Jumanne, Septemba 30, 2014

SIMULIZI YA MAISHA "USILIE NADIA SEHEMU YA 15"

Ndipo nilipokutana na Jesca, niliwahi kuwa mwanafunzi hivyo nilijua kila kitu, Jesca hakuwa na nia ya kuja chooni lakini nia yake ilikuwa kufuata majibu aliyokuwa ameyahifadhi chooni, nilimuona alipoyahifadhi na hata alipoenda kuyachukua nilimuona pia. Lakini licha ya kumuona yeye pia kuna kitu nilikigundua, kuwa kuna mwalimu alikuwa ameyaona yale majibu na alikuwa anategea amwone aliyeyaweka, nilimtambua mwalimu Temba maana alikuwa anaogopwa sana na kuna wakati alikuwa akitugeuzia kibao hata sisi ambao aliamini tunaokota mabaki ya chakula kile kwa ajili ya bata nyumbani, hakujua mimi nilikuwa nakula chakula kile.

Yule binti alivyotoka darasani nami nikasimama ilimradi tu nipishane naye, nikajifanya namuulizia kitu, akanitazama kwa hasira kali. Bila shaka hakuvutiwa na ombi langu!! Sikutaka apige hatua mbele zaidi, “dada mwalimu Temba amekutegea ameyaona majibu yako!! Usiende!” nilimwambia na kuhakikisha amesikia kisha nikachukua hamsini zangu nay eye nikamwacha bila kumtazama tena……sikujua nini kiliendelea lakini jioni Jesca alinitafuta!! Huo ukawa mwanzo wa urafiki wetu, urafiki ulioniingiza katika jina jipya na MATESO MAPYA!!
MATESO MATAKATIFU!!!”

USIKU ulikuwa mrefu sana nikijiuliza ni nini kilimsibu Nadia hadi kufikia hatua ya kuitwa Mariam. Hakika nilijaribu kuumiza kichwa lakini hata kubabia nini kimemsibu nilishindwa. Nikatwaa dawa za maumivu na kujidunga kisha nijilaza kitandani na kupitiwa na usingizi.

Asubuhi niliwahi sana kuamka nikajiandaa kisha nikaenda chumbani kwa Nadia, siku hii niliamua kumfuata katika namna ya kuanzia pale tulipoishia usiku uliopita, niliamua kukiuka kila ambacho nilikuwa nimejipangia katika kuandaa maandiko haya kutoka katika maisha ya Nadia.
Nilifika na kugonga mlango ukafunguliwa, Nadia alikuwa amechanuka na tabasamu jepesi usoni. 

Nikamjulia hali, naye kanijulia hali yangu!!
Nikaketi, kisha nikanyanyua mkonga wa simu na kuwapigia wahusika wa hoteli ile tayari kwa kutuandalia kifungua kinywa.
“Nimewaambia tayari kama ni chai au kuna jingine.” Alinikatisha baada ya kuigundua nia yangu.
Nikamtazama akanikonyeza!!
“Silali fofofo kama wewe….”aliniambia na hapo mlango ukagongwa akaenda kufungua.
Kwa mara nyingine tena ilikuwa ni kapuchino!!
Vikombe viwili!! Sijui alijuaje kama nami ningefika kwa wakati.
Kila mmoja akatwaa kikombe chake!! Kimya kikatanda wakati tukifungua kinywa!!

Nadia alipoona kimya kimetanda sana alichukua rimoti na kuwasha luninga. Akakutana na muziki akaacha katika chaneli hiyohiyo. Mara muziki ukamalizika kikafuata kipindi kingine, Nadia hakujishughulisha kubadili chaneli badala yake akatabasamu akitazama ile luninga nami nikatazama nini kinamfanya atabasamu!!

Kilikuwa ni kipindi cha kawaida tu!! Basi nikajiongeza kuwa alikuwa na lake la ziada. Mara akatua kikombe chini akanitazama. “Hivi na wewe umewahi kuingia studio?” aliniuliza. Nami nikakitua kikombe changu chini. Kisha kwa kujiamini kabisa nikamjibu, “Yaani mwandishi mzima kama mimi hadi leo niwe sijaingia studio?”

“Umenijibu ama umeniuliza swali?” aliniambia, mara tukajikuta tumecheka wote kwa pamoja. “Nimewahi kuingia mara kwa mara Nadia.” Nilijirekebisha hatimaye. “Mwenzangu, yaani namuangalia huyu mdada hapa hajiamini kabisa sijui ni mara yake ya kwanza kuingia studio huyu?...maana dah! Mi mwenyewe mara ya kwanza kuingia studio nilikuwa natetemeka kweli, yaani studio bwana haijalishi wewe una degree wala nini yaani unaweza kuaibika. Mara ya kwanza niliingia katika studio ya redio moja hapo Musoma inaitwa Victoria FM ebwana wee mimi nilimwambia Jesca ukweli kuwa sijawahi kuingia studio, akalazimisha kweli hadi tukaenda, sema hakuwa na nia mbaya, aliamua kunisaidia kutokana na ukarimu wangu kwake. 

Maana aliniapia kuwa laity kama angekamatwa anaangalizia kwenye ule mtihani angewekewa sifuri kisha angefukuzwa shule na kutakiwa kurudi na mzazi wake shuleni baada ya adhabu atakayokuwa amepewa kumalizika. Ni katika maongezi hayo Jesca akanieleza kuwa anasomeshwa na mjomba wake na ni mkali sana huku shangazi yake akiwa hampendi hata kidogo. Jesca akataka kujua kidogo kuhusu mimi pia, hakuamini hata kidogo kuwa nimemaliza chuo kikuu, akajiroga na kuanza kuzungumza nami kiingereza hapo nikampoteza vibaya. Yaani alipotea kweli maana alikuwa na kiingereza cha kuungaunga huku mimi nikiifurahia lugha ile.”

 Hapa Nafia akasita kisha akatabasamu, bila shaka aklifurahia sana kumbukumbu ile. Kisha akaendelea, “nilimweleza mengi sana kuhusiana na masomo, naam Jesca akaniona mimi kuwa wa muhimu kwake, akaniunganisha kwa rafiki yake mtaani nikaanza kuishi hapo huku akinipatia shilingi kama elfu kumi na tano hivi na vifaa kadha wa kadha nikaanza kuuza mihogo ya kukaanga. Hakika lilikuwa jambo jema, nilikuwa makini sana na yule niliyeishi naye pia nilikuwa makini nisiropoke lolote zito kwa Jesca asije kuwa kama waliotangulia, waliishia kunijua tu lakini mwisho wakanitenda. 

Nilivuta subira hadi nilipomzoea kisha nikamwamini Jesca ndipo nikaanza kumshirikisha mambo yangu, na nilifanya hivyo kwa sababu tu alikuwa mtu wa kutafiti sana, alikuwa akiniuliza maswali mengi na mara nyingine ni kama alikuwa akinirudisha darasani kwani aliniomba nimsaidie mambo kadha wa kadha, nilipoweza nikasaidia na niliposhindwa nikamweleza. Jesca akawa rafiki mwema!!

Swali lake gumu nililoshindwa kulijibu ni moja tu!! Kwanini nipo hivyo wakati nimesoma hadi chuo kikuu??
Nilipomjibu kuwa baba yangu alichoma vyeti vyangu na sasa sikuwa na ushahidi wowote wa elimu yangu likazaliwa swali jingine la kwanini ilikuwa hivyo nikamweleza tena sababu moja baada ya nyingine, na hatimaye nikajikuta nimemweleza juu ya Desmund!!
Simulizi ya maisha yangu ikambamba na kumliza Jesca, akaamua kutafuta namna ya kunisaidia na mwisho akakutana na Abraham Swea, mtangazaji wa redio Victoria katika vipindi mbalimbali kimojawapo kikiwemo MAPITO.
Siku moja Jesca akanieleza kuwa Abraham alikuwa akihitaji kufanya kipindi na mimi. Kipindi ambacho kitaniwezesha kupata msaada wowote ule kwani yeye Jesca alikuwa anakaribia kumaliza shule hivyo lazima ningeteseka sana. Hakika alikuwa amesema jambo la maana, nikakubaliana naye lakini nikamweleza kuwa jina la Nadia ni jina chafu tayari linaweza kuniingiza matatani. Sipo tayari kulitumia na watu walifahamu!! Sikutaka kumweleza kiundani juu ya kesi ya mauaji niliyoamini kuwa inanikabili. Lakini alinielewa, akazungusha kichwa huku na kule na mara akaanguka na jina ‘MARIAM’ akaniambia kuwa nitumie jina la hilo badala ya Nadia.

“Ni jina la marehemu mama yangu!! Nilimpenda sana, japo sikuwahi kumwona na siiikumbuki sura yake lakini niliambiwa na jamaa zake kuwa nililia siku tatu mfululizo baada ya kufariki kwake.” Jesca alinipa sababu ya kulitumia jina lile. Kwa sababu zake zile sikuweza kumpinga. Nikakubali kuwa Mariam.

Siku mbili baadaye nikaingia studio kwa mara ya kwanza, katika kipindi cha mapito. Kipindi ambacho kiliibadilisha tena historia ya maisha yangu. Nilijieleza kwa umakini sana huku nikikwepa kulitaja jina la Desmund, nikayaelezea magumu niliyopitiakatika jiji la Mwanza nikamtaja Jadida kama dada yangu wa kuzaliwa, nikasimulia juu ya utata wa Musoma vijijini nilipotaka kubakwa na akina Mwita. Hata kabla sijamaliza kusimulia Abraham alikuwa anatokwa na machozi, waliopiga simu wote walikuwa wanalia. Hapo sasa nikagundua kuwa mambo ambayo nilikuwa nimeyapitia hakutakiwa kuyapitia mwanadamu wa kawaida. Huenda Nadia mimi sikuwa wa kawaida!!!

Nilipata misaada mbalimbali, lakini msaada moja mkubwa ulikuwa ni kazi! Mzee mmoja alipiga simu akajitambulisha kama mzee Matata, alikuwa ananingoja nitoke studio aweze kuonana nami aangalie uwezekano wa kunipa ajira baada ya usaili. Maana nilisema kuwa eleimu yangu ni ya chuo kikuu lakini vyeti vyangu viliungua katika ajali ya moto ambayo iliondoka na uhai wa wazazi wangu wote wawili. Mzee Matata akawa ameguswa.
Nikiwa palepale studio nilipata msaada wa takribani shilingi laki moja. Jambo jema kabisa. 
Nilipotoka nje nilimkuta Jesca akiwa analia kwa furaha na huzuni, alikuwa kikifuatilia kipindi kile moja kwa moja katika redio ndogo aliyokuwa amekuja nayo.
Wakati nazungumza na Jesca, ndipo nikaitwa katika gari moja ya kifahari kiasi. Aliyeniita alikuwa mzee Matata. Alikuwa na sura iliyojaa majonzi tele! Akajitambulisha nami nikajitambulisha, mara akafika Abraham tukaungana katika maongezi, maongezi juu ya ajira. Baada ya mazungumzo akanipatia namba zake za simu, akanisihi nimpigie simu siku inayofuata.

Siku iliyofuata nikafanya kama alivyoagiza, akanielekeza ofisi yake ilipokuwa, maeneo ya Mwisenge nje kidogo ya mji wa Musoma. Ilikuwa ofisi iliyojishughulisha na mambo ya usafirishaji, nikawekwa kama mwanafunzi wa majuma mawili nikawa mwepesi wa kuelewa na baada ya hapo nikahamishiwa katika ofisi zilizokuwa maeneo ya Nyasho!!
Huku nikaanza kufanya kazi, huku kila siku nikiamini kuwa kuna jambo sijalitimiza. Nilikuwa nadaiwa suala la kumkomoa Desmund!! Nikaliweka kiporo hili huku kila siku nikiombea nisikutane naye, yeye wala mkewe.

Ilikuwa kazi nzuri iliyonilipa vyema, mkurugenzi alinipatia chumba katika nyumba yake, huko nikawa naishi na msichana wake wa kazi. Yeye alikuwa akiishi nyumba kubwa pamoja na familia yake. Nilichezwa machale tangu mwanzo kuwa nikianza kula vizuri tu nitapendeza, na hapo matatizo yataanza tena. Naam ukafikia ule wakati wa Nadia ambaye wakati huo niliitwa Mariam kuanza kuumiza akili yangu.
Bosi alikuwa akinitaka kimapenzi!

Haya yalianza baada ya kuniandalia safari ya kikazi kwenda Mwanza kwa ajili ya kuwafundisha kazi katika ofisi ya usafirishaji jijini huko. Akanipangia hoteli nzuri, na baada ya siku mbili alifika usiku kunijulia hali. Kwa sababu alikuwa mtu mzima sana mimi nilimkaribisha chumbani kwangu. Huko akapata nafasi ya kunitamkia kuwa alihitaji kunioa.
Nilipepesa macho huku na kule na kutamani atoweke mbele yangu, lakini alikuwa akingoja jibu langu.
Nikamtazama na bila kusita NIKAMKATAA!!

Hakuniaga akaondoka kisha akanitumia ujumbe kuwa nifikirie mara mbili!! Lakini sikuwa na haja ya kufikiria mara mbili wala kuhoji juu ya familia yake italichukuliaje jambo hilo, nilikuwa nimesimamia hapo hapo kuwa SIMTAKI!!!
Hilo lilikuwa kosa klililonitupa katika kinywa kingine kisichokuwa na huruma!!
Lakini labda kosa hilo lilikuwa dogo sana, nikafanya dhambi kwake nikamweleza mfanyakazi mwenzangu juu ya jambo hilo, sidhani kama nilifanya jambo sahihi.
Juma moja baadaye akanitumia ujumbe “NASIKIA UMEWATANGAZIA WATU KUWA UMENIKATAA”….Nikajua yule mfanyakazi mwenzangu amewasambazia watu wengine jambo hilo, ni mimi nilitakiwa kujilaumu.
Nilimpigia simu Jesca na kumweleza kila kitu, akanitoa hofu na kunambia kuwa mzee yule ni mtu wa watu sana na anaheshimika kutokana na moyo wake wa kujitolea, hawezi kunifanyia jambo lolote baya kitu cha msingi nilitakiwa kumwomba msamaha!!!
Msamaha?? Nikajiuliza, msamaha kwa lipi sasa, yaani amenitongoza nimemkataa nimwombe msamaha looh!….nikaamua kupuuzia. Huku nikimdangaya Jesca kuwa nitamuomba msamaha mzee Matata. 
Ni heri ningejifanya mjinga nimwombe msamaha kuliko ukaidi nilioufanya!!!!

Usiku wa siku hiyo nikavamiwa pale chumbani, sikuchukua dakika nikakutana na giza nene!! Bila shaka waliniwekea madawa wanayojua wao!!
Nilipokuja kufumbua macho nikajikuta katika chumba kikubwa sana na sikuwa peke yangu, tulikuwa wengi lakini ni mimi pekee nilikuwa na afya tele. Wenzangu walikuwa wamekonda na walikuwa uchi wa mnyama, hawakuwa wakijiweza hata kidogo japo macho yao wengine yalikuwa wazi na wengine walikuwa wamesinzia. Hakuna aliyejishughulisha na mimi, chumba kilikuwa kina mwanga lakini ni kama hawakuwa wakiona lolote.
Nilipogeuka kushoto nikakutana na kikaratasi.

“WAULIZE WENZAKO NINI KILIWASIBU…KISHA UJIANDAE NA WEWE”
Mwandishi nilichanganyikiwa ujue yaani muda mfupi uliopita nilikuwa katika chumba cha hoteli jijini Mwanza, sasa nipo katika chumba cha ajabu sana na watu nisowafahamu tena wakiwa katika hali ya utatanishi! Uchi wa mnyama!!, nilichanganyikiwa sana. Nikasimama niweze kutafuta pa kutokea, nikajikuta nimekanyanga mkono wa mtu, sijui ulivunjika ule!! Alilia sana..alilia na hakuwa na la kufanya, kama alidhani kuwa alinipiga basi alikuwa amenipapasa tu!!
Nikahaha huku na kule!
Sikuupata mlango hata nilipofanikiwa kuzurura kila kona!!!
MARA KIZA !! NILIPAGAWA

Niliita jina la Jesca, ni huyu aliyekuwa ndugu wa pekee katika himaya yangu kwa wakati ule, ningeweza kuita mama lakini mama huyo alikuwa amenimwagia laana tayari, mzee Matata ambaye alikuwa ameniajiri sijui kama ndo huyu alikuwa ameniweka katika himaya hii ya kutisha ama vipi? Nilikosa majibu mara nikauona mkoba wangu upesi nikaupapasa na kukutana na simu yangu ya mkononi, nikaichukua upesi nikataka kupiga, nikakutana na neno ‘insert sim card’, nikajiuliza ni muda gani niliitoa kadi yangu ya simu!! Sikukumbuka hata kidogo!!....mwandishi kuna wakati niliwahi kuombea kifo lakini hapa nilikiogopa sana, kifo cha kufa kimateso namna ile, haikutamanisha hata kidogo kuwatazama watu wale waliokuwa kando yangu!! Bila shaka kabla ya kuwa vile walipitia magumu sana!!!........” Nadia akanyamaza kisha akaangaza huku na kule. Kisha akaniambia, “Tutelemke chini tukanunue maji nina kiu sana.” 
Nikavaa makubadhi yangu nay eye akajitanda kiremba chake tukafunga chumba na kutelemka chini!!! Huku nikiwa nina wahka wa kujua nini kilijiri??? USIKOSE SEHEMU YA 16




Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Dah!! Inasisimua sana, dada della uwe unaweka hadithi hii hata mara 3 kwa wiki, inasikitisha sana

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom