji. Nikaisikia sauti ikiunguruma kwa chini chini, bila shaka katika simu. Nikaganda katika friji na sasa nikaweza kusikia maneno baadhi, lakini muongeaji akaendelea kujisahau na mwisho akawa anazungumza kwa sauti ya juu.
“Ameshasinzia nimeenda chumbani alipo nimemuita haitiki, amechoka kwakweli. Sasa sika wewe kitu cha msingi kama unafahamiana na bodaboda yeyote yule akupeleke kituoni asubuhi, si umeshachukua RB….wewe wape hela ya mafuta mje na difenda yao mtamkuta hapa…..
….wewe usijali kuhusu hilo, nitakifunga kile chumba mtamkuta kama alivyo. Tena jitahidi sana maana mambo aliyoniambia ni balaa, wewe naye ujifunze kuwa na siri mbona anajua mambo mengi hivyo, je angeenda kwa mtumishi mwingine unadhani tungeonekanaje mpenzi wangu.
……sio kama nakulaumu mamangu, mi nakwambia ukweli mpenzi. Haya hayo yaishe maana hukawii kukasirika. Wewe asubuhi sana uje umchukue halafu mimi nitamalizana na mkuu wa upelelezi afanye tunayotaka. Mbaya sana huyu binti, na niliwahi kukwambia kabisa haya mambo ya kufuga viumbe usiowafahamu ipo siku utafuga majini………(kimya akisikiliza upande wa pili)
…..kuhusu mtoto usijali hata cha msingi huyu paka kwanza. Alfajiri nakifunga chumba mtawakuta wote. Alijifanya mjuaji sana kukupigeni na kukimbia hii Mbeya yetu asingeweza, wewe nilikwambia ukajifanya kukata tamaa…..wewe saa kumi na mbili fika hapa…”

Nilibaki kama sanamu nimeganda pale katika friji. Alikuwa ni mchungaji Stephano, mtu pekee niliyekuwa namwamini kuwa atanisaidia katika tatizo hili linalonikabili, sasa anazungumza na mama Aswile, yaani mama Aswile na mchungaji kumbe ni wapenzi. Mungu wangu!! Nilipagawa, mbaya zaidi alikuwa amesisitiza kuwa asubuhi polisi wanakuja kunishika, na kuhusu Jonas watajua cha kumfanya. Nilitetemeka sana, nikaondoka kwa kunyata nikaelekea chumbani, Jonas alikuwa anapepesa macho huku na kule, na yeye alikuwa ametoka usingizini tena. Ukutani kulikuwa na saa, ilikuwa ni saa nane na dakika hamsini hivi. Sikutakiwa kulala tena, lakini ningetoka vipi katika nyumba ile.
Nadia mimi nilikuwa nimetupiwa pepo la kusalitiwa na kukataliwa, hata kiongozi wa kiroho alikuwa amenisaliti!!!! Hakika niliumia sana, na hapa nikajiona nisiyekuwa na ujanja tena.
Majira ya saa kumi na moja  chumba kile kilifungwa kwa nje.
Saa kumi na mbili kama nilivyoyasikia mazungumzo kwenye simu ndo muda ambao askari walitakiwa kufika pale kunikamata. Jonas abaki na kufanywa wanavyotaka.
Milango ya jela nikaiona ikifunguka na Nadia mimi nikitakiwa kuingia. Nikaona akina Desmund wakitabasamu huku mzee Matata na wenzake wakinicheka, Bryan alikuwa akinizomea na familia yangu nzima ikipiga makofi, hata mama yangu akiwa mmoja wao katika orodha.
Nitafanya nini nikwepe mtego huu, kumwamini mtumishi wa kiroho kumeniponza. Muda nao ukazidi kusogea dakika kwa dakika………..mwandishi umewahi kuusikia moyo wako ukiwa wa moto huku ukidunda pigo moja baada ya jingine kwa kasi isiyohesabika. Basi nilikuwa namna ile. Sikuona dalili yoyote ya kujiokoa kutoka pale. Mlango mkuu wa kutokea nje ulikuwa umefungwa na mbaya zaidi mlinzi atakuwa amezuiwa asiniruhusu kutoka nje……..nilimwomba Mungu ile laana iishie kwangu lakini sasa alikuwa kwa mara nyingine amenihukumu na kunipa kisogo, Jonas alikuwa anaishi katika laana yangu, Jonas alsiyejua hili wala lile anahangaika nami..Jonas…Jonaa….asiyeweza hata kusema neno lolote la ubaya kwa mtu anahukumiwa na wanaojitambua, walimuita mwanaharamu sasa watamuua.” akasita kuzungumza, kilio cha kwikwi kilikuwa kimelikamata koo lake. Akalia kwa kujibana bana lakini hakuweza. Alikuwa anatetemeka sana.
Nikamchukua shingo yake na kumlaza begani mwangu, akaendelea kulia.
“USILIE NADIA….machozi yako bado yana thamani sana usiyaruhusu yamwagike zaidi ya hapa Nadia, nilikuahidi tangu siku ya kwanza kuwa sitakusaliti kamwe na nitakupigania upate unachokitafuta. Niamini, na nilikwambia tukifika Dar utajua nini namaanisha….” Nilimsisitiza lakini bado alilia kwa uchungu sana.
Nikamlaza kitandanbi kwangu, nikamfunika na shuka langu, mimi nikakaa katika kochi, Nadia akiwa analia pekee katika shuka.

Katia makochi mimi nikazidi kuchanganyikiwa.

Nadia alikamatwa ama alifanikiwa kuwashawishi wakamwachia?
Kama alikamatwa ilikuwaje akaachiwa huru wakati alikuwa na siri nzito kifuani mwake?
Na Jonas mwisho wake ulikuwa upi?
Vipi kuhusu Desmund?
Vipi mkewe Desmund?? Vipi mama mzazi wa Desmund na yule mzee Matata naye vipi?
Jesca hajulikanai alipo, na yeye hatima yake vipi?

Hakika maswali yalikuwa mengi kuliko majibu…nikatamani Nadia ajue jinsi gani maswali yale yananiumiza kichwa anyanyuke na kuendelea kunijibu. Lakini Nadia hakuwa anajua hilo….akasinzia pale kitandani.


*****

Nilisinzia katika yale makochi pale bila kujitambua kama nilisinzia, nilikuja kushtuka baada ya kusikia napapaswa. Nilipofumbua macho alikuwa ni Nadia, alikuwa anatabasamu pana usoni.
“Utaibiwa wewe!!” aliniambia huku akirejea kukaa kitandani.
“Mh!! Hivi saa ngapi sasa hivi?” nilimuuliza, akanieleza kuwa tayari ilikuwa saa kumi na mbili asubuhi. Nililala kwenye kochi na yeye alilala kitandani.
“Duh mgongo unauma kweli…umenilazaa kwenye kochi we mtoto.” Nilimtania Nadia wakati huo nikijinyoosha.
Nadia alinitazama kisha akajiweka katika namna ya kuchukua egemeo ukutani. Na hapo akaanza kuzungumza.
“Walaah!! Ungekuwa wewe usingeweza kudumu hata saa zima kumbe, yaani hadi Jonas anakuzidi kumbe, yule mtoto alikuwa jasiri sana, niliamini kabisa kuwa lazima ataniumbua tu usiku ule, lakini ya Mungu mengi kwakweli Jonas alivumilia. Nilimbeba akiwa katika usingizi nikamuhamishia nyuma ya kochi kubwa katika sebule ya kifahari ya mchungaji Stephano, nikamtandikia kitambaa chepesi tu nikamlaza katika vigaye vile, bila shaka unajua jinsi gani vigaye vinakuwa na baridi kali, pale kitandani nikaacha mashuka yakiwa katika namna ya kufunika viumbe hai. Ni hilo lilikuwa jaribio langu la mwisho kabla mchungaji hajachukua uamuzi wa kukifunga kile chumba kama alivyokuwa amesema katika simu.
Hakika baada ya kutoka mle chumbani na kujificha nyuma ya kochi lile mimi na Jonas wangu nilimsikia mchungaji akinyata hadi akaufikia mlango  ule wa kitasa, akaingiza funguo kwa tahadhari bila hata kujihakikishia kama bado nilikuwa ndani ya chumba kile. Akaufunga mlango!! Baada ya hapo akampigia simu mama Aswile na kumweleza kuwa amekifunga chumba tayari.
Niliendelea kubaki nyuma ya kochi kubwa pale sebuleni huku nikiomba dua zote Jonas asije kushtuka na kuanza kulia.  Jambo ambalo kwangu mimi lilikuwa  hatari sana, na jinsi mchungaji yule alivyokuwa anazungumza kwa hasira na chuki basi angeweza kunitoa roho kama angegundua nimemchezea shere katika jambo hilo.
Niliendelea kuwa pale, Jonas alikuwa amelala lakini mimi nilikuwa nimejikunja katika namna ambayo mwanadamu wa kawaida katika mazingira ya kawaida asingeweza kudumu walau kwa nusu saa, lakini Nadia mimi kwa wakati ule sikuwa mwanadamu wa kawaida na kubwa zaidi sikuwa katika mazingira ya kawaida. Nilikuwa katika hatari na nilitakiwa kuchukua maamuzi ya haraka, maamuzi ambayo yangeniamulia kuwa aidha naendelea katika harakati zangu za kulipiza kisasi na kukomboa mali zangu kutoka kwa Desmund huku nikimfanya aione dunia chungu, ama kuzembea kidogo na kujikuta nikiishia jela ambapo nitakuwa katika machungu, labda kupita haya ya awali.
Hali hiyo ilinipa ujasiri na kuendelea kujikunja pale, sio siri mgongo ulikuwa unaniuma sana, ulichemka na kuwa wa moto, lakini kipi kingekuwa bora kwangu, aidha kuuumia kwa muda ama kuja kuteseka maisha yangu yote. Hali ilikuwa tete.
Majira ya saa kumi na mbili kwa mujibu wa saa iliyokuwa ukutani nilisikia kile ambacho Stephano alikuwa ameahidi, niliisikia gari ikisimama nje  na geti likafunguliwa. Baada ya hapo chumba cha Stephano kilifunguliwa alipofika sebuleni, nikasikia vishindo vingine.
“Mh…..nikumbatie kwanza la sivyo simtoi..” nilimsikia mchungaji akisema, kimya kikatanda, na mara wawili hao ambao niliisikia miguno ya kimahaba ikiwatoka wakaangukia katika lile kochi ambalo mimi nilikuwa nimejificha nyuma yake, kishindo cha kuliangukia lile kochi mara Jonas naye akafumbua macho, Mungu wangu!!  Nikajua kifuatacho ni kutokwa na kilio, nikaundaa mkono wangu iwapo Jonas atathubutu kutoa kilio niweze kumziba mdomo, hekaheka ziliendelea katika lile kochi bila shaka walikuwa wakibusiana, na walikuwa wamenogewa hadi pale honi ilipopigwa.
“Ndo hao uliokuja nao.” Stephano aliuliza.
“Nimekuja naye mmoja tu mbona, tumechukua teksi tu walishauri hivyo.” Alijibu mama Aswile sasa niliweza kuisikia sauti yake vizuri.
“Mpenzi yaani nd’o alikukwangua hivi?” mchungaji aliuliza.
“Mwendawazimu sana yule mtoto, namfunga maisha haki ya Mungu!!” aliapa kwa hasira, nami nikazidi kutetemeka lakini sikuhamisha macho kutoka machoni mwa Jonas. USIKOSE SEHEMU YA 23

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Jamani Nadia...

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom