Jumapili, Julai 19, 2015

ISOME KWA UMAKINI WASEMAVYO WASOMI "Uchambuzi: Kuondolewa Lowassa ndio mwanzo wa siasa za Ukabila/Ukanda Tanzania


Mwalimu Nyerere alisema " Ukimchana Mtanzania kidogo tu utapata damu ya ukabila na udini ipo karibu sana." Mwl alikuwa sahihi maana umoja wetu uliletwa na kitu kimoja tu, nacho ni "Siasa Safi." Kwa majirani zetu wa Kenya ambao ukabila umeshamiri, mkoloni hakuacha ukabila. Odinga Snr ndie alikuwa awe Waziri Mkuu wakati huo kenyatta akiwa kizuizini lakini akakataa na akasema wazi kuwa lazima Kenyatta aachiwe na yeye atakuwa Makamu wake. 

Kungekuwa na ukabila asingeacha kukamata madaraka na kumfunika Kenyatta. Baadae kukaanza siasa chafu za " Jaluo hawezi kuwa Rais." Kilichotokea ni Wajaluo kuhujumiwa na kutengwa na mwishowe walivyoona wanaonewa kana kwamba si wakenya kamili wakaanza kujenga umoja kwa ajili ya kushinikiza maslahi yao na kujilinda pia. Hii dhana ikaenea kwa makabila mengine na ndio Kenya tunayoiona leo.


Hapa Tanzania, huko nyuma zilitolewa kauli za baadhi ya wana CCM kuwa Rais wa Tanzania hawezi kutoka Kaskazini. Sijui kwamba Kaskazini si watanzania au wamefanya dhambi gani. Kwa masikitiko kabisa chama hakikutoa kauli rasmi kukanusha au kuipinga kauli hii.

Yaliyotokea Dodoma tumeyaona. Kwa ufupi kabisa ukiisoma Katiba ya CCM inasema kikao cha mwanzo cha kuchuja majina ya wagombea urais ni Kamati Kuu. Na moja ya kazi za Kamati Kuu kwa mujibu wa Ibara ya 109 (6)(b) ni kufikiria na kutoa mapendekezo yake kwa H/K majina ya wanachama wasiozidi 5 kwa nafasi ya mgombea urais. Kwa makusudi kabisa K/K ilinyang'anywa mamlaka yake ya kikatiba ya kufikiria.... Kamati Kuu ingefikiriaje kama haikupelekewa baadhi ya majina?

Chama cha Mapinduzi kina haki ya kumkataa mtu asigombee. Lakini lazima zitolewe sababu za kukata jina la mtu lakini pia jina linapaswa kukatwa na kikao chenye mamlaka ya kikatiba ya kufanya hivyo. Hatuwezi kujenga umoja wa nchi kwa kuishi kwa hisia kwamba mtu fulani ni fisadi wakati hajawahi kuambiwa rasmi kuwa yeye ni fisadi ili ajipime kama bado anaweza kugombea urais kwa tiketi ya CCM. Mwalimu Nyerere alivyompinga Malecela aliuelezea umma udhaifu wa Malecela na akamwandikia hadi kitabu kueleza kwanini Malecela hafai. 

Malecela hakuondolewa kwa hila bali alitakiwa ajipime na aone kama kweli anaweza kupeperusha bendera ya CCM pamoja na udhaifu wake. Malecela baada ya kujipima aliamua kujiondoa mweyewe kwanye mbio za urais. Je, unadhani Malecela angeondolewa kwa hila bila kuambiwa kwa uwazi madhambi yake angeridhika?

Tumekuwa tunasikia kwa chinichini kuwa Lowassa ni fisadi. Kwa miaka nane ya umbea hakuna kiongozi wa juu wa CCM aliyetoka hadharani akataja ufisadi wa Lowassa upo wapi. Hakuna aliyesema Lowassa ameiba kiasi gani. Hatukuambiwa kama Lowassa ni mwizi kwanini asipelekwe mahakamani kama wengine. Tumebaki tunabweka kama mazuzu kwamba fulani fisadi bila hata kusema hasa ufisadi wake ni nini. Kujiuzulu pekee hakutoshi kusema mtu ni fisadi maana hata Mzee Mwinyi alijiuzulu kwa kuwajibika na baadae aliteuliwa kugombea urais.

 Na ukihesabu utakuta mawaziri waliojiuzulu Tanzania ni wengi ila kwa sababu ambazo hazieleweki Lowassa ndie amekuwa "victim" wa siasa za kuchafuana. Kama nilimwelewa alisema kwa vile nchi ilikuwa gizani ilikuwa lazima hatua za haraka zichukuliwe kutafuta umeme na hivyo utaratibu wa kawaida wa tender ambao ungechukua muda mrefu usingeweza kufanyika katika hali ya dharura. Lakini pia alisema wenzake serikalini waliambiwa na hivyo hakufanya kwa siri. Mwisho wa siku hatukuambiwa aerikali ilipata hasara ya shilingi ngapi kwa maamuzi yaliyofanywa.


Kwa maoni yangu CCM imefanya makosa makubwa ambayo yanaweza kuigharimu nchi kwa kumwondoa Lowassa kwa hila. Wangemweleza makosa yake na akaambiwa ajipime na akaondoka huku akijua makosa yake na watanzania wakaambiwa ukweli ulivyo, asingepata nafasi ya kulalamika. Kwa vita aliyopigwa ikiambatana na kuvunja katiba ili kuhakikisha anaondolewa inaimarisha hoja ya "Rais hatatoka Kaskazini" maana watu wameanza kujenga hisia hizo kwamba kwa vile hatukuelezwa makosa ya EL huenda aliondolewa kwa ukaskazini wake. Huwezi kuwakataza watu kufikiri hivyo isipokuwa pale watakapopata majibu ya kutosha.

Madhara yake ni nini? Watu wa kaskazini wata fight back kuwa tunaonewa na matokeo yake zitaanza taratibu kujengeka siasa ya ukanda huku zikinyemelewa na udini. Yaliyotokea Monduli si ya kupuuza hata kidogo. Nini kifanyike? CCM itoke hadharani iwaombe radhi wanachama wake kwa ukiukwaji mkubwa wa katiba na kanuni za chama. Pili, itueleze bila kumung'unya maneno, tatizo la kimaadili analoshutumiwa nalo Lowassa ni lipi. Baada ya hapo yeye atapata nafasi ya kujitetea lakini angalao yeye na watanzania wengine wataridhika na kuendelea na siasa za umoja.

 Tukiendeleza vijembe badala ya kutatua tatizo kwa uwazi na ukweli nchi itatumbukia kwenye siasa mbaya za ukanda ambazo zitatuathiri wote. Nasisitiza, hapa hakuna uchama. Wale wanaoonewa watasahau vyama vyao watajikuta wapo kwenye chama fulani kwa convenience tu ili wapiganie maslahi yao kwa pamoja. Haya ni maoni yangu tu wala hayana uhusiano na siasa za vyama.
OK. Na Dk. Onesmo Kyauke mhadhiri kutoka chuo Kikuu cha Dar es salaam.

Maoni 1 :

Mbele alisema ...

Masuali anayouliza mwandishi na dukuduku zake ni muhimu. Mimi si mwanachama wa chama chochote cha siasa, bali naafiki kauli kwamba vyama vifuate taratibu na katiba zao kikamilifu. Hata hivi, kama CCM wanahujumiana, ni tatizo lao, si tatizo la nchi. Ingawa CCM wenyewe wanajiona sana, ni muhimu wakumbushwe kwamba CCM sio nchi na nchi sio CCM.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom