Jumapili, Juni 21, 2015

SIMULIZI FUPI "MAUMIVU YA MAPENZI

Mbona unaonekuna kuwa na mawazo mengi sana vipi, una matatizo gani Jojina? Aliuliza na kuhoji, Monika  huku akimtazama Jojina ambaye alikuwa amejiinamia bila ya kusema chochote, baada ya muda kidogo Jojina alinyanyua uso wake na kumtizama Monika kisha akasema “Unajua katika maisha yangu sikuwahi kufikiria hata sikumoja , yaani hata maramoja kama  Mbuso angeweza kunifanyia hivi, siamini na pia naumia sana, halafu kwanini amenitendea yote haya mimi nilimpenda kwa moyo wangu wote nilimthamini sana  inamaana kweli yote aliona kuwa hayatoshi akaamua kuniumiza kiasi hiki, inaniuma sana, naumia Monika moyo wangu unaumia sana”.

Aliongea Jojina huku machozi yakiwa yanambubujika kwenye paji la uso wake mithili mtu aliyemwagiwa maji kichwani, na kwa wakati wote huo Monika alikuwa akimsikiliza kwa umakini sana kisha alisogea na kuketi karibu na Jojina aliyekuwa ameketi kwenye mkeka uliokuwa kibarazani  nyumbani kwake, alisogea na kuketi kisha akamshika mkono na kuuliza “Jojina, mbona sikuelewi kwani shemeji Mbuso amefanya nini?  Halafu ukiwa unalia hivi unanichanganya kuna tatizo gani? .


 Aliuliza Monika huku Jojina akiwa anajifuta machozi  alinyamaza kimya na moyoni mwake akiwa anawaza “Ama kweli dunia siyo mbaya walimwengu ndiyo wabaya, mimi nilikutana na Mbuso miaka mitatu iliyopita, na baada ya mwaka mmoja tulifunga pingu za maisha, na katika safari yetu ya maisha ya ndoa tulijitahidi sana ili tuweze kufanikiwa katika mambo mbalimbali kweye maisha, na kweli Mungu alitujalia tukafanikiwa kujenga nyumba na kupata mtoto mmoja , mwanangu Joyce ana mwaka mmoja na nusu  bado ni mdogo sana, na hata siku moja sikuwahi kufikiria kama mume wangu angekuja kuniumiza kiasi hiki tena  yaani sijui kwakweli  kama kidonda hiki kitapona” Alikuwa akiwaza moyoni mwake  Jojina bila yakuzungumza chochote  na wakati huo Monika bado alikuwa akimtizama  kwa uso uliojaa maswali mengi ambapo alikuwa akisubiri Jojina amweleze ana matatizo gani.


 Moja kwa moja Jojina alishusha pumzi kisha akamtizama Monika na kusema  “Usijali rafiki yangu, mimi nitakuwa sawa , wewe nenda, naomba uniache kwasasa kwani siwezi kukueleza chochote” Aliongea  kwa sauti ya unyonge huku akimtizama Monika ambaye  bado alikuwa anataka kujua nini kimemsibu rafiki yake baada ya kumbembeleza sana ndipo Jojina alipoamua kusema “Unajua Monika wewe ni rafiki yangu ambaye nakuona zaidi ya rafiki kwani wewe ni  kama ndugu yangu kutokana na urafiki tulionao, mimi nina matatizo katika ndoa yangu mume wangu amebadilika sana imefikia kipindi ananiambia anataka tutengane kwani amenichoka, na pia anasema moyo wake unamuhijati mwanamke mwingine eti leo hii mimi Mbuso ananiambia sina vigezo ambavyo alikuwa anavitaka kwa mwanamke, hivyo anataka tutengane, yaani mwanzoni nilifikiri ni utani, lakini kumbe ni kweli sasa ameondoka na kuniacha mimi na mwanangu nilijitahidi sana kumbembeleza lakini alinijibu hawezi kuishi na mwanamke ambaye hana mapenzi naye, na tena kama haitoshi anasema akiniona anasikia kichefuchefu, kweli leo hii Mbuso ni wa kuniona mimi kama takataka, nilimpenda sana siamini mimi kama yote haya yametokea nipo kama nimechanganyikiwa inauma jamani yaani naumia Monika”

 Alikuwa akizungumza  Jojina huku machozi yakiwa yanamlengalenga, Monika alinyamaza kimya kidogo kisha akasema “Pole sana rafiki yangu , unajua mapenzi yanachangamoto nyingi sana, lakini mimi nikushauri kitu kimoja  usiwaze sana kwani utajiumiza , mshukuru Mungu huyo Mbuso ameondoka angalau amekuachia nyumba yako, na wewe unafanya kazi hivyo utaweza kujikimu kimaisha yaani familia yako haitatetereka na kingine kwanini umlilie mtu ambaye hana mapenzi na wewe, Jojina rafiki yangu  usijiumize kichwa  wewe fikiria maisha mapya na mtoto wako” Aliongea Monika huku akimtizama Jojina kwa kumkazia macho  na wakati wote huo Jojina alikuwa akimsikiliza kwa umakini kisha akasema  “Unajua ni vigumu sana kuamini yote haya yametokea na pia nampenda sana mume wangu hivyo ukiniambia niwaze maisha yangu mapya ni kitu kigumu sana kwangu hakuna mtu ambaye anapenda  familia yake itengane, yaani naumia sana”.

 Aliendelea kuzungumza Jojina kwa uchungu huku  akimtizama Monika ambaye aliguna kidogo kisha akasema “Unanishangaza sana rafiki yangu kumbuka maji ya kisha mwagika hayazoleki, na pia mpende akupendaye asiyekupenda achana naye, sasa wewe unataka kulazimisha mambo yasiyowezekana , usiwe mjinga kiasi hicho rafiki yangu, Mbuso ameshakuacha tena amekutamkia wazi kuwa hakupendi sasa wewe unacholazimisha  ni kitu gani? Achana naye endelea na maisha yako huo ndiyo ushauri wangu wa mwisho” 

 Aliongea  Monika kwa msisitizo.  Waliendelea  na mazungumzo lakini baadaye Monika aliamua kuaga na kuondoka huku akimuacha Jojina akiwa mwingi wa mawazo “Huyu Monika, anafikiri haya mambo ni madogo sana, yalaiti ingelikuwa ni yeye sizani kama angeweza kuvumila, unajua maumivu ya kitu chochote anayajua muhusika yaliyomkuta lakini kwa Yule ambaye hayajamtokea hawezi kuona maumivu, mimi hili jambo limeniumiza sana na siwezi kujidanganya kuwa sijaumia Mungu naomba unisimamie”

 Aliwaza Jojina na baadaye aliingia ndani kwenda kupumzika, ilipita kama wiki moja mume wake hakurudi kabisa nyumbani na hata alipomtafuta kwenye simu haikupatikana hewani, kilasiku alikuwa ni mtu mwenye mawazo mengi sana baadaye alifikiria ni namna gani anaweza kufanya ili aweze kuondokana na mawazo aliyonayo “Mimi sijui nifanyeje , ama kweli Mbuso hanipendi tena na sasa nahisi hata namba yake ya simu amebadilisha, ni wazi kuwa hataki kuniona tena na mimi bado naendelea kumuwaza sana, ila nikiendelea hivi nitaumia zaidi ni bora nijaribu kumsahau kabisa  kama Monika alivyonishauri, na sasa nimfikie mtoto wangu pekee”.

 Alikuwa akiwaza Jojina na baadaye aliamua kwenda nyumbani kwa Monika ili kumjulia hali na kumueleza kile alichoamua kukifanya, alipofika nyumbani kwa Monika alimkuta dada mwingine mgeni ambaye alijitambulisha kwa jina la Salima, walisalimiana na kisha alimuomba akamwite Monika,  ambapo Yule dada alimtizama na kusema “Samahani dada  mimi ni mpangaji katika nyumba hii kwasasa Monika  amehama hapa kama wiki moja imepita ila naweza kukuelekeza anapoishi”.

 Nilishangaa sana kusikia kuwa Monika amehama tena bila ya kunipa taarifa ila Yule dada alinielekeza na moja kwa moja nilienda nyumbani kwa Monika nilipofika tu Monika alinikaribisha ndani vizuri, ilikuwa ni nyumba kubwa nzuri na ya kifahari  tulisalimiana kisha nikamuuliza “Mwenzangu mbona umehama  bila ya kunipa taarifa, mimi nimetoka kwenye nyumba ile ya zamani nikijua bado upo pale” Monika alimtizama kisha akasema “Hivi Jojina kwani ni lazima mtu ukihama utoe taarifa, siyo kila jambo ni la kusema mambo mengine tunafanya kimya kimya”

Aliongea huku akimtizama Jojina ambaye alikuwa akipepesa macho huku na kule ghafla aliona picha ya Mbuso akiwa na Monika imebandikwa ukutani, alishtuka na kusema “Hivi ni macho yangu au naona vibaya, huyu si Mbuso, eeh wewe Monika, mbona sielewi halafu….” Kabla hajamaliza kuongea Mbuso alikuwa ametoka chumbani akamuona na kusema “Wewe mwanamke kinachokushangaza hapo ni nini, hivi mbona unapenda kunifuatafuata nilishakuambia sikutaki sasa naona umeamua kuja kunivuruga katika maisha yangu mapya”.

 Aliongea Mbuso huku Monika akiwa ameketi na kutabasamu, na kwa wakati huo Jojina alikuwa amebaki ameduwaa huku akisema “Ama kweli kikulacho ki nguoni mwako, na rafiki yako ndiyo adui yako, kweli wewe Monika ndiyo chanzo  cha kila kitu wewe umeamua kuingilia ndoa yangu, siamini mimi jamani, rafiki yangu niliyekuwa namuona kama ndugu kumbe unanichekea usoni, moyoni ulikuwa umepanga kuniangamiza, leo hii umeamua kuishi na mume wangu tena unafurahi kuwa nimeachika, siamini ninachokiona wewe unaroho mbaya tena unaweza kumuuwa mtu, yaani sijui, kweli ,,ah, aah” 

Aliongea Jojina kwa uchungu sana lakini Monika hakujali kitu alibaki akitabasamu kwa dharau na kusema  “Sikiliza nikuambie Jojina, ndiyo maana nilikuambia mpende akupendaye asiyekupenda achana naye, Mbuso na mimi tunapendana hivyo wewe tafuta atakayekupenda mapenzi  hayalazimishwi” Aliongea Monika bila hata ya huruma huku Mbuso akimfukuza Jojina “Naomba uondoke na kamwe usirudi hapa, nimesema sikutaki, kama nilikupenda ilikuwa zamani, tena nahisi ilikuwa bahati mbaya mimi siwezi kuwa na mwanamke kama wewe” Aliongea kwa msisitizo na kuacha Jojina akitoka nje huku akiwa ameishiwa nguvu na machozi yakimbubujika “Asanteni sana kwa yote mliyonitendea  leo kwangu kesho kwako Mungu yupo atanisimamia, asanteni sana ama kweli ubinadamu kazi sikuwahi kufikiria kama ningekuja  kuumia kiasi hiki”.

 Aliondoka Jojina na kurudi nyumbani alilia sana, kila kukicha alikuwa mwenye mawazo mengi  baadhi ya watu walimcheka na wengine walimpa matumaini ya kuendelea na maisha mapya, ambapo baadaye aliamua kusahau yote yaliyotokea na kufanya kazi kwa bidii huku akimlea mtoto wake peke yake maumivu ya mapenzi yalimfanya aogope kupenda tena siku zote aliishi kwa kumuomba sana Mungu hata ikitokea akapenda tena basi awe ni mwanamume sahihi katika maisha yake.WADAU MAONI YENU NDIYO YATAKAYONIFANYA NIENDELEE KUWALETEA SIMULIZI MBALIMBALI

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Hii hadithi ina mafundisho na mtiririko mzuri. Kwa kweli nitapenda kuona kitakachoendelea.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom