Jumanne, Novemba 25, 2014

SIMULIZI YA MAISHA "USILIE NADIA SEHEMU YA 24"


ILIPOISHIA
“Kwani bila haya mambo huyu mtoto ungempata mbona unaleta mambo ya kitoto kama umezaliwa jana.” Aliniambia kwa jazba. Sasa alikuwa akinizongazonga kama anayelazimisha.
“Sikia Mariam, kwani wewe unataka shilingi ngapi? Sema nikupe!!!”
“Rama sihitaji chochote kutoka kwako, mimi sio changudoa, sijiuzi Rama.” Nilijitahidi kuwa mstaarabu lakini bado haikuwezekana.USIKOSE SEHEMU YA 24

INAPOENDELEA 
Mara Rama akaniachia, akaenda katika kiti kilichokuwa wazi pale chumbani, chini ya kiti akatoka na kibegi kidogo, akakifungua. Akatoka na mabulungutu ya pesa.
“Tatizo unanichukulia poa sana Mariam, haya sema unataka shilingi ngapi unipe.” Aliniambia huku akitoa noti nyingi na kunirushia pale kitandani.

 Ni kweli nilikuwa nahitaji sana pesa lakini sikuwa tayari kuwa mwepesi kiasi nkile, Rama alitaka kunidhalilisha na alikuwa anataka kuyafanya hayo katika mwezi mtukufu. Hakika nilikuwa na dhambi nyingi lakini sikutaka kumwingiza Rama katika dhambi ile ya kuzini katika mwezi mtukufu.



“Rama ….SITAKI!!” sasa nilimwambia kwa ukali.

“UTATAKA!!” alinikaripia na sasa alinikamata kwa nguvu. Rama alikuwa na nia ya kuniingilia kwa nguvu. Sikuwa na msaada zaidi ya mwanangu pale kitandani. Rama alikuwa na nguvu sana lakini nilijilazimisha nikafurukuta huku na kule kumwepuka, mbaya zaidi nilikuwa nimelala na nguo ya ndani pekee.

Mara Rama akaruka chini na kutua katika kibegi kile akakipapasa huku na kule,  akachomoka na bisibisi.

“Ukijifanya mjanja Mariam nakuchomachoma tumboni.” Alinitisha na hakuonekana kutania, karipio lake likamshtua Jonas, akagutuka kutoka usingizini, akabaki kushangashangaa. Rama hakuonyesha kushtuka wala, akaendelea kunisogelea. Hakika alikuwa amenuia kunifanyia kitu kibaya.

“Haya Rama nimekubali.” Nilisalimu amri, nikanyanyua mikono juu. Na hapa Rama akafanya kosa ambalo wanaume wewngi hulifanya na kisha kuukosa hata muda wa kujuta.

Kosa la kumwamini msichana upesiupesi!! Rama akaweka bisibisi chini kisha akatoa nguo zake, akabaki kama alivyozaliwa, akanisogelea na mimi ili aweze kunitoa nguo yangu iliyobakia, nikamruhusu akanisogelea. Lakini akili ikiwa haijakubali kudhalilishwa mbele ya mtoto wangu JONAS……

Rama akawa ananivua huku akininong’oneza maneno ya kimapenzi. Alipopanda kitandani nikapata fursa ya kufanya nilichokiota. Kabla ya kukifanya nikamshukuru Mungu kwa sababu ananipa akili mara kwa mara na huku akinipa nafasi moja tu ya kufanya maajabu.

Upesi nikamkumbatia Rama kimahaba, akajua nimekolea halafu sekunde hizohizo nikamgeuza yeye chini mimi juu. Halafu mwisho nikamrusha kwenda sakafuni nikiwa juu yake. Kichwa chake kilitua katika marumaru ya pale chumbani. Rama hakupiga kelele na ule ulikuwa mwisho wa ile jeuri yake, na hapo nikashuhudia damu zikimchuruzika kutoka katika kichwa chake na kutapaka kwa haraka sana.

Nikamnyakua mwanangu na kuanza kushuka ngazi kuelekea chini. Nilishuka kwa mwendo wa kasi na sikukumbuka kama ile ilikuwa ghorofa ya kumi juu, ajabu sasa sikuchoka wala kupata dalili ya kuchoka.

 Nilipofiuka ghorofa ya pili kwenda chini nikakumbuka jambo la msingi zaidi.

Pesa!! Yule mtu niliyemuacha anavuja damu pale chini alikuwa na pesa. Hapo hapo nikageuza na kupanda kazi, Jonas alikuwa analalamika lakini sikujali. Nikarejea kule chumba kwa tahadhari kubwa, nikaingia na kuchukua lile begi. Kwa mwendo wa haraka tena nikaanza kushuka zile ngazi, G nikikwambia kuwa huyu muhudumu aliyekuja kutuhudumia ni mzembe naomba uniamini, sawa baadaye niligundua kuwa nilichoka sana lakini cha muhimu ni kwamba nilishusha nikapandisha na nikashusha tena.

Mapokezi nilimkuta yule msichana wa mapokezi amelala, mlango ulikuwa umefungwa.

Nikamwamsha akaamka na kuniuliza kulikoni saa tisa usiku nahitaji kutoka.

“Nimegomaba na mpenzi wangu…hivyo tu..sitaki kuwa hapa tena.” Nilijibu kiujasiri. Akajizoazoa taratibu, nilitamani kumtusi lakini ningezua mengine na kumjengea wasiwasi, mwisho akanifungulia mlango nikatoka nikiwa na Jonas wangu mikononi. Na begi la pesa likiwa pamoja nasi.

Nikachukua taksi na kumuamuru dereva atupeleke Mbezi ya Kimara. Nikapekua lile begi nikavuta noti ya shilingi elfu kumi.

Nikampa dereva akakanyaga mafuta gari ikatoweka. Barabara ilikuwa tupu hadi tunafika Mbezi mwisho. Nikashuka bila kuonyesha wasiwasi wowote, na hapo nikaangaza huku na kule nikaona kibao kinachoonyesha nyumba ya kulala wageni, nikajongea huku nikitembea kijasiri sana.

Bahati ikawa upande wetu tena tukapata chumba, nikawalipa tukakabidhiwa chumba chetu. Humo ndani hata Jonas naye hakutaka kulala alikuwa na furaha sana na alikuwa akichekacheka, amakweli pesa sabuni ya roho.

Nikahesabu mafungumafungu yote ya pesa na kufanikiwa kiwepesi kugundua kuwa jumla ilikuwa takribani milioni moja na laki tano.

Katika mahesabu hayo juu palikuwa na kikaratasi, kilikuwa na namba ya akaunti.

Jina lilikuwa la kampuni ya yule mfadhili wangu wa kutoka Mbeya!! Nilijisikia vibaya sana kwa kuwa zile pesa zilikuwa mikononi mwangu na ikiwa ni hasara kwa mtu aliyenifadhili, hapohapo nikajisafisha na kudai kuwa mimi si mkosefu wa kulaumiwa ni Rama.

Nililala nikiwa nimelikumbatia lile begi imara kabisa mikononi mwangu.

Asubuhi saa kumi na mbili nilimchukua Jonas mgongoni mwangu na kuondoka kuelekea barabarani ambapo tulisubiri mabasi yaendayo Mwanza yenye utaratibu wa kuchukua abiria barabarani.

Naam! Nikapata basi mimi na Jonas tukaingia humo na bahati nzuri zaidi tukapata nafasi ya kuketi. Nilikuwa nimeandaa pesa ya nauli tayari tayari hivyo sikulifungua tena lile begi.

Safari ikaendelea ya kuliacha jiji la Dar es salaam. Nilifumba macho yangu na kuduwaa ni kwa namna gani maisha yanaenda kasi namna ile, ndani ya juma moja tu yalikuwa yametokea mambo mengi sana katika maisha yangu. Nilikuwa nimepigana na familia ya mzee Aswile, nilikuwa nimekutana na mchungaji mnafiki Stephano, nilikuwa nimeponea tundu la sindano kukamatwana polisi, nililala nje jijini Mbeya, nilikutana na mkurugenzi wa mabasi na nilisafirishwa kuja Dar, nimekutana na Rama na tumefarakana nikamsukuma chini, sasa nina pesa nyingi na nipo safarini kuelekea jijini Mwanza. Safari ambayo sijui kwa nini naenda huko lakini ndo mji pekee ambao ulikuja ghafla katika kichwa changu. Wewe G wewe hivi unataka shida yako nisile chapatti zangu ama, mwee!! Nina njaa mwenzio tena nina njaa kweli.” Nadia alisema haya huku akifungua chupa ya chai, kisha akamimina katika vikombe vyote viwili, na hapo tukaanza kushughulika na mambo ya chai. Simulizi ile ikakaa kando.



****



“Kuna wanadamu wenyewe wameumbwa wakiwa na huruma tu, wameumbwa wakiwa na mioyo ya kujitolea tu, wana maisha magumu lakini wanapoweza kujitolea wanajitolea. Wanadamu kama hawa ni wachache sana, yaani wenyewe hali haziwabadili maana walipewa mioyo ya uaminifu, hakika uaminifu unaweza kumponza na kumpoteza kabisa mtu lakini hawa hawataki kujua kuhusu hayo kabisa.” Nadia alianza tena kusimulia baada ya kumaliza kunywa chai.

“Nilipofika Mwanza niliuhesabu kuwa mkoa ambao ulikuwa mbaya sana kwangu na mkoa ulionipa machungu mengi, lakini bado ilikuwa lazima nipite hapo ili niweze kufika mkoani Mara, wilaya ya Musoma. Kama kawaida tena nililala nyumba ya wageni, asubuni sana nilikuwa macho, kutazama saa ukutani ilikuwa ni saa kumi na moja na nusu.

Kuna mtu nilimuwaza kabla sijalal usiku uliopita hivyo nikaamua kwenda kumtafuta. Nilipenya huku na kule hadi nikaifikia nyumba aliyokuwa amepanga wakati ule. Nilikuwa na mashaka sana kuwa huenda aliwahi kuhama hivyo nilifanya kama kubahatisha.

Ajabu nilimkuta akiwa anaishi pale pale, niligonga mlango wake akaufungua, mwanzoni hakunitambua lakini baada ya sekunde kadhaa akanitambua. Akanirukia kwa nguvu na kunikumbatia, hakuamini hata kidogo kama ni mimi nilikuwa mbele yake. Huyu alikuwa ni yule dada ambaye wakati nikiwa baamedi niliwahi kuishi kwake, na ni huyu aliyekuwa wa mwisho kuniona jijini Mwanza wakati ule nikikabiliwa na kesi ya kumuua bosi wangu. Hata nilipoishi na Jesca kwa wiki kadhaa kabla hajanisaliti na kujikuta akiingia safari nyingine nami nyingine sikupata nafasi ya kwenda kuonana na dada yule. Lakini sasa alikuwa mtu wa muhimu sana kwangu.

Akanisikiliza vyema nikamueleza juu juu shida zangu, kubwa zaidi ilikuwa juu ya Jonas, nikamweleza kuwa nahitaji kuwa huru kiasi fulani katika kuzikabili changamoto kadhaa za maisha yangu kwa takribani siku kumi tu hivyo nilihitaji sana Jonas abaki naye pale halafu nikirejea nitamchukua. Yule dada hakupinga japo alijaribu kunieleza ugumu wa maisha alionao kwa kipindi kile, alikuwa hana kazi na aliishi kwa kubangaiza bangaiza hivyo hofu yake kuu ilikuwa ni kwa namna gani ataishi na Jonas. Nikakumbuka ile siku ananipatia shilingi elfu ishirini nikiwa naenda Musoma, alikuwa mpole na mwenye huruma na hata sasa alikuwa katika hali hiyo, huu ukawa wakati wangu wa kumwachia chochote kitu, nikajipekua katika ule mkoba nikatoa shilingi laki tatu na kumpatia kama matumizi, hakuamini kabisa akakodoa macho lakini nikamwondoa mashaka, nikamweleza kuwa naenda kufuatilia mali zangu nilizodhulumiwa Musoma.

Baada ya makubaliano  nikambusu Jonas shavuni, na kumpa yule dada mkono wa heri tukaagana.



Majira ya saa kumi na mbili asubuhi hiyohiyo nilikuwa katika basi kuelekea Musoma. Sasa sikuwa na uoga tena moyoni, nilikuwa na kiasi cha pesa ambacho niliamini sitapata shida Musoma kwa namna yoyote, safari nzima niliwaza ni adhabu gani ambayo Desmund anayejiita muheshimiwa diwani anastahili, nikamuwazia pia mzee Matata ambaye alikuwa mtuhumiwa wangu wa kwanza kumuhisi kuwa alinbitupa katika domo la mamba na nikaokolewa kimiujiza. Huyu kama angekiri ni yeye ni hapo ningejua nini cha kumfanya.

 Nilipofika Musoma nilinunua wigi jeusi na miwani nyeusi vilevile, nikaliweka kichwani, kisha nikaanza kutembea kwa kujiamini kabisa, sikutaka kulala kabisa, nikazunguka huku na kule hatimaye nikapata magari ya kukodisha. Tatizo lilikuwa moja sikuwa na mdhamini wa kuniwezesha kupewa gari lile mimi kama mimi, hivyo nilitakiwa kuwa na dereva wao ambaye atakuwa nami kila kona. Jambo hilo sikulitaka hata kidogo, nilihitaji kuwa peke yangu.

Nikaamua kuachana na magari ya kukodi, nikaamua kwenda moja kwa moja jirani na duka kubwa la mke wa Desmund, pale dukani hakuwepo yeye, nikaenda pale kama mnunuzi wa kawaida tu nikamkuta kijana wa kichaga, nikamchangamkia mara ninunue hiki mara kile ilimradi tu niweze kujua mambo kadhaa ambayo yangeweza kuja kunisaidia baada ya siku chache. Mara akaja mtoto mdogo pale, nikajifanya kustuka.

“Mh!! Mtoto wa muheshimiwa huyu ama…” nilijisemesha kama nisiyekuwa na athari.

“Mtoto wa mheshimiwa shangazi yangu.” Alinijibu bila kutilia maanani anachokijibu. Sikuendelea kuhoji juu ya jibu hilo badala yake nikahamia kwa yule mtoto.

Nikamsemesha semesha huku nikiwa mchangamfu sana na moyoni nikiwa na hasira kali, mtoto akawa ananijibu maswali yangu yote vizuri, akaniambia shule anayosoma akaniambia umri wake na mengine mengi.

Moyo uliniuma sana nikajisikia aibu kuu, kumbe Desmund alikuwa ana mtoto wakati nipo naye katika mahusiano, Desmund hakujali hata kidogo kilio changu juu ya lini tutapata mtoto wetu, kumbe nd’o maana alikuwa mwepesi kunibadilikia, kunipiga na kunisulubu awezavyo! Kumbe tayari ana mtoto wake wa kumzaa, hakika niliumia sana. Lakini mbele ya yule mtoto sikuacha kulitoa tabasamu langu.

Baada ya kulipia vikorokoro nilivyovinunua niliondoka pale.

Nikatafuta chumba nikajipumzisha huku nikiufikiria unyama wa Desmund ambaye anaheshimika kabisa kama diwani wa kata yake. Diwani mwongo, mtesaji na muuaji kabisa.

Desmund asiyejua uchungu wa mwenzake bali kujali masilahi yake, mwanaharamu kabisa asiyekuwa na chembe ya huruma wananchi wakamchagua aiongoze kata yao tena baada ya kumuua aliyekuwa diwani mtiifu.

Siku nzima sikutia chochote mdomoni, hivyo usiku huo nilijilazimisha kuonja chakula, kisha nikalala, kama kawaida begi langu likiwa kitu cha muhimu zaidi.

Siku iliyofuata majira ya saa nne nilikuwa nimechanganyikana na watoto wadogo wa shule fulani hivi ya mtu binafsi. Nilikuwa nawauliza maswali kadha wa kadha na kisha huku nikitazama huku na huko kama nitaweza kuiona damu ya Desmund.

Naam! Nikafanikiwa kumuona yule mtoto, uzuri wa watoto akishakuamini mara moja basi yatosha. Aliponiona akanikumbuka na kunikimbilia akiwa na wenzake, nikawapa senti kidogo kisha nikabaki na yule mtoto peke yake. Ili kuondoa utata nikaenda katika uongozi nikajitambulisha kama shangazi yake na yule mtoto ambaye aliniambia kuwa alikuwa anaitwa Desmund Juniour. Jina baya kupita yote katika akili yangu.

Walimu hawakuwa na shaka nilipowaeleza naenda kumnunulia chai mara moja, kwa sababu mtoto mwenyewe alionyesha kunijua basi hawakuwa na swali.

“Mama yake leo amechelewa kweli huwa hakosi kupita au ndo amekuagiza.” Mwalimu mmoja aliniambia.

“Hapana nadhani ametingwa tu maana yule dah simuwezi.” Nilidanganya na upesi nikaondoka na yule mtoto, nikiwa katika tahadhari kubwa maana kauli ya kuwa mama mtoto huwa anakuja mida kama hiyo ilinishtua.

“Gari ya mama ileee.” Tukiwa nje yule mtoto alinionyesha kwa kidole gari iliyokuwa inaingia pale shuleni. Akimaanisha ni ya mama yake, nikazidisha mwendo na kukata kona mbili tatu. Sikutaka kupoteza muda zaidi, nikafanya nilichopanga, nikampa yule mtoto pipi, akaidaka na kuitupia mdomoni, baada ya dakika ishirini nilikuwa nimetoa kanga na alikuwa mgongoni kwangu kama mwanangu wa kumzaa vile amelala hoi. Hatua ya kwanza ilikuwa imefanikiwa kwa kiasi kikubwa.USIKOSE MWISHO WA SIMULIZI HII

Maoni 1 :

Bila jina alisema ...

Jamani..Adela nna ombi moja. Naomba usikawie kuweka kwani tunakuwa tunasahau za nyuma. Hata hivyo ubarikiwe sana.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...

share bottom